ILIPOISHIA.........
Watu hao ambao walikuwa wakitafutwa kwa udi na uvumba,
alfajiri iliwakuta wakiwa wamesimama mbele ya hoteli moja ndogo katika mtaa
uliojaa watu waliokuwa wakijadiliana. Macho yao yaliwatazama raia hao wa
makaburu waliojaa wasiwasi kwa dhihaka. Kadhalika, waliwakebehi askari na poli
ambao walikuwa wakipita huku na huko katika mtaa na vichochoro huku wakiwapita
bila ya kuwatupia macho. Isingekuwa rahisi kwa mtu yeyote kuwashuku kwa
urahisi. Pamoja na kukesha, pamoja na kuchoka kwa kazi ya kwenda hapa na pale
huku wakilazimika kuua na kuua tena, bado walijitahidi kuwa katika hali ya
kawaida kama raia yeyote wa kawaida katia nchi hiyo. Hali ambao ilitokana na
mavazi waliyovaa pamoja na rangi yao.
Yeyote aliyewaona aliamini kuwa alikuwa akiwaona
vijana wengine wa kikaburu. Hayo yalikuwa matokeo ya moja ya shughuli nyingi
ambazo Joram alifanya kwa gharama kubwa sana aliposafiri hapa na pale katika
miji mbalimbali. Alimpata mtaalamu ambaye aliwatengenezea ngozi za bandia
zilizovaliwa usoni, mikononi na kufunika vichwa vyao kwa nywele za kizungu.
Vitu hivyo ni miongoni mwa mali zake ambazo alizisafirisha kwa hila kwa
kumtumia yule Mmarekani Moole.
SASA SONGA NAYO...........
Kwa ujumla Joram aliona kuwa mambo yote yalikuwa
yakienda kama yalivyopangwa, ingawa kiasi yalianza ghafla kuliko alivyotegemea.
Alishtuka sana jana alipoambiwa na yule kiongozi wa BOSS kwamba leo saa nne
wangeilipua Dar es Salaam na miji mbalimbali ya nchi za Kiafrika kwa ile silaha
yao iliyoko angani. Hivyo, hakuwa na simile tena moyoni. Ndipo alipolazimika
kufanya mapenzi ya hali ya juu na Nuru akiwa na hakika kuwa anatazamwa na ule
mtambo wao ambao alikwisha uona. Alifanya hivyo ili kuwapumbaza watazamaji hao.
Baada ya hapo ndipo alipofanya hila kukorofisha mtambo huo. Katika kipindi
hicho cha kutoonekana aliondoka na kupenyapenya kwa hila katika viochochoro
hadi nyumbani kwa Moole ambako alibisha mlango na kufunguliwa na Moole
mwenyewe. Alipoomba mzigo wake Moole alikanusha kabisa kwamba hakuwa amechukua
mzigo wa mtu kama huyo. Lakini ngumi mbili tatu zilimfanya amwongoze ghalani
ambako Joram alimvamia na kumfunga mikono na miguu, kisha akaufungua na
kuchukua vile vitu muhimu tu. Akarudi haraka hadi chumbani kwake ambako,
akisaidiwa na Nuru alipekuapekua na kupata ramani walizoziandaa, pesa na vitu
vingine. Ni wakati Joram alipomaliza kujivisha ngozi hizo zilizomfanya aonekane
kama alivyo sasa, alipoingia yule kachero wa kwanza. Hila aliyoitumia Nuru ya
kujifanya kuwa alikuwa akipambana na mzungu aliyetaka kumnajisi ilimsaidia
sana. Ndipo kachero huyo alipopata kile alichostahili kupata. Nao akafanya
haraka kumsaidia Nuru kuvaa “Uzungu” wake na alipokamilika walivichukua vilivyokuwa
muhimu na kuingia mitaani.
Wakiwa wameikariri ramani hiyo kikamilifu, kazi
waliyoifanya mitaani humo ilikuwa kufuata yale majengo waliyokusudia na kutega
vile vigololi vilivyopatikana kwa Chonde na kuvitegesha katika kipindi cha saa
tatu kamili. Walifanya kazi hiyo kwa ukamilifu kuliko walivyotegemea. Watu
wachache ambao walilazimika kupoteza maisha ni wale walioshuku jambo au
kujaribu kuwazuia kufanya kazi yao. Wakiwa hawajui kuwa wanapambana na nani
watu hao walikufa kwa utulivu kabisa, isipokuwa yule ambaye kifo kilimtetemesha
hata akaamua kuruka dirishani kutoka ghorofa ya nne akiwa na kisu kifuani.
Sasa kazi ya kutega vigololi ikiwa imekwisha, Joram
alimtazama Nuru na kumnong’oneza, “Awamu iliyobaki ni yangu peke yangu. Ni
lazima niingie katika mtambo wao na kuulipua. Nikiweza kuulipua kabla ya
madhara tuliyoandaa katika jiji hili kutokea litakuwa jambo jema sana.
Nikishindwa, mioto itakapoanza nenda pale ambapo nimekuonyesha katika ramani
ukanisubiri.”
“Hatuwezi kwenda wote?”
“Haiwezekani. Tumelijadili hilo mara nyingi sana.” Wakakubaliana.
Kisha Joram akajiingiza miongoni mwa watu waliokuwa
wakipita katika mitaa hiyo, akielekea ilikomwelekeza ramani yake. Mwendo wake
ulikuwa wa haraka na uhakika, ingawa alifahamu kikamilifu ulinzi mkali
uliozunguka mtambo huo. Matumaini ya kurudi yalikuwa ndoto isiyo na hakika.
Hakujali. Asingejali kufa, endapo tu kifo hicho kingetokea baada ya kufanikiwa
kutega mabomu yake katika mtambo huo. Aliamini kuwa Nuru asingeshindwa kurudi
Tanzania katika msukosuko mkubwa utakaoutokea mji huu, saa mbili na nusu
baadaye.
Nuru alimwacha Joram na kuondoka kwa hatua chache. Mara tu alipoamini kuwa asingegeuka tena kumtazama, alianza kumfuata. Hakujua kuwa yeye pia alifuatwa na watu wanne wenye silaha kali mkononi na mioyo yenye hofu na hasira dhidi yake.
MKOBA wake wenye silaha zake zote ukiwa umetulia
mkononi, kwa utulivu na uhakika kama mzigo wowote ambao haukuchukua chochote
cha haja, Joram alipiga hatua moja baada ya nyingine katika mitaa ya mji mkuu
wa Afrika Kusini. Alipishana na wengi akiandamana na wengi wenye misafara yao.
Kitu fulani katika damu yake kilimnong’oneza kuwa
anafuatwa. Hilo halikumshangaza. Tangu alipoachana na Nuru alifahamu fika kuwa
angepinga ushauri wake wa kumsubiri pale alipomwelekeza hadi atakapoimaliza
awamu hii ya mwisho ambayo ilikuwa ya hatari mno. Akiwa ameshangazwa na ushujaa
wa msichana huyu, jinsi alivyokuwa tayari kuihatarisha roho yake kwa hiari,
aliamini kabisa kuwa asingekubali kuikosa fursa hii ya mwisho, fursa ambayo
endapo ingefanikiwa isingefutika katika kurasa za matukio muhimu ya kihistoria
duniani.
Hivyo, hakujishughulisha kugeuka nyuma, kwa hofu ya
kuwafanya makachero, ambao aliamini wamezagaa kote mitaani wakimtafuta,
kumshuku. Badala yake aliendelea na safari yake huku akitafuta nafasi na wasaa
ambao ungemwezesha kumtia Nuru chenga ya mwili. Hakuumaliza mtaa huo kabla
fursa hiyo haijajitokeza. Katika kona ya mtaa huo Joram alikuta mahala
palipokuwa na ajali ya magari matatu yaliyogongana.
Watu wengi walikuwa wamejazana kuitazama ajali hiyo.
Kati yao, Joram aliweza kuona nyuso za watu wenye dalili ya ukachero na
uaskari. Hakuwajali. Badala yake alijitia mmoja kati ya raia waliokuwa
wakiitazama miili ya madereva wawili ambao hawakuwa na dalili ya uhai.
Aliitumia fursa hiyo kutoa kofia mfukoni na kuivaa
kichwani, pamoja na kuyafunika macho yake kwa miwani ya jua. Kisha akajipenyeza
katika kundi hilo na kutokea tayari akiwa amemchanganya Nuru. Hivyo, akaendelea
na safari yake, mluzi mdomoni, tabasamu usoni na hadhari moyoni.
Baada ya mitaa kadhaa aliumaliza mji. Kwa mbali,
aliliona jengo lenye mtambo aliokuwa akiuhitaji. Ili kuthibitisha alitumia hila
kuitazama ramani yake. Hakuwa amekosea. Akaendelea na safari yake akianza
kujikumbusha kwa mara nyingine hila ambazo aliziandaa ili zimwezeshe
kufanikisha jukumu lililokuwa mbele yake. Hakuwa amekosea.
Akaendelea na safari yake akianza kujikumbusha kwa
mara nyingine hila ambazo aliziandaa ili zimwezeshe kufanikisha jukumu
lililokuwa mbele yake. Moyoni alijua kabisa kuwa alikuwa akikaribia mbele ya
domo la mauti lililo wazi. Kuingia ulikuwa wajibu wake, lakini kutoka kinywani
humo akiwa hai ni jambo ambalo hakuwa na hakika nalo.
Hakuogopa. Lakini kutokuogopa hakukumfanya astahimili
kujikuta akitokwa na sala ndefu kimoyomoyo, jambo ambalo hakumbuki kwa mara ya
mwisho alilifanya lini.
********
“Bado yuko mbele yetu mzee…” Taarifa ilimfikia Von
Iron ambaye alitulia katika ofisi yake, mara kwa mara akitazama saa yake ya
mkononi. “… Tufanyeje mzee? Tumuue?” sauti iliendelea.
“Nimesema mwacheni,” Von alinguruma katika walkie
talkie iliyokuwa mbele yake. “Mfuateni hadi mtakapopata nafasi nzuri mumkamate.
Tunamtaka hai.”
“Anaelekea kuwa anaweza kuleta madhara, mzee. Anaweza
kuwa na silaha…” sauti iliendelea.
“Unataka kuniambia kuwa wanaume wanne mnashindwa
kumkamata malaya mmoja tu wa Kiafrika?”
“Sivyo, mzee. Lakini…”
“Lakini nini? Mnachotakiwa kufanya ni kumleta hapa
akiwa hai, ili atueleze wapi alikotorokea Joram Kiango. Mkishindwa kufanya
hivyo nadhani hamtashangaa kwa lolote litakalowapateni.” Alimaliza na kufunga
redio hiyo.
Taarifa ya kuonekana kwa Nuru ilimfikia nusu saa
iliyopita. Fununu iliyosaidia kupatikana kwake ililetwa na mtu aliyefia
hospitali baada ya kuruka dirishani kwa maumivu ya kisu. Kabla ya kukata roho
mtu huyo alifaulu kutamka kuwa aliuawa na msichana wa kizungu mwenye lafudhi ya
Kiafrika. Wakagundua kuwa mafanikio yote ya Joram yalitokana na hila ya
kujifanya mzungu.
Ndipo wakuelekeza upelelezi kwa namna nyingine. Na
haukupita muda kabla hajatiliwa mashaka msichana huyu ambaye alikuwa akitembea
mitaani kwa namna ambayo si ya kawaida kwa wasichana, asubuhi kama hiyo. Mtu
alimsogelea. Akamsalimu. Majibu aliyopata yaliutia kasoro uzungu wake kutokana
na lafudhi. Mwingine alimkaribia.
Akajitia kukosea na kuugonga mkoba wake, kisha
aliinama mbiombio kumsaidia kuuokota. Alishangazwa na wepesi wa msichana huyo
katika kuuokota mkoba huo. Alimtazama vizuri zaidi. Akaona dalili ya Uzungu
bandia katika uso na mwili wake. Ndipo akaandamwa, bila ya yeye kufahamu,
dakika yoyote akiwa tayari kupigwa risasi, endapo Iron angeafiki…
Iron hakuwa tayari kuafikiana na makachero hao
waliojaa hasira na uchu wa kumuua Nuru. Hakuafiki kwa kuwa yeye pia alijawa na
uchu moyoni, uchu wa kumpata Nuru akiwa hai, uchu wa kuonja kile ambacho
aliambulia kukishuhudia kwa macho tu. Ndiyo, kufa, Nuru alikuwa hana budi.
Lakini angeweza kufa baadaye. Hakuiona sababu yoyote ya kufanya haraka.
“Bosi tumeamua kumnasa…” taarifa ziliendelea kumfikia.
“Mkamateni.”
Mara zikasikika purukushaniu katika chombo hicho.
Zilifuatiwa na milio ya risasi tatu. Moyo wa Iron ulidunda kwa hofu.
Asingevumilia endapo msafara wa risasi hizo ungeishia katika mwili wa Nuru
kabla…
“Bosi amemjeruhi mtu wetu… turuhusu tummalize…”
“Nasema mleteni akiwa hai,” Iron alinguruma.
*******
Mara chombo cha mawasiliano kikazimwa. Dakika chache
baadaye mlango wa ofisi ya Iron ulifunguka na kumruhusu msichana ambaye alikuwa
akisukumwa kwa mitutu ya bastola nne kuingia chumbani humo huku akipepesuka.
Alikuwa hai. Lakini jeraha la kisu katika mkono wake wa kulia, kuchubuka
shavuni, na uvimbe usoni, vilidhihirisha kuwa aliupigania uhai wake kwa gharama
kubwa.
“Ameua watu wawili,” kiongozi wa msafara huo alieleza.
“Atajuta…” lilikuwa jibu pekee la Iron.
“Amegoma katakata kuelekeza alikojificha mwenzake.”
“Ataeleza.”
Makachero hao walishangazwa kiasi na tabia hiyo mpya
ya kiongozi wao. Hakuwa Von Iron waliyemfahamu. Von Iron waliyemfahamu angekuwa
wa kwanza kutamka kwa ukali “ua.” Na endapo kifo kisingetokea mapema Von Iron
waliyemfahamu angeshuhudia ukatili wa hali ya juu ukitendeka katika mwili wa
msichana huyo jeuri aliyetisha, hasa jinsi ngozi yake ya bandia iliyobanduka
hapa na pale kwa purukushani na kufanya mabaka ya ngozi yake asilia yajitokeze
kwa namna ya kuchekesha na kutisha kiasi.
“Sikieni,” Von aliwaamuru. “Huyu niachieni mimi.
Nitajua la kumfanya. Fanyeni hivi, endeleeni kumtafuta Joram Kiango. Mkimpata
namtaka vilevile. Hai au maiti. Sawa?”
“Sawa, bosi,” waliafiki wakitoka mmojammoja, baada ya
kutazamana tena kwa mshangao.
Walipobaki peke yao Von Iron alikiacha kiti chake na
kumsogelea Nuru. Akamkazia macho yake makali. Mara alilazimika kuyainamisha
macho hayo mara moja baada ya kuona kitu ambacho hakupata kukiona katika macho
ya msichana yeyote, kitu kisichoelezeka kwa ukamilifu, kitu kama nuru ya aina
yake ambacho kilifunua mapazia fulani na kuacha barabara ndefu inayoelekea
kusikojulikana; kilichomfanya Joram ayaepuke macho hayo ni zile hisia za
kutatanisha ambazo zilimjia ghafla zikimfanya ajihisi kama anayeifuata barabara
hiyo akielekea huko ambako hakujulikana, katika dunia nyingine inayotatanisha.
“Una habari kuwa maisha yako yamo mikononi mwangu?”
Von Iron aliuliza.
Hakupata jibu, jambo ambalo lilimfanya ainue tena
macho na kumtazama Nuru.
Ile nuru ya kutisha aliyoiona awali katika macho hayo
haikuwepo tena. Badala yake alikutana na macho yaleyale aliyoyategemea, macho
aliyotamani kuyaona, macho ya msichana, yenye dalili zote za usichana. Mara
akawakumbuka marehemu wazazi wake. Akakumbuka kuwa ni kitu fulani katika maumbo
ya msichana mweusi kama huyu ambacho kiliwafanya waondoke duniani kwa aibu na
uchungu, kitu ambacho Von alikuwa akikitamani ili akione au kukionja. Leo
ilikuwa fursa ya kipekee. Atamtumia msichana huyu kumfunulia siri hiyo, kisha
angemwua.
“Una habari kuwa maisha yako yamo mikononi mwangu?”
alilirudia swali lake.
Bado Nuru hakumjibu. Aliendelelea kusimama paleplae
alipokuwa, uchovu ukimsumbua, maumivu yakimtesa. Moyoni hasira kali ilikuwa
ikichemka dhidi ya watu hawa. Hakuwa na shaka kuwa maisha yake yalikuwa
ukingoni. Lakini si hilo lililomtia hasira. Hasa alisikitika kwa kule kuona
kuwa amekamatwa kabla ya kazi ya mwisho kukamilika. Japo alikuwa na hakika kuwa
Joram alikuwa hajakamatwa, lakini aliamini kuwa ingekuwa haki yake kushirikiana
na Joram bega kwa bega katika awamu ya mwisho kama walivyofanya katika ile ya
awali. Kiasi, vilevile, alikuwa akijiuliza kama hakuwa amefanya makosa kwenda
kinyume cha matakwa ya Joram na kumfuata kwa siri badala ya kumsubiri kama
alivyoamriwa. Alijuwa wazi kuwa ni kitendo hicho ambacho kilimtia mashakani.
Hata hivyo, hakuwa na hofu kubwa sana juu ya maisha
yake. Hakuamini kuwa kifo kilikuwa karibu kiasi hicho. Mipango waliyoiandaa
ilimtia hakika kuwa ingetokea fursa nzuri ambayo ingempa mwanya wa kutoroka
hadi nchi jirani za mstari wa mbele. Imani hiyo ilijengeka katika moyo wake
mara alipojikuta amezungukwa na askari wenye silaha, lakini wakiwa hawana
dalili ya kuzitumia silaha hizo dhidi yake. Hata baada ya kutoa bastola yake na
kuwaua wawili kati yao walifyatua silaha zao kwa dhamira ya kumtisha tu; akajua
kuwa walimtaka hai ili wamlazimishe kutoa siri fulani. Hivyo, hata alipozidiwa
nguvu, baada ya kuvamiwa na kupigwa sana, hakuwa na shaka sana.
Na hasa huyu mtu mnene anayeonekana kama kiongozi wao.
Huyu ambaye tamaa ya kimwili ilikuwa wazi katika macho yake. Kosa analofanya
huyu la kumtamani lingeweza kabisa kusaidia kuyaokoa maisha yake na ya Joram
Kiango. Alichohitaji ni muda kidogo.
Suala hili la kupendwa au kuhitajiwa kimapenzi
halikumshangaza. Kwa kweli, alilitegemea. Joram alikuwa amemfafanulia hilo pia
walipokuwa wakijiandaa kuingia nchini humu. Alimweleza kwa lugha ya kishairi
akisema “Katika silaha zote za mwanamke uzuri unazitangulia.” Akamweleza
kinagaubaga nini la kufanya. Hata walipokuwa wakifanya mapenzi kitandani, kabla
ya Joram kutumia hila ya kuharibu kile chombo chao cha kutazamia
alimnong’oneza, “Tutafanya kila kitu. Najuwa wanatutazama, usione haya. Nataka
tuwatie homa ili endapo watatukamata, watamani kuyashuhudia waliyoyaona kwa
vitendo. Nafasi ambayo natumaini hutashindwa kuitumia.”
Haya, sasa nafasi hiyo imetokea… Nuru alijiambia
kimoyomoyo. Akayainua macho yake, akayalegeza kidogo, akiruhusu tabasamu dogo.
“Najua kuwa ninakufa…” alimjibu Iron kwa sauti ndogo ambayo masikioni mwa
mwanaume ilitosha kuanzisha kongamano fulani baina ya mwili na damu.
Kufa huna budi! Iron alisema rohoni… utakufa kifo
kibaya. Lakini itakuwa baada!... kwa mdomo alisema, “Nimesema maisha yako yamo
mikononi mwangu. Vitendo vyenu vilikuwa vuya kinyama mno. Pamoja na kupokelewa
vizuri katika nchi hii na kuahidiwa kuishi kwa amani na starehe, bado mmediriki
kufanya mambo yasiyoeleweka. Mnapita kuua watu wasio na hatia bila sababu
yoyote. Naamini huo ni ushauri wa huyu mwendawazimu uliyefuatana naye.
Unafahamu alikokimbilia?”
“Sifahamu…”
“Amekutoroka,” Iron alidakia. “Amekutoroka. Bila shaka
hivi sasa anajaribu kuitoroka nchi. Hafiki mbali. Dakika yoyote ataletwa hapa
akiwa hai au maiti,” alimaliza akimkazia macho Nuru. Macho yake yalikumbuka
alichohitaji. Akazisahau hasira zake dhidi ya Joram na kumnong’oneza Nuru kwa
sauti ambayo kwake ilijaa upendo. “Suala lako ni tofauti bi mdogo. Una nafasi
nzuri ya kusamehewa madhambi hayo iwapo tu… iwapo…”
Mara Iron alijikuta hajui lipi zaidi amwambie Nuru.
Hakuwa hodari wa kutongoza. Ingawa alisoma riwaya nyingi za mapenzi, lakini
ilikuwa vigumu sana kila alipotamani kuyaweka aliyoyasoma katika vitendo.
Sababu moja kati ya nyingi zilizomfanya hadi leo awe hana mke ni hiyo ya
kutojua kuwakabili wanawake wote aliowahitaji walikuwa kama wanaomdhihaki kwa
kusubiri aseme nini. Wale ambao hakuwataka ndio waliojileta kwake kwa urahisi.
Alipolewa hakubabaika kuwalaki. Lakini leo, kichwani akiwa hana hata tone moja
la pombe, hakuona vipi ampate Nuru. Akaduwaa akimtazama.
Nuru aliuhisi unyonge huo. Akaamua kusubiri.
Nusu dakika ilipotea kabla ya Iron kujua aseme nini.
Kisha alikumbuka kuwa alikuwa na akiba nzuri ya vinywaji vikali. Akafungua
kabati na kutoa chupa moja ya John Walker ambayo aliimimina katika glasi.
Alimkaribisha Nuru ambaye alikataa. Akaimimina tumboni mwake. Glasi ya pili
ilimchangamsha. Akarudisha vifaa hivyo katika kabati na kumsogelea Nuru na
kumgusa bega huku akinong’ona kwa sauti ambayo kichwani mwake alihisi imejaa
mahaba. “Wewe ni msichana mzuri sana wa Kiafrika. Sijapata kumwona mwingine wa
aina yako.” Mkono wake ukagusa pale ambapo ngozi ya bandia ya Uzungu aliyoivaa
Nuru ilikuwa imebandukabanduka kwa purukushani. Akaishika na kuibandua. Gundi
nyepesi iliyotumiwa kuiambatanisha ngozi hiyo ya nailoni na mwili iliacha
mabaka meupe. Lakini nyuma ya mabaka hayo ulijitokeza uso mzuri, uso asilia wa
Nuru. “Wewe ni mzuri kama ulivyo. Huhitaji kabisa ngozi hii,” Iron alisema
akizidi kuzibandua ngozi sehemu za mapajani.
Sasa aliyesimama mbele yake hakuwa tena yule msichana
wa Kizungu. Alikuwa msichana wa Kiafrika, msichana mzuri, ambaye kwa muda,
uzuri wake ulimpumbaza kaburu Iron. Kisha tamaa ikamzidi nguvu, mikono yake
ikapoteza utulivu na kuanza ziara kutambaa katika mwili wa Nuru. Mara ulimi
wake ukaanza kudai njia katika kinywa cha Nuru, huku akitweta kwa nguvu na
kunong’ona maneno ambayo Nuru hakuyaelewa. Hakutofautiana na sokwe mweupe
aliyeonjeshwa asali. Kila kitendo cha Von kilizidisha hasira katika moyo wa
Nuru. Mikono hiyo ilipoyafikia matiti yake na kuyachezea, akahisi kama
aliyeguswa na kinyaa ulimi ulipokuwa ukibishana na meno yake ukitafuta mwanya
wa kuingia mdomoni mwake, aliona kichefuchefu. Ambacho alitamani kufanya ni
kutumia fursa hiyo kuachia pigo ambalo lingeondoa uhai kisha kutafuta fursa ya
kutoroka. Hata hivyo, hakuthubutu kufanya hivyo kwa kuchelea kuharibu mambo.
Hakukoma kuitazama saa kubwa iliyokuwa ukutani. Kila dakika iliyopita alikuwa
akisheherekea kimoyomoyo. Sasa ilikuwa imebaki kama saa moja tu kabla ya mitego
waliyoitega kufyatuka. Wakati huo asingekosa mwanya wa kutoroka. Kabla ya hapo
alihitaji kuubembeleza muda kwa bei yoyote, isingemgharimu chochote kuendelea
kuliruhusu jitu nene liendelee kujipumbaza katika mwili wake. Mara moja mbili
akaguna na kutetemeka kwa namna ya kumfanya aonekane kama aliyeshikwa na
ashiki.
Kitendo hicho kilichochea wazimu wa Iron. Mara
akapambua mavazi ya Nuru. Mikono yake iliyokuwa ikitetetemeka iligombana na
vifungo vya mavazi huku akizidi kunong’ona hili na lile. “Sikiliza…” Nuru
alimweleza akiushika mkono wake na kuutoa mapajani mwake huku akimfinyafinya.
“Hapa ni ofisini. Mtu yeyote anaweza kuingia…”
“Hii ni ofisi yangu,” Von alikoroma. “Hamna anayeweza
kuingia bila ruhusa yangu.”
“Sio vizuri.”
“Tafadhali…” kisha Von alijilaumu kwa kutamka neno
hilo. Vipi amtafadhalishe mtu mweusi? Zaidi, mtu ambaye roho yake iko katika
mikono yake. Akaupeleka mkono wake wa pili katikati ya mapaja ya Nuru kwa nguvu
kidogo. Nuru aliyabana mapaja yake. Ni hapo Von alipokumbuka kuwa isingekuwa
kazi ndogo kumtenda msichana huyu bila hiari. Hakuwa amezisahau zile picha za
sinema ambazo huonyesha jasho linavyowatoka watu wanaojaribu kunajisi. Wala
asingesahau yaliyosemwa katika kile kitabu cha mapenzi alichowahi kusoma, “…
hicho ni kitu pekee ambacho mwanamke ana mamlaka nacho… kitu pekee anachoweza
kujivunia… rasilimali yake pekee…” hivyo, akajikuta akilazimika kutumia njia nyingine.
“Una habari kuwa maisha yako yamo mikononi mwangu? Dakika yoyote nitakayosema
ufe utakuwa marehemu. Najaribu kukuokoa kwa kuwa sioni kama unastahili kufa
mapema kiasi hiki,” alimweleza Nuru.
“Nitajuaje kama hunidanganyi? Nitajuaje kama baada ya
kumaliza shida zako hutaniua?” Nuru alisema akimlegezea macho.
“Nakuhakikishia kuwa utakwenda zako kwa amani na
furaha kokote unakotaka kwenda.” Von alipoona hajaaminika kikamilifu alimwacha
Nuru kwa muda na kuliendea kabati ambalo alilifungua na kutoa bahasha kubwa.
Ndani ya bahasha hiyo mlikuwa na pesa nyingi za nchi mbalimbali. “Hizi ni pesa
zenu. Ni miongoni mwa vitu vyenu mlivyonyang’anywa mlipofika hapa. Sasa hivi
nakukabidhi pesa hizi ukae nazo ili utakapoondoka zako ukaishi popote
unapotaka.” Alimpa Nuru na kuziweka katika mfuko wake. Alikuwa akicheka
kimoyomoyo akifahamu kuwa mara baada ya kuimaliza hamu yake na kumwua Nuru
angezirejesha fedha hizo katika himaya yake. “Sasa tunaweza kuendelea,” alisema
akianza upya kuchezea mwili wa Nuru.
Nuru hakumzuia mara moja. Alikuwa hajafahamu atumie
hila ipi kumchelewesha tena. Safari hiyo kilichomwokoa Nuru ni king’ora
kilichotoa mlio wa aina ya paka aliyekabwa koo katika moja ya mitambo ya Von.
Sauti hiyo ilimfanya Von aruke hadi kwenye simu ambako aliichukua na kusikiliza
kwa makini. Sauti nyembamba ilisema kwa wasiwasi, “Bosi, inaelekea kuna jambo
la hatari katika mtambo maalumu. King’ora cha hadhari kimekuwa kikilia kwa muda
mrefu. Simu za walinzi wetu huko hazipokelewi.”
“Impossible,” Von alifoka. “Unataka kuniambia kuwa
maafa yanayotokea mjini yanaweza kuhamia huko nje ya mji?”
“Inaelekea, mzee. Kwa sababu huyu mtu anayeitwa Joram
haelezeki. Aweza kuwa huko sasa hivi.”
“Impossible,” alifoka tena. “Na kama kweli kaenda
huko, basi kajipeleka mwenyewe kaburini.” Von alisita kidogo. Kisha aliongeza,
“Sikia. Andaa helikopta yangu na dereva. Nataka kufika huko mara moja. Nataka
kushuhudia kwa macho yangu mwenyewe mtu huyo anayejiita Joram Kiango
anavyosulubiwa.
***
Huko angani Nuru aliziona vizuri kabisa maiti nne za
askari wa Makaburu zilizovalia magwanda na silaha zao mikononi. Zilikuwa
zimelala sakafuni mbele ya lango kubwa la chuma ambalo lilizunguka ua wa
seng’enge uliozunguka jumba kubwa. Helikopta ililizunguka jengo hilo mara tatu,
Von akitazama kwa darubini huku na kule. Aliporidhika alimwamuru rubani kutua
kando ya ua huo katika kichaka kilichoutenga mtambo huo na mji.
Kutoka mjini hadi hapa, ilikuwa safari ya dakika mbili
tatu tu. Kabla ya kuanza safari hiyo Von alitupiana maneno makali na msaidizi
wake ambaye alishangazwa na uamuzi wa Von kumpeleka Nuru huko. Alimwambia,
“Sikubali kabisa. Nadhani ni wewe mwenyewe uliyeweka sharia ya kupigwa risasi
mtu yeyote atakayekaribia mtambo ule, awe raia wa nchi au mgeni. Vipi aende
huyu ambaye tunamhisi kuwa ni mwenzi wake ambaye amefika huko kufanya
mashambulizi?”
“Huyu ni mateka wangu,” Von alimjibu. “Bado nina mengi
ya kumsaili. Zaidi ya hayo, kama kweli Joram yuko huko tutamtumia huyu kumfanya
Joram asithubutu kuendelea na chochote anachoota kichwani mwake.”
“Bado sikubali,” msaidizi huyo alieleza. “Nimeandaa
kikosi cha askari wanne ambao ungefuatana nao huko. Kadhalika, nilikuwa
nikisubiri amri yako ili nitumie askari wengine hamsini kwa gari. Inaelekea
yote niliyofanya ni bure.”
“Ni bure kabisa,” Von alimjibu. “Unajua kabisa kuwa
mtambo ule unalindwa katika hali isiyo na shaka kabisa. Hata kama atafanikiwa
kuingia ndani hawezi kabisa kufanya madhara yoyote. Baada ya juhudi zake zote
ataambulia kufa tu. Hivyo, nakushauri urudi na hao askari wako uliowaandaa.
Nitakwenda mimi, huyu mateka na dereva tu. Sawa?”
Msaidizi huyo alimtazama Von kwa hasira ya mshangao.
Alizithamini sana hekima zake katika masuala yote ya kiusalama katika nchi hii
miaka yote aliyokuwa naye. Lakini vitendo vyake saa chache zilizopita
vilimchanganya kabisa. Vilikuwa vitendo ambavyo havikubaliki. Yeye, kama mtu wa
pili katika usalama wa utawala huu, hakuona kama alistahili kumtii Von hata kwa
hilo. Hivyo, alimtupia jicho la hasira na kumwambia, “Kwa mara ya kwanza
nitafanya kinyume cha matakwa yako.”
“Na kwa mara ya kwanza nakuambia kuwa… kuwa… hufai
kufanya kazi chini yangu. Baada ya suala hili nitaangalia suala lako,” Von
alisema akimsukumiza Nuru katika helikopta na kumwamuru rubani kuondoka.
Hata hivyo, rohoni alikuwa na mashaka kwa uamuzi wake
huu. Alijua kabisa kuwa alikuwa akifanya kosa kubwa kufuatana na Nuru huko
aendako. Hata hivyo, alifahamu fika kuwa hii ilikuwa nafasi yake pekee ya
kufanya naye mapenzi na baadaye kumwua. Kimojawapo cha vyumba kadhaa katika
jengo la mtambo huu kilikuwa chumba maalumu cha faraja kwa ajili yake na
wakubwa wachache sana. Chumba hicho kilikuwa na mitambo ya televisheni, ambayo
ilitumia nguvu ya setilaiti yao hiyo iliyoko angani kuitazama miji mbalimbali
ya Afrika kinaganaga. Vilevile kulikuwa na chombo maalumu ambacho kinaweza
kutazama shughuli zote zinazofanyika katika chumba hicho. Mara kwa mara Von
hujifungia humo na kutazama utendaji kazi wahandisi bila ya wao kuwa na habari.
Mhandisi mmoja aliwahi kupoteza kazi na maisha yake baada ya kushukiwa na Von kuwa
alikuwa na dhamira mbaya kwa mtambo huu. Hivyo, kifo chake machoni mwa watu
wengi kilionekana kama ajali tu iliyosababishwa na dereva mlevi kugonga mtu
anayetembea kando ya barabara katika mitaa ya Johanesburg. Leo Von alitegemea
kukitumia chumba hicho kujistarehesha na mwili wa Nuru kabla ya kutulia na
kuanza kuangalia kwa furaha watu wanavyoteketea kwa moto katika miji ya Dar es
Salaam, Lagos, Lusaka, Harare na kwingineko.
Furaha iliyokuwa ikichemka katika fikra za Von
iliingia nyongo mara baada ya helikopta yake kupita juu ya jengo hilo na
kushuhudia walinzi wake walivyolala ovyo wakiwa maiti. Hivyo, akamtupia Nuru
jicho la chuki. Tamaa aliyokuwanayo dhidi yake ilianza kuyeyuka na nafasi yake
kuchukuliwa na hasira kali. Alitamani ammalize papo hapo na kuyasahau yote
aliyokuwa akiyawaza juu yake. Hata hivyo, wazo jingine lilimjia akilini. Nuru
alionekana katili sana ambaye haogopi kifo kama wanawake wengine anaowafahamu.
Hata hivyo, anaweza kufa baada ya kutaabika sana. Hakuna mateso ambayo
yatamtaabisha zaidi ya kushuhudia kifo cha mpenzi wake, Joram Kiango. Akiwa na
hakika kabisa kuwa Joram alikuwa maala fulani katika jengo hilo akifa au
kusubiri kifo, Von alitoa bastola yake na kuigongagonga katika kisogo cha Nuru.
“Twende,” alimwamuru, baada ya kumtaka rubani asubiri katika helikopta.
Nuru alitelemka na kufuata maelekezo ya Von. Waliipita
miili ya marehemu waliolala ovyo, damu ikivuja kutoka katika majeraha ya risasi
miilini mwao.
Von alimshangaa Joram, peke yake, aliwezaje
kuwaangamiza askari wengi kiasi hicho bila wao kufanya lolote. Lakini
haikumshangaza Nuru hata kidogo. Wala Nuru hakuhitaji kusimuliwa. Akiwa mtu
anayemfahamu Joram na hila zake nyingi alijua kuwa alitumia njia moja au
nyingine kuwafikia askari hao waliojiamini kwa silaha zao aina ya machine gun.
Baada ya hapo alitoa hati zake za bandia kuwaonyesha askari hao, hati ambazo
zilifungwa kinamna kiasi cha kuhifadhi hewa ya sumu ambayo, bila shaka,
iliwafanya askari kulewa ghafla na hivyo, kuwaua mmoja baada ya mwingine
haikuwa kazi ngumu.
Kilichomshangaza Nuru ni kutofahamu Joram alikuwa
akifanya nini muda wote huo katika eneo la hatari kama hilo. Alikadiria kuwa
dakika tano zingetosha kabisa kuuteketeza mtambo huo na kutoweka. Na kwa mujibu
wa ramani yao ndani ya kiwanda hicho hamkuwa na ulinzi wowote zaidi. Vipi
asitokee na kummaliza mtu huyu mnene ili waondoke zao?
Von hakumpa nafasi ya kuwaza zaidi. Alikuwa akimsumbua
mbele kwa mtutu wa bastola yake harakaharaka. Nuru hakuwa mzito wa kuelewa kuwa
Von alikuwa akimtangulia kwa dhamira ya kumfanya ngao endapo lolote lingetukia
kinyume na mategemeo yake.
Baada ya kukagua vyumba mbalimbali wakafika katika
chumba cha Von. Ukiondoa makochi na kabati lililojengwa ukutani chumba hicho
hakikutofautiana na maabara au studio ya aina yake machoni mwa Nuru. Mashine na
mitambo mingi ilikuwa imepangwa kwa tafsiri fulani, kuta zikiwa screen
zilizopangwa katika hali ya kupokea habari mbalimbali. Von aliisogelea mashine
moja ambayo machoni mwa Nuru ilikuwa kama kompyuta na kubonyeza swichi
ainaaina. Kioo katika ukuta mmoja kilipata uhai na kuanza kuonyesha mambo ya
ajabuajabu. Baada ya hali kutulia Nuru aliona kuwa walikuwa wakitazama chumba
baada ya chumba katika jengo hilo. Kilitokea chumba ambacho kilikuwa na mitambo
mingi ya kutisha. Chumbani humo Nuru aliwaona wahandisi watatu waliokuwa makini
wakichapa kazi ya kuongoza mitambo bila dalili yoyote kuwa mambo yanakwenda
mrama. Hilo lilimfurahisha sana Von. Akaangua kicheko kwa furaha. Ni yeye
aliyependekeza kuwa kwa usalama wa mitambo ishara za hatari zisiwafikie
wahandisi hao, wasije wakapata hofu na kusababisha setilaiti iliyoko angani
kukosa uongozi wa ardhini, jambo ambalo lingeweza kusababisha maafa na hasara
isiyokadirika. Kwa jinsi jengo hilo lilivyoandaliwa Von alikuwa na hakika
kabisa kuwa ingemhitaji binadamu mwenye moyo wa malaika kuwafikia wahandisi hao
na kuuharibu mtambo huo. Joram hakuwa na moyo huo. Ni hilo lililomtia nguvu.
Sasa ameamini kuwa hakukosea. Kwa muda, aliwatazama wahandisi hao
wanavyoshughulikia. Wakijua kuwa leo ilikuwa siku ya kazi kubwa walifanya kila
kitu kwa juhudi na umakini wa hali ya juu. Kisha Von alibonyeza sehemu
nyingine. Chumba hicho kikahama na vyumba vingine kuanza kupita katika kioo.
“Nataka tumwone mpenzi wako anavyokufa au alipofia,” alimweleza, tabasamu la kifedhuli likiyasindikiza maneno yake. “Keti tafadhali. Keti ili uone kwa starehe.”
KIOO kilionyesha vyumba mbalimbali ambavyo
vilijitokeza na kupita. Kila chumba kilikuwa na vitu mbalimbali vilivyoyavuta
macho ya Nuru. Lakini ilielekea kuwa havikuwa vyumba Von alivyovihitaji.
Aliuendesha mtambo huo harakaharaka kwa kubonyeza kidude hiki na kile kama
karani anayepiga chapa. Mara kilitokea chumba ambacho Von alikuwa akikitafuta.
Katika chumba hicho, ambacho kilionekana kidogo, walikuwemo watu wawili
waliokuwa wakipigana. Mmoja hakuwa mtu bali jitu. Lilikuwa pande la mwanamume,
refu, nene, jeusi lenye magumi manene na macho ya kutisha. Lilikuwa likipigana
kwa maguvu yote katika hali ambayo ilionyesha kuwa lilikusudia kuua kwa mikono.
Jitu hili halikuwa na dalili yoyote ya uchovu wala maumivu yoyote. Kinyume
kabisa cha mtu wa pili ambaye lilikuwa likipambana naye. Huyu alikuwa kijana wa
kizungu, mwenye dalili zote za ushujaa na ufundi wa kupigana ngumi na karate.
Lakini ufundi wake haukuwa na dalili yoyote ya kuonyesha kulishinda jitu hili
kwani tayari kijana huyo alikuwa akivuja damu hapa na pale katika majeraha ya
kutisha, huku akiwa na dalili za uchovu mkubwa.
ITAENDELEA..............
0 Comments