TUTARUDI NA ROHO ZETU? (11)

 


ILIPOISHIA......................

Kisha alimkumbuka Nuru. Kiasi hofu ikamrudia alipojiuliza kama atafanikiwa kunusurika katika mapambano haya. Alikuwa amempa maelekezo yote muhimu na kusisitiza wakati gani aanze safari ya kutoroka zake endapo asingemwona.

Bila shaka hakuna hatakayehangaika kumtafuta msichana mmoja ambaye hana tofauti na wasichana wengine wakati mamia ya watu yakiungua, maelfu yakikimbia kwa fujo na mamilioni yakiwa yamepigwa na butwaa, wakati majumba na viwanda vitakuwa vikiteketea kwa moto mkali ambao mfano wake haujapata kutokea katika historia ya nchi hii na dunia kwa ujumla, wakati chombo kisichoonekana kwa macho ya nguvu ya kawaida kitakuwa kikielea angani; na baadaye kuanguka; nguvu yake inayokifanya kielee angani na za madini inayokifanya kutoonekana zikiwa zimekwisha.

Hapana, Joram hakuona kama Nuru angeshindwa kuitumia fursa hiyo. Bila shaka baada ya kumchanganya kwa hila alipokuwa akimfuata, atayafuata maelezo yote.

Joram asingejisamehe endapo lolote lingemtukia msichana yule na kumpotezea maisha. Licha ya kwamba uzuri wa Nuru haukustahili kuharibiwa kwa mkono wa Kaburu yeyote katili, ushujaa wake ulikuwa nguzo ambayo Joram aliitegemea sana. Yote aliyoyatenda, hekima na juhudi za Nuru zilimsaidia. Mungu msaidie arudi salama, alimwombea.

SASA SONGA NAYO...................

Utulivu aliokuwa nao pindi akiwaza hayo ulimfanya panya mmoja amrukie kifuani na kujaribu kumwuma. Joram alimkwepa na kuliachia teke dhaifu ambalo panya alilikwepa vilevile. Hata hivyo, panya huyo alimfanya ayatoe mawazo yake nje na kuyarudisha katika pango hilo la mauti. Harufu mbaya ya binadamu waliooza ikamrudia tena akilini na moyoni. Akajisikia kutapika lakini akajikaza kisabuni.

 

Kisha alikumbuka kumtupia jicho jingine yule Mrusi. Akashangaa kuona kundi dogo la panya likiwa juu ya uso wake, wakimla. Kwanza alishangaa, kisha akaelewa. Mrusi huyo alikuwa amekata roho! Kichefuchefu kikamrudia tena Joram. Alitamani afumbe macho asiendelee kuona ukatili wa panya hao kumla mtu ambaye dakika chache walikuwa wakizungumza naye, mtu ambaye bila shaka ni mwema sana. Vinginevyo angewezaje kujitolea aliwe akiwa hai? Joram aliuliza.

Ghafla mwujiza ulitokea.

Joram aliuona mlango ukitikisika na hatimaye kufunguka. Yeyote ambaye angeingia Joram alitegemea kumlazimisha ama amwue kwa risasi ama amtoe chumbani humo. Hivyo, alisubiri kwa hamu akitazama kwa makini tayari kwa lolote, heri au shari.

Bastola ilichungulia ikiwa katika mkono wa kike. Ilifuatwa na uso mzuri, wenye jasho na damu. Uso wa Nuru.

“Joram?” alipiga ukelele wa furaha mara alipomwona Joram kasimama kando akimtazama.

“Naweza kuyaamini macho yangu?” Joram alimwuliza akiwa bado amesimama palepale. “Wewe ni Nuru kweli au malaika?” aliongeza.

Hakupata muda wa kujibiwa. Tayari Nuru alikuwa kifuani mwake kamkumbatia kwa nguvu huku akilia kwa sauti ndogo. Wakati ikimpambazukia Joram kikamilifu kuwa haikuwa ndoto – huyu alikuwa Nuru halisi aliyekuja kumwokoa – alianza kuinua mikono yake ili naye amkumbatie. Lakini Nuru tayari alikuwa amejitoa mikononi mwake na kumvuta nje harakaharaka huku akisema, “Twende zetu. Wakati umewadia.”

Joram alimfuata kikondoo.

Wakiwa nje baada ya kupigwa na hewa safi, fahamu zilimrudia Joram kikamilifu. Saa yake ilikuwa imevunjwa katika mapambano na jitu lile, aliitazama ya Nuru na kuelewa kwa nini aliambiwa wakati umewadia. Uhai ukamrudia mara moja rohoni, ingawa kimwili alikuwa bado dhaifu. “Niambie Nuru tafadhali. Niambie, mitego tuliyoitega haijafyatuka tu? Mji haujaungua?”

Badala ya kumjibu Nuru alimwambia, “Sikiliza.”

Kwa mbali mjini kulikuwa na kelele nyingi za hofu. Vilio na milipuko ya kutisha ilisikika kutoka katika kila upande. Walisikiliza kwa nusu dakika, kisha Joram alitabasamu na kusema polepole, “Nadhani inatosha. Wanakufa wenye hatia na wasio na hatia. Sasa iliyobaki ni ile kazi moja ya mwisho. Kuulipua huu mtambo.”

Alimshika Nuru mkono na kuanza kukiendea tena chumba cha mitambo. Nuru, akiwa na ramani halisi ya jengo hilo, alimshauri Joram wapitie wapi. Dakika mbili baadaye tayari walikuwa wamewasili katika chumba hicho.

 

Wahandisi watatu walikuwa chumbani humo, jasho likiwatoka kwa mshughuliko wa kutoelewa kinachotokea, hawakuweza kuwaona Joram na Nuru walioingia ghafla. Walipotanabahi walikuwa wakitazamana na bastola mbili. Wakaduwaa. Mshangao wao ulikoma pale risasi za mfululizo zilipopenya katika miili yao na kuwafanya waangukiane, damu zikiwavuja.

Joram aliikimbilia mitambo hiyo na kuanza kuikoroga kama alivyokusudia. Alipotosheka aliyatoa mabomu yake ya mkono na kuyatega sehemu mbalimbali za mtambo huo. Mara tu alipomaliza alimshika Nuru mkono na kutoka naye mbio.

Nje ya jengo, kwa mbali, waliona moto mkali uliokuwa ukipaa angani kwa namna ya kutisha. Kisha waliona kitu kingine cha kutisha. Kundi la askari wenye silaha likija mbio kiwandani huko.

Joram aliduwaa kidogo, akijiuliza wafanye nini. Kurudi ndani isingewezekana kwani jumba hilo pia lingelipuka wakati wowote. Na kukimbia ingewachukua hatua chache kabla ya kukamatwa na risasi za askari hao. Lakini Nuru, alijua la kufanya. Alimwongoza Joram katika upenyo alioutumia na Von hadi nje ya uwa ambako walipiga mbio wakitegemea kumkuta rubani akiwemo, ili wamlazimishe kwa bastola kuendeshwa kutoka nchini humo. Hakuwemo. Bila shaka “miujiza” iliyokuwa ikitokea ilimtia kiwewe hata akaondoka zake, au alikimbilia familia yake kwa matumaini ya kuiokoa. Hivyo, kiasi Nuru alikata tamaa. Lakini Joram alimrejesha matumaini alipomwamuru kupanda mara moja. Wakaingia.

Joram alikuwa na ujuzi wa nadharia juu ya kuendesha helikopta. Alilazimika kujikumbusha ujuzi huo kwa vitendo, jambo ambalo liliwagharimu zaidi ya dakika mbili. Wakati huo askari walikwishawaona na kuanza kuwafuata kwa nguvu zaidi.

Askari mmoja aliamua kutokimbia, badala yake aliilenga bunduki yake na kuiandaa kupiga.

Wakati huohuo jambo jingine la kushangaza lilitokea. Jumba hilo, ambalo lilikuwa hifadhi ya mitambo haramu lililipuka kwa mshindo mkubwa. Moto wa kutisha ulipanda juu na kusambaa kote.

Wakati askari hao walipokuwa wakitazama hilo, pia kwa mshangao, helikopta ilikuwa angani. Walipokumbuka kupiga risasi ilikuwa ikigeuzwa kuelekea Botwasana.

*****SURA YA KUMI NA MBILI*****

“… NA kama anafanya mauaji hayo kulipiza kisasi dhidi ya maafa ambayo utawala huu utayafanya katika nchi hii saa chache zijazo, bado si kitendo cha kujivunia sana, kwani haitasaidia kitu,” Kombora alinong’ona. Alikuwa akisema peke yake, akiwa kimya katika ofisi yake.

Hayo yalimtoka mara baada ya kutazama televisheni na kusikia habari za kutatanisha kutoka BBC, bila shaka zikiwa zimekuja kutoka Afrika Kusini bila hiyari ya utawala huo, kwamba Joram alikuwa ametoweka kutoka katika jumba alilowekwa nchini humo. Kwamba mauaji ya ajabuajabu dhidi ya makaburu katika nchi hiyo yalitokea usiku huo. Na kwamba kulikuwa na mashaka kuwa mwuaji au wauaji hao hawakuwa wengine zaidi ya Joram na Kiango na yule msichana anayefuatana naye, Nuru.

Habari hizo, zikiwa zimewasili pindi vyombo vyote vya habari nzito zaidi ya hiyo zilipokelewa kama habari ndogo na kupuuzwa mara moja. Kwa wananchi wa Tanzania na nchi nyingine ambazo zilikuwa mashakani zikisubiri maafa makubwa kwa hofu na mashaka makubwa, walizipokea kwa shangwe na vigelegele kwa dakika mbili tatu, dakika zilizofuata ikawa imesahauliwa. Hofu ikachukua nafasi yake. Wakaendelea kusubiri, kusubiri kifo.

Waumini wa dini walikisubiri kifo katika makanisa na misikitini. Wakristo walichubuka magoti kwa sala ndefu zilizoambatana na vilio. Waislamu walivunjika migongo kwa kwenda rakaa huku wakimlilia Mola. Wasiomjua Mola walikisubiri kwa namana mbalimbali. Wako waliotulia kwa utulivu, wako waliopiga kelele na kuna wachache ambao waliamua kufa wakiwa wamelewa; hivyo, chochote walichokuwa nacho walikitumia kununulia pombe. Watoto ambao walipata hisia fulani kutokana na tofauti katika tabia za wazazi wao walitulia kimya, kwa mara ya kwanza maishani mwao wakionja ladha ya hofu. Hata wanyama wanaofugwa, kama kuku, mbwa, mbuzi na ng’ombe hawakuwa katika hali ya kawaida kwani ilikuwa siku yao ya kwanza ambayo hawakushuhudia binadamu akila mayai, kuchinja mbuzi wala kumkamua ng’ombe.

Jeshi liliwekwa katika hali ya hadhari, tayari kwa lolote ambalo lingeweza kutukia. Lakini kwa vile madhara hayo yalikuwa hayafahamiki yangetokea upande upi, na silaha ipi ingeweza kuyazuia, ilikuwa dhahiri kuwa jeshi hilo lisingeleta upinzani wowote. Ilikuwa kama waliowekwa tayari kusubiri kifo.

Rais na mawaziri wake, pamoja na viongozi wa ngazi za juu katika Chama walijiinamia juu ya viti vyao vya Ikulu. Mengi yalikuwa yamesemwa, mengi yalifanywa, lakini halikuwepo lolote lililoelekea kuwa kipingamizi kwa maafa yaliyokuwa yakiendelea dakika baada ya dakika. Wao pia ilikuwa kana kwamba waliamua kusubiri kifo kwa pamoja. Mara kwa mara walitazama saa zao kisha wakatazamana. Kisha kiongozi mmoja aliinuka baada ya kumnong’oneza jirani yake kuwa anakwenda haja. Hakurudi. Mwingine aliondoka taratibu kwa madai hayohayo. Yeye pia hakurudi. Yuko ambaye alikwenda moja kwa moja msikitini. Kuna aliyekwenda kanisani. Mwingine alikwenda nyumbani ambako aliungana na familia yake, kusubiri kifo.

Tahamaki Rais alijikuta kabaki na Waziri wake Mkuu. Walitazamana kwa muda, kisha mmoja aliyaepuka macho ya mwenziwe, wakizitazama saa zao. Zilisalia dakika tano tu. Wakatazamana tena. Wakazitazama tena saa zao. Dakika tatu… Dakika mbili… mmoja alimsika mwenziwe akiguna. Mwingine aliinuka akiwa kaloa jasho ambalo hakufahamu lilivyoishinda air conditioner ambayo ilikuwa ikifanya kazi kikamilifu. Kisha aliketi tena na kuyafumba macho yake.

Dakika moja…

******

Dakika yoyote kuanzia sasa! Kombora aliwaza akitoka dirishani alikokuwa akichungulia na kukirudia kiti chake. Alikuwa ameamua lolote ambalo lingetukia limkute katika ofisi yake. Hakuiona haja ya ya kutaabika wala kwenda kushuhudia maisha yanavyowatoka wanawe endapo nyumba yake ingetukia kuwa moja kati ya nyumba zisizo na bahati.

Mara mawazo ambayo hakutaka yamjie akilini yakamtoka. Mawazo ya upweke, unyonge na msiba mkubwa, mawazo ambayo yalikuwa yakimfunulia hali ambayo angekuwa nayo endapo ingetukia yeye kuwa mmoja kati ya wale watakaosalimika na familia yake nzima kuteketea. Angeishi vipi bila ya mama watoto wake, yule mwanamke mpole ambaye hajaacha kumwonea haya kwa kiwango kilekile walipokuwa wachumba hadi leo ambapo wamekuwa pamoja zaidi ya miaka thelathini. Angeishi vipi bila ya watoto wake wanne, mmoja akiwa mwanamume ambaye amehitimu Chuo Kikuu na kuajiriwa mwaka jana na wale wa kike ambao wote wameolewa na kumpatia wajukuu watano? Maisha yangekuwa vipi endapo yote hayo yangebadilika ghafla kwa ajili ya ukatili wa utawala dhalimu wa weupe wachache huko kusini?

Kisha alikumbuka saa yake. Dakika kumi zilikuwa zimepita! Hakuyaamini macho yake. Akayainua na kupiga hatua mbili tatu kuliendea dirisha. Akachungulia chini. Mitaa yote ya Dar es Salaam ilikuwa imetulia kabisa. Kelele ndogo zilisikika kwa mbali kutoka katika viwanda kadhaa ambavyo vilikuwa vikiendelea na kazi. Kombora aliirudia meza yake na kuketi. Masikio yake yalikuwa wazi yakisubiri kwa hofu kudaka mlio wowote wa mashaka ambao ungesikika. Macho pia yalikuwa wazi yakitazama angani kupitia dirishani.

Dakika ishirini!

“Wakati wo…” alitaka kutamka. Sauti yake ilikatizwa na ukelele wa ghafla ambao ulivuma ghafla katika anga. Bila ya kutegemea aliyafumba macho yake kwa nguvu na kutamani kuweka vidole masikioni ili asisikie zaidi. Kelele ziliendelea kwa mvumo mkubwa zaidi. Hisia zilimfanya Kombora adhani kuwa zilikuwa kelele za kushangilia badala ya vilio na maombolezo kama alivyotarajia. Akasikiliza kwa makini zaidi. Naam. Watu walikuwa wakipiga vigelegele na kucheka kwa nguvu.

Watu wote!

Kama waliopatwa na wazimu!

Dakika moja baadaye Kombora alikuwa miongoni mwa watu wengine katika chumba cha habari, ghorofa ya mwisho. Askari hao walikuwa wakitokwa na machozi ya furaha huku wakisikiliza redio BBC ambayo ilikuwa ikiendelea na taarifa.

…hadi sasa inaaminia kuwa utawala wa Afrika Kusini haujafanikiwa kuuzima moto huu mkali ambao unateketeza majumba mbalimbali ya mjini johanesburg. Kadhalika, haijafahamika watu wangapi wamefariki na wangapi ni majeruhi japo inaaminika kuwa idadi hiyo itakuwa kubwa sana.

Kadhalika, mtambo wa siri ambao ulikuwa umejengwa na utawala huo ukiendesha setilaiti ya aina yake, isiyoonekana kwa macho, umelipuliwa na wahandisi wake wote kuteketea. Inasemekana kuwa baada ya mtambo huo kulipuka chombo hicho cha ajabu kimeanguka katikati ya mji wa Johanesburg na kusababisha madhara makubwa kwa maisha na mali za wananchi. Kadhalika, inaaminika kwamba afya za wananchi katika mji huo zitakuwa mashakani kutokana na nguvu ya nyuklia zilizoshirikishwa katika kukiunda chombo hicho. Kwa kila hali inaonyesha dhahiri kuwa Joram Kiango alishirikiana na mwenzi wake, yule msichana mzuri, Nuru, wameshiriki kwa njia moja au nyingine katika kufanya haya yaliyofanyika huko Afrika Kusini. Na endapo wasingekifanya walichokifanya dakika hii Afrika nzima ingekuwa katika msiba kwani kulikuwa na mipango ya mtambo huo kuzishambulia nchi zote za mstari wa mbele kwa pamoja…

Kombora hakustahimili. Machozi mengi yalimtoka na kuteleza juu ya mashavu yake, machozi ya furaha. Joram Kiango tena! Kwa mara nyingine ameliokoa taifa lake na Afrika nzima kuepuka kipigo cha kikatili ambacho kisingesahaulika. Joram, ambaye alimfikiria vibaya kwa kutoweka kwake na pesa nyingi za umma ambazo amezichezea duniani kote.

Ghafla, ikampambazukia Kombora. Joram hakuwa ameziiba zile pesa. Alizichukua kwa mtindo ule ili ionekane kama ameziiba ili azitumie kwa shughuli hii pamoja na kuaminika kama msaliti mara aingiapo nchini Afrika Kusini. Angeweza kuchukua hata zote! Kombora aliwaza. Angeweza kuzitumia apendavyo! Kijana huyu ni nani kama sio malaika aliyeletwa kuishi kama binadamu kwa manufaa ya binadamu wengine?

Kombora alirejea ofisini kwake. Mara tu alipoketi simu zilianza kumsumbua. Nyingi zilikuwa za waandishi wa habari zikiuliza hili na lile. Swali kubwa lilikuwa kutaka kujua kama kweli ni Joram Kiango aliyeifanya kazi hiyo ambayo majeshi yote ya nchi za Kiafrika yasingeweza kufanya. Zaidi walitaka kujua Joram yuko wapi.

Simu ambayo ilimsumbua Kombora kuliko zote ni ile iliyotoka Ikulu. Alizungumza na Rais mwenyewe. “Tunamtaka haraka kijana huyu ndugu Kombora. Kuna tuzo maalumu ya ushujaa ambayo inamsubiri…”

Kwa kadri Kombora alivyomfahamu Joram, hakuamini kama angepatikana kwa urahisi kiasi hicho, na hasa kujitokeza aipokee tuzo hiyo hadharani.

Siku mbili baadaye uhai ulilirudia jiji la Dar es Salaam kama kawaida. Pilikapilika za mitaani, viwandani na maofisini ziliendelea mtindo mmoja. Kila uso ulikuwa na furaha, tabasamu likiwa karibukaribu. Jina la Joram lilikuwa katika fikra za kila mmoja. Ambao hawakupata kumfahamu waliuliza huyu Joram ni nani?

“Humfahamu?” waliulizwa huku wakitazamwa kama wapumbavu.

Tawi la Benki ya City Drive lilikuwa na uhai vilevile. Wateja wengi walifurika kama kawaida wakiweka au kuchukua pesa, kuangalia hesabu zao na shughuli nyingine mbalimbali. Pilikapilika hizo ziliwafanya wasimtazame zaidi ya kawaida mzee huyu aliyevaa kanzu nyeupe na koti jeusi, ambaye alikuwa na nywele na ndevu nyingi nyeupe kwa wingi wa mvi. Mkononi alikuwa na mfuko mnene wa ngozi. Aliwapita wateja wote, akipokea shikamoo zake hadi chumbani kwa meneja ambaye alimpokea kwa heshima zote, kwani haikuwa mara kwa mara kutembelewa na watu wenye umri kama huo.

“Marahaba,” Babu huyo aliitikia. “Wewe ndiye meneja mwenyewe?”

“Ndiye.”

“Ndiyo wewe uliyeibiwa zile pesa za kigeni?”

“Ni mimi, mzee.”

“Basi huu hapa mzigo wako,” mzee huyo alisema akifungua mfuko huo na kutoa mabunda ya noti. Pesa za kigeni na shilingi chache za Tanzania. “Nimetumwa na kijana mmoja anayesema anaitwa Joram nikuletee. Amesema nikuombe radhi sana kwa kuzichukua. Alikusudia kuzitumia kwa safari yake lakini alipata pesa nyingine kutoka kwa jasusi moja ambalo alilikamata kule New Africa Hotel. Hivyo, alizitumia pesa zile badala ya hizi. Hata hivyo, amesema zimepungua kidogo atalipa…”

Meneja alikuwa hamsikilizi kwa makini. Mshangao ulikuwa umemshika. Alimtazama mzee huyo kwa muda kisha aliinama na kuanza kuzihesabu kwa mabunda. Katika hesabu ya harakaharaka zilipungua dola mia mbili. Akazirudisha katika mfuko wake na kuinua uso ili amshukuru mzee na kumwambia la kufanya. Hakumwona. Mzee alikuwa ameondoka bila ya kuaga alipokuwa kainamia meza.

Meneja huyo aliduwaa. Kisha alikumbuka la kufanya. Akauchukua mfuko huo wa pesa na kuondoka nao hadi katika gari lake. Akalitia moto hadi katika ofisi ya Kombora ambako alimwona moja kwa moja na kumsimulia mkasa mzima.

 “My God,” Kombora alifoka. “Aliyezileta pesa hizo kwako hakuwa mzee. Alikuwa kijana sana, Joram Kiango mwenyewe!”

Meneja huyo alizidi kushangaa. “Mbona alikuwa mzee, Inspekta? Hata sauti yake ilionyesha…”

“Huyo ni Joram,” Kombora alimkatiza. “Ametumia moja ya mbinu zake ili asipatikane na kupewa heshima yake. Amejifanya mkongwe kama alivyofanya katika mkasa ule ulioitwa Salamu Toka Kuzimu.” Kombora alijiinamia kwa muda. “Tulimhitaji sana,” alisema kama aliyemsahau Meneja huyo wa Benki na badala yake kujizungumzia peke yake. “Anahitajika. Kumtafuta haitasaidia kitu. Kwa jinsi ninavyomfahamu hatajitokeza hivi karibuni hadi hapo mchango wake utakaposahauliaka, au litakapotokea suala jingine linalohitaji ushujaa."

                                                        ***MWISHO****

Post a Comment

0 Comments