TUTARUDI NA ROHO ZETU? (10)


 ILIPOISHIA...............................

“Nataka tumwone mpenzi wako anavyokufa au alipofia,” alimweleza, tabasamu la kifedhuli likiyasindikiza maneno yake. “Keti tafadhali. Keti ili uone kwa starehe.”

KIOO kilionyesha vyumba mbalimbali ambavyo vilijitokeza na kupita. Kila chumba kilikuwa na vitu mbalimbali vilivyoyavuta macho ya Nuru. Lakini ilielekea kuwa havikuwa vyumba Von alivyovihitaji. Aliuendesha mtambo huo harakaharaka kwa kubonyeza kidude hiki na kile kama karani anayepiga chapa. Mara kilitokea chumba ambacho Von alikuwa akikitafuta. Katika chumba hicho, ambacho kilionekana kidogo, walikuwemo watu wawili waliokuwa wakipigana. Mmoja hakuwa mtu bali jitu. Lilikuwa pande la mwanamume, refu, nene, jeusi lenye magumi manene na macho ya kutisha. Lilikuwa likipigana kwa maguvu yote katika hali ambayo ilionyesha kuwa lilikusudia kuua kwa mikono. Jitu hili halikuwa na dalili yoyote ya uchovu wala maumivu yoyote. Kinyume kabisa cha mtu wa pili ambaye lilikuwa likipambana naye. Huyu alikuwa kijana wa kizungu, mwenye dalili zote za ushujaa na ufundi wa kupigana ngumi na karate. Lakini ufundi wake haukuwa na dalili yoyote ya kuonyesha kulishinda jitu hili kwani tayari kijana huyo alikuwa akivuja damu hapa na pale katika majeraha ya kutisha, huku akiwa na dalili za uchovu mkubwa.

SASA SONGA NAZO....................

“Unaona?” Von alisema akicheka. “Mpenzi wako yuko mashakani. Wakati wowote ataaga dunia. Hajatokea binadamu aliyewahi kumshinda Toto na kukivuka chumba kile akiwa hai.”

“Kwanza Nuru hakuelewa. Kisha akaelewa. Kijana wa kizungu aliyekuwa akipambana na jitu hilo la kutisha hakuwa mwingine zaidi ya Joram Kiango, akiwa bado katika hali ya Uzungu bandia. Moyo ulimdunda Nuru kwa hasira kuona akiwa ameketi hapa, juu ya kiti cha starehe, hali Joram anateseka peke yake. Akamgeukia Von kutazama uwezekano wa kumwua na kwenda kumsaidia Joram Kiango. Alikutana na macho makali ya Von ambayo yalimtazama katika hali ya kuyasoma mawazo yake kinaganaga. Bastola yake ilikuwa imara mkononi, ikimwelekea Nuru kifuani. Nuru hakuwa na la kufanya zaidi ya kuyarejesha macho yake katika screen na kulitazama pambano hilo lilivyokuwa likiendelea. Kichwani alikuwa akijiuliza kwa mshangao ni jitu la aina gani hili, kubwa kupindukia, jeusi kupindukia lenya nguvu kupindukia ambalo, badala ya kutumia maguvu hayo kupambana na utawala dhalimu wa makaburu bado, linawatetea kiasi hiki?

Alijilazimisha kutulia na kuendelea kulitazama pambano hilo la kutisha. Joram alibadili mbinu mbalimbali, akikwepa kiufundi karibu kila konde lililotupwa na jitu hilo, pamoja na kulipachika makonde mazito. Lakini haikusaidia. Joram hakuweza kupita chumba hicho kukiendea chumba cha pili ambako angeifikia mitambo aliyokusudia kuilipua. Kwa muda, Nuru alimwona Joram kama mtu aliyekata tamaa, akifikiria kuitumia bastola yake ambayo bila shaka ingewaweka tayari wahandisi aliokuwa akiwanyatia au kurudi alikotoka. Hapana, alimwona vizuri zaidi. Joram alikuwa akiwaza kwa makini huku akilitazama jitu hilo ambalo lilitulia kimya, likimsubiri kwa utulivu kama ambalo halikuwa na uhusiano wowote na matukio yote yaliyokuwa yakitendeka. Baada ya kulitazama sana jitu hilo Joram alifuta jasho na damu iliyojaa usoni mwake na kutamka maneno fulani ambayo hayakuwafikia Nuru na Von. Alitamka neno jingine.

Jitu hilo lilitulia kama lililosikia lugha yoyote ya dunia. Joram alipolisogelea hatua moja lilikaa tayari kwa mapambano. Aliposogea hatua ya pili lilirusha ngumi nyingi mfululizo. Joram akarudi nyuma na kuangua kicheko. Kicheko chake kilipokelewa na Von Iron ambaye alikuwa akilitazama pambano hilo kwa furaha. “Naanza kumheshimu mpenzi wako. Tayari amegundua kuwa hapigani na binadamu wa kawaida.”

Nuru alijikuta akijiuma mdomo kwa hasira. Kwa nini muda wote huo alikuwa hajagundua hilo? Joram alikuwa hapambani na binadamu. Alikuwa akipambana na jitu lililoundwa kwa mkono wa binadamu katika umbo la binadamu, yaani robot. Aliwahi kusikia kuwa matajiri wengi wamekwishaanza tabia ya kuyaweka madude haya kama walinzi wao badala ya binadamu wa kawaida ambaye hutokea siku akakukimbia au kukugeuka.

“Sasa tuone atafanya nini,” Von alikuwa akisema.

Nuru aliyafuata macho yake kumtazama Joram ambaye alionekana akiacha kujisumbua kupambana na jitu hilo na kuchungulia kwa makini, alifunua hiki na kile. Pilikapilika zake hizo zilimwezesha kufunua mahala ambapo kulikuwa na waya ainaaina hadi alipoona jitu hilo likijiweka sawa kama askari katika gwaride. Kisha lilianguka kifudifudi. Nuru alishangilia kimoyomoyo. Kwa mshangao alimwona Von akishangilia vilevile. “Ana akili. Amegundua kuwa dude hilo linaendeshwa kwa nguvu ya sumaku ya umeme ambayo mitambo yake iko pale alipofunua. Ana akili…” Von alisema katika hali hiyo ya kushangilia. Alizidi kucheka. Nuru alizidi kushangaa kwa kutomwelewa hadi alipoongeza, “Ana akili ndiyo. Lakini zitamsaidia nini? Kwa kweli, jitu lile lina huruma sana. Muda wote huu lilikuwa likimrudisha kwa makonde ili asiende kujiua mwenyewe. Sasa mtazame. Ona mpenzi wako anavyojiua… Ona…”

Roho ikiwa juu Nuru, hakuwa na la kufanya zaidi ya kutazama. Alimwona Joram akitazama saa yake na kuanza mwendo wa haraka kukiendea chumba alichokuwa akikihitaji. Mwendo wake ulikuwa wa hadhari na uhakika, macho yakiwa wazi, mikono tayari kwa lolote ambalo lingetukia. Mara aliufikia mlango wa mwisho, uliomtenga na lengo lake. Alinyoosha mkono na kugusa kitasa. Papo hapo ardhi miguuni mwake ilifunuka na Joram kudidimia ghafla. Juhudi zake za kushika kando hazikuzaa matunda yoyote. Ardhi ilijifunika kama ilivyokuwa na Joram kupotea kama ndoto iliyofikia ukingoni.

“Tayari…” Von alichekelea.

Nuru alijikuta yuko wima mbele ya Von akinyoosha mikono kumpiga huku akifoka, “Yuko wapi Joram? Sema yko wapi?”

Pigo la kitako cha bastola ambalo lilitua barabara kichwani mwake lilimpoteza fahamu. Fahamu zilipomrudia alikuwa amelazwa chali juu ya kochi alilolikalia awali. Alikuwa uchi kama alivyozaliwa, mavazi yake yaliyochakaa yakiwa yametupwa kando. Von alikuwa kaketi palepale alipokuwa, sigara mdomoni. Macho yake yalimtazama Nuru kwa namna ya mtu aliyekuwa ameikata kiu yake ya muda mrefu. Nuru alimtazama kisha akajitazama na kuona alivyochafuka. Hakustahimili. Aliinuka na kumwendea Von kwa nia ya pambano jingine. Lakini hakumfikia. Hatua mbili alizozipiga zilimfanya ashindwe kuendelea na badala yake kuanguka sakafuni. Hata hivyo, mdomo haukuwa na udhaifu kiasi hicho.

“Wewe ni mshenzi kuliko washenzi wote niliopata kuwaona,” alifoka. “Mwanaume hayawani… Haya unasubiri nini? Niue kama ulivyomwua Joram. Niue…”

Von alitabasamu kifedhuli. Kitendo cha mapenzi ambacho kilimchukua dakika moja, Nuru akiwa hana fahamu, kiliupa moyo wake faraja kubwa. Hakutegemea. Mara akawa ameelewa kisa cha baba yake kupoteza maisha kwa ajili ya msichana mweusi. Hata hivyo, baada ya kuionja ladha aliyohitaji sana alianza kuiona athari ya kumwacha kiumbe huyo aendelee kuwa hai. Mapambano aliyoyaona baina ya Joram na robot yalikuwa yanatosha kabisa kumwonyesha watu hawa walivyo wapiganaji wasiokata tamaa. Joram amekwisha, lakini huyu japo ni mwanamke yungali hai, na anaweza kufanya lolote. Kifo cha haraka alichokidai kilikuwa halali yake kabisa.

Hata hivyo, angehitaji kumwona akifa kwa mateso zaidi. Angependa kuona tena anavyotaabika kushuhudia mji wao mashuhuri wa Dar es Salaam unavyoteketea. Angependa kuuona uso wake ukijaa hofu na majonzi kama ulivyofanya wakati Joram alipokuwa akiadhibiwa na robot Toto, na hasa pale alipodidimia ardhini.

“Ungependa kufa sasa hivi au baadaye kidogo?” aliuliza bila mzaha wowote katika sauti yake. “Saa moja na dakika chache baadaye kioo, ambacho kilikuwa kikionyesha mchezo wa ngumi baina ya mpenzi wake na Toto, kitaonyesha mchezo wa kupendeza zaidi. Jiji lenu la Dar es Salaam na miji mbalimbali ya Tanzania na nchi nyinginezo, litapata sura mpya, sura ya kupendeza. Natumaini ungependa kuliona hilo pia kabla hujafa ili upate habari ambayo utamsimulia Joram huko kuzimu alikotangulia.”

Nuru, nguvu na fahamu zikizidi kumrejea, aliufurahia uamuzi wa Von. Aliyakumbuka maneno fulani ya Joram, kati ya mengi aliyokuwa akimpa, aliposema: katika mambo haya, kila dakika ambayo inaweza kukuweka hai zaidi inunue kwa bei yoyote. Aliamua kuafikiana na Von. Wazo hilo hasa lilimjia baada ya kukumbuka kuwa, kama walichofanya ni kitu chenye uhakika, dakika chache kuanzia sasa jiji la Johanesburg litakuwa mashakani na Von atakuwa akisema mengine. Nafasi kama hiyo itakapowadia asingeshindwa kuitumia.

Hivyo, alijifanya mnyonge zaidi. Akajiweka kitini hapo katika hali iliyotosha kumsumbua mwanamume yeyote. Von alikwisha timiza Fula yake ya kimwili kwa Nuru. Hata hivyo, Nuru alijua fika kwamba, kutokana na tabia ya roho ya Fula ya mwanaume; dakika chache baadaye angerudiwa na Fula ileile kwa kiwango kikubwa zaidi.

“Wewe ni mshenzi…” alimchokoza tena ili atazamwe wakati huohuo akiyalegeza macho yake na kuzidi kujiweka juu ya kochi kinamna fulani.

*********

Kitu hiki ambacho asili kiliwekwa baina ya mwanaume na mwanamke, kitu ambacho hakielezekai kikamilifu kwa maneno, kilitimiza wajibu wake. Nuru alibaini kuwa Von na ukatili wake, pamoja na kuamini kwake kuwa ametosheka na kukinai, alianza upya kutaabika. Macho yake hayakuweza tena kutulia, mikono yake ilikuwa haikai pamoja. Alihangaika, akienda hapa na pale na kushika hiki na kile. Tahamaki akawa ameketi kochi moja na Nuru, mkono wake mmoja ukikosa kochi na kuangukia juu ya paja nono la Nuru. “Wewe ni mtu mbaya sana,” Nuru alisema, sauti ikiwa laini, huku akijitia kusogea kando kidogo.

“Sikiliza…”

Nuru alijitia kumsikiliza. Alichofanya hasa ilikuwa kuupima uwezekano wa kumzidi Von maarifa aikwapue bastola yake ambayo ilikuwa imara kama hirizi katika mkono wake wa pili.

Von hakuwa mgeni kwa silaha hii ambayo ilikuwa ikitumiwa na Nuru. Alifahamu fika kuwa msichana huyu alikuwa akitumia mbinu ili ayaokoe maisha yake. Lakini kufahamu huko hakukukata shauku yake ya kutamani tena. Alitamani tena, kwa mara ya mwisho. Nuru angefanya nini? Kama kuna kisu basi Nuru alikuwa ameshika makali yake yeye akiwa ameshikilia mpini. Hata hivyo, alijua kuwa anacheza mchezo hatari, anacheza na nyoka. Haikuwa busara kuchezea roho kando ya shimo la mauti lililowazi kiasi hicho. Ni hilo ambalo lilimfanya aendelee kuishikilia bastola kama roho yake.

Wakati huo Von alikwishaibonyeza mitambo yake ambayo alisema ingemwezesha kuiona setilaiti hiyo ikishuka taratibu toka angani na kuiendea anga ya Tanzania ambapo ingesubiri muda uliopangwa kabla ya kuanza kuachia dhoruba za hewa ambayo ingezusha moto wa kutisha. Katika kioo hicho waliweza kuyaona mawingu mazitomazito yakipita katika kioo. Kisha dude la ajabu likajitokeza. Lilikuwa kubwa, jeusi lenye muundo wa ndege aina ya kunguru. Lilikuwa likisafiri kwa mwendo mkali sana kama linaloifuata televisheni hiyo.

Von aliinuka ghafla huku ameshikwa na mshangao. Aliiendea meza iliyokuwa na chombo chenye vidude vingi alivyokuwa akivibonyeza na kuvikagua kwa makini. Alibonyezabonyeza na kutazama tena katika kioo. Alikuwa kama ambaye hakuyaamini macho yake kuliona dude hilo likizidi kusogea. Mara jiji la johanesburg likajitokeza katika kioo hicho, majumba fulanifulani makubwa yakitoa nuru nyekundu kama gari linaloonyesha linaelekea upande upi. Nuru hiyo ilipokelewa au kujibiwa na dalili hiyo ya moto kutoka katika domo la chombo hicho ambacho sasa kilikuwa kikielea juu ya mji.

Nuru aliyaelewa majumba yote hayo ambayo yalionyesha alama za moto. Ni yale ambayo yeye na Joram walifanikisha kutega vile vigololi walivyovipata kutoka kwa hayati Chonde. Akaitazama saa yake. Ilikuwa ikikaribia muda uleule ambao Joram alikuwa ameviandaa vidude vile kufanya kazi. Alitamani apige ukulele wa furaha. Tangu walipoanza harakati hizo hakuwa na hakika kama walikuwa wakifanya kitu chenye uhakika. Wala hakumwona Joram kuwa na hakika hiyo, pamoja na kufunua majitabu mengi ambayo yalikaribiua kumtia wazimu. Kumbe alijua anachokifanya! Ndoto yake imetukia kuwa kweli.

Wakati Nuru akifanya sherehe hiyo moyoni, Von alikuwa akitaabika kichwani. Hakuelewa kinachotokea. Dalili zilizojitokeza zilikuwa za kutisha kabisa, zisizokubalika. Ilionyesha kuwa wakati wowote mji wa Johanesburg ungekuwa ukiwaka moto, Johannesburg badala ya Dar es Salaam, aliwaza kwa hasira. Haikuwepo njia nyingine ya kufanya zaidi ya kuamuru setilaiti hiyo iharibiwe na kuanguka. Si kitu ikiangukia mji na kuua watu kadhaa. Heri nusu shari kuliko shari kamili. Ni hilo alilokusudia kufanya, kuinua simu na kuwapa wahandisi amri hiyo.

Hilo pia hakuweza kulifanya. Alijikuta akitazamwa na bastola yake mwenyewe, ambayo alihisahau kando alipokuwa akihangaika na mitambo. Bastola ilikuwa imara mikononi mwa Nuru, macho yake yasiyo na mzaha yakitangaza shari. “Pokea chako, mwuaji mkubwa,” Nuru alinong’ona akifyatua bastola.

Kwanza Von hakusikia maumivu. Alihisi kitu kikipenya kifuani na kuupapasa moyo wake. Kisha alisikia moyo ukiwaka moto. Akahisi kifo. Alipiga ukelele wa nguvu akichupa kumwendea Nuru mikono yake ikiwa wazi, tayari kumkaba koo. Lakini Nuru alimwepuka kwa urahisi na kumwongezea risasi nyingine ambayo ilimfumua fuvu la kichwa chake. Akadondoka chini na kulala kwa utulivu kama nguruwe aliyechunwa kwa maji ya moto.

Nuru aliyatazama matokeo ya kazi yake harakaharaka. Akaibusu bastola hiyo. Kisha akafanya haraka kujivika mavazi yake. Baada ya hapo alikimbilia kabati la Von ambalo alilifunua na kuanza kupekuapekua harakaharaka. Alipata alichokitaka. Ilikuwa ramani ya jengo hilo, ikiwa tofauti na ile waliyoitumia awali. Aliisoma himahima, kwa makini, kisha akaiweka mfukoni na kuuendea ukuta ambao ulikuwa na funguo nyingi. Akazichukua na kuziweka katika mfuko wake. Kisha, bastola ikimtangulia, alitoka chumbani humo mbio kama miguu yake ilivyoweza kumruhusu.

*********

 

Kuanguka umbali wa zaidi ya mita ishirini kutoka angani hadi juu ya sakafu ngumu sio mchezo. Bila ya uhodari wake wa karate na sarakasi, kama Joram asingefikia kichwa basi angefikia mgongo na kuvunjikavunjika. Lakini alijitahidi kusahau uchovu na maumivu makali aliyokuwanayo, akaikusanya akili yake pamoja na kubingirika. Hata hivyo, fahamu zilimtoka kwa dakika kadhaa.

Uhai ulipomrudia alifungua macho yake kwa taabu na kutazama pande zote. Aligutuka kujikuta akiwa amelala katikati ya mizoga mingi ya binadamu, baadhi ikiwa mifupamifupa, baadhi ikiwa imevimbiana, mingine ikiwa imeoza kabisa. Mara akapatwa na harufu kali ya kutisha, harufu ambayo iliambatana na mainzi mengi manene ya kutisha, ambayo yalikuwa yakirukaruka katika hali ya kushangilia mawindo haya rahisi. Licha ya mainzi hayo Joram aliwaona panya wakubwa mithili ya paka waliokuwa wakifanya karamu katika miili ya binadamu hao. Panya mmoja alikuwa akipita kumzunguka Joram huku akimtazama kwa namna ambayo ilionyesha kuwa alitamani kuanza kumla akiwa hai bado.

Moyo ulimdunda Joram. Ingawa hakujua au kupata kuhisi hofu katika moyo wake lakini kitu fulani kilimpanda moyoni na kumtia hasira na kichefuchefu. Alihisi kama aliyeruka jivu na kukanyaga moto. Kama kufa kwa nini afe kifo kibaya kama hiki? Afe huku anaona? Huku analiwa na panya? Kwa nini asingeruhusu lile dude limwue?

Kisha alijikaza kiume na kujikongoja kusimama wima. Ilikuwa baada ya kujikumbusha ule usemi wake wa mara kwa mara kuwa “Binadamu hufa kwa uzee, hufa kwa ajali, hufa kwa maradhi. Lakini kuna binadamu ambao hufa kwa uvivu vilevile, hasa katika shughuli hizi za upelelezi.” Wazo hilo lilimtuma aanze kutembeatembea humo akitafuta mwanya ambao ungeweza kumtoa nje ya kaburi hilo.

Alizitazama kuta na kugundua kuwa zilijengwa kwa chuma cha pua, zikiwa kama chumba kirefu chenye upana wa mita kumi kwa ishirini. Akatazama juu, akiangalia uwezekano wa kupanda hadi huko alikoangukia. Ilikuwa ndoto nyingine. Ukuta ulikuwa laini mithili ya kioo ambacho kingemshinda hata paka.

Afanye nini? Aketi kukisubiri kifo? Alijiuliza. Hapana, lazima ajitahidi kutafuta mwanya. Lazima kuna mahala pengine penye mlango unaotumiwa kuwaleta watu hawa kusubiri kifo. Akaendelea kutembea akiiruka mizoga na wakati mwingine kulazimika kukanyaga mifupa. Mainzi na panya vilimwongezea msukosuko kwa kukimbia hapa na pale, bila ya shaka kwa mshangao wa kuona mlo wao ukitembea ovyoovyo kwenda huko na huku.

Joram alichunguza kila ukuta kwa makini. Hatimaye, aliufikia ukuta uliokuwa na mlango wa chuma uliofungwa kwa nje. Alijaribu kuutingisha mlango huo bila ya mafanikio. Ulikuwa mlango imara kama ukuta huo. Akautia mkono wake mfukoni na kuitoa bastola yake ambayo aliilenga mlangoni na kuifyatua. Risasi iliugonga na kuanguka ardhini kama gololi. Hata bomu lisingeubomoa mlango huo, jambo lililomfanya Joram aduwae kwa mara nyingine akifikiri la kufanya.

Mara macho yake yakavutwa na maiti moja iliyokuwa ikitikisika. Akaisogelea na kuitazama kwa makini. Naam, ilikuwa na uhai mdogo mwilini mwake. Miguu yake ilikuwa imekatwa na Joram aliona vilevile kuwa jicho lake moja lilikuwa limeng’olewa. Huyu alikuwa mtu mweupe, kinyume cha wengi ambao walikuwa weusi. Bila ya shaka alikuwa Mrusi.

“Pole,” Joram alimwambia.

“Wewe ni nani?” mtu huyo aliuliza kwa udhaifu.

“Itakusaidia nini kunifahamu?” Joram alimjibu. “Unakaribia kufa.”

Mtu huyo alicheka kidogo kabla ya kujikongoja kusema polepole, “Kweli. Haiwezi kunisaidia chochote. Hata hivyo, naona wewe utakufa kabla yangu. Mwenzio hii siku ya kumi na nne bado naishi.”

Joram hakuona kama kuna umuhimu wowote wa kuendelea kumsikiliza mtu huyo aliyekaribia kukata roho. Lakini hakukuwa na jambo muhimu la kufanya na akaendelea kumsikiliza. Haikuchukua muda kabla hajafahamu kuwa Mrusi huyo alikuwa mmoja kati ya watu wengi waliokuwa wakiuawa kinyama baada ya kushukiwa kuwa walikuwa wakifanya upelelezi dhidi ya utawala wa makaburu.

Pango hili lilichimbwa maalumu kwa ajili ya kuwaangamiza watu hao kwa siri baada ya mateso mengi. Wengi waliachwa na kufa kwa majeraha waliyoyapata, lakini adhabu kubwa iliyowaangamiza ilikuwa njaa.

“Usishanagae,” aliambiwa. “Ni njia pekee ya kutuwezesha kuishi.” Alipomwona Joram akizidi kushangaa aliongeza, “Au unaogopa kula maiti? Sikia, unaweza kunila nikiwa hai. Sina dalili ya kupona. Na ninavyokuona unaonyesha kuwa tuko pamoja katika kupambana na utawala huo haramu. Unaweza kunila ukaishi kwa wiki moja zaidi, pengine mwujiza utatokea nawe ukapona na kuendelea na pambano. Usiogope wala usinishukuru. Wala sitaki kujua wewe ni nani. Haitanisaidia.”

Joram aliona kama angerukwa na akili endapo angeendelea kuketi hapo akimsikiliza mtu huyo ambaye ilikuwa dhahiri kuwa uhai mdogo aliobakiwa nao ulikuwa mdomoni mwake tu. Akaondoka hapo taratibu na kuurudia mlango huo ambao alitulia tena akiutazama kwa makini.

Bado hakujua angeweza kufanya nini kuufungua. Ingehitaji mwujiza. Harufu ya maiti hizo, kelele za panya na mainzi yaliyokuwa yakishangilia bahati zao, vilizidi kumsumbua. Joram alijua kuwa harufu na usumbufu huo vingemwua kabla hajasikia njaa.

Aliutazama tena mlango kwa uchungu na hasira. Akatamani apige magoti na kumwomba Mungu ili afanye mwujiza mlango ufunguke. Hilo hakufanya. Ingekuwa unafiki kwani hakuwa amemwomba Mungu walao kwa kumshukuru kwa miaka mingi sasa. Vipi amkumbuke wakati wa shida? Na vipi ategemee mwujiza mkubwa kiasi hicho wakati enzi ya miujiza ilikwishapita? Hii ilikuwa enzi nyingine, enzi ya kutumia akili na nguvu.

Bado hakuona kama alikuwa na lolote ambalo angeweza kulifanya kujitoa katika gereza hilo kwani kwa kila hali alijiona kama aliyefikia mwisho wa msafara wake kimaisha. Kwa mara ya kwanza alilaani bahati yake.

Si kwa hofu wala uchungu aliyoipata katika gereza hilo ambalo halikutofautiana na kuzikwa hai. Hasa alijilaumu kwa kuikosa fursa ya kujionea kwa macho yake mwenyewe utawala wa makaburu na raia wake watakavyotaabika pindi mitego aliyoitega itakapofyatuka na silaha ambayo waliiandaa kuwateketeza watu wasio na hatia itakapowageukia. Joram, kama alivyo, hakuna ambacho kingemsisimua zaidi ya hilo. Aone macho ya mshangao yanavyowatoka wakubwa wa utawala na machozi yaliyochanganyika na kamasi yanavyowatiririka juu ya mashavu yao meupe. Aone majumba yao makubwa waliyoyajenga kwa jasho la wanyonge yakiteketea na kubomoka kama milima ya barafu. Na hatimaye, aone setilaiti yao ikianguka katikati ya mji wao baada ya mitambo inayoiweka angani kulipuliwa. Ndiyo.

Ni hayo tu aliyoyahitaji Joram. Ni hayo ambayo yalimfanya ayahatarishe maisha yake kwa muda wote huu na hata kumwaga damu isiyo na hatia, ili, afanikishe dhamira yake. Hayo, kuyashuhudia kwa macho yake kungempendeza zaidi ya pesa na kumsisimua zaidi ya starehe. Kwa nini amekuwa hana bahati hiyo? Alijiuliza.

Kisha alimkumbuka Nuru. Kiasi hofu ikamrudia alipojiuliza kama atafanikiwa kunusurika katika mapambano haya. Alikuwa amempa maelekezo yote muhimu na kusisitiza wakati gani aanze safari ya kutoroka zake endapo asingemwona.

Bila shaka hakuna hatakayehangaika kumtafuta msichana mmoja ambaye hana tofauti na wasichana wengine wakati mamia ya watu yakiungua, maelfu yakikimbia kwa fujo na mamilioni yakiwa yamepigwa na butwaa, wakati majumba na viwanda vitakuwa vikiteketea kwa moto mkali ambao mfano wake haujapata kutokea katika historia ya nchi hii na dunia kwa ujumla, wakati chombo kisichoonekana kwa macho ya nguvu ya kawaida kitakuwa kikielea angani; na baadaye kuanguka; nguvu yake inayokifanya kielee angani na za madini inayokifanya kutoonekana zikiwa zimekwisha.

Hapana, Joram hakuona kama Nuru angeshindwa kuitumia fursa hiyo. Bila shaka baada ya kumchanganya kwa hila alipokuwa akimfuata, atayafuata maelezo yote.

Joram asingejisamehe endapo lolote lingemtukia msichana yule na kumpotezea maisha. Licha ya kwamba uzuri wa Nuru haukustahili kuharibiwa kwa mkono wa Kaburu yeyote katili, ushujaa wake ulikuwa nguzo ambayo Joram aliitegemea sana. Yote aliyoyatenda, hekima na juhudi za Nuru zilimsaidia. Mungu msaidie arudi salama, alimwombea.

ITAENDELEA...........................................

Post a Comment

0 Comments