TUTARUDI NA ROHO ZETU? (07)

 

ILIPOISHIA............

Hayo yalisemwa baada ya watu kuwatazama Joram na Nuru wakitoka katika ndege iliyowaleta, huku wakiwa wametanguliwa na rubani ambaye walikuwa wamemshikia bastola. Nje ya ndege Joram aliitupa chini bastola yake na kuweka mikono yake juu. Ndipo Polisi wa makaburu ambao walikuwa wameuzingira uwanja wakiwasubiri, wakajitokeza na kuwakimbilia.

 Wakawavamia na kuwakagua harakaharaka. Walipoona kuwa hawana silaha nyingine wakawaongoza kuliendea gari lililokuwa likisubiri. Muda wote huo kamera za televisheni na zile za wapiga picha wa magazeti ziliwaelekea Joram na Nuru kwa ukamilifu. Kama kuna chochote kilichowashangaza watazamaji ni jinsi sura za vijana hawa zilivyoonekana tulivu, nzuri, zisizo na dalili zozote za ugangwe kama walivyotegemea.

Msafara wa gari uliishia katika jumba moja kubwa lenye ghorofa kadhaa. Humo, badala ya lifti waliyoingia kuwapandisha juu iliwateremsha chini ambako walijikuta katika chumba kilichoelekea kuwa maalumu kwa kuhoji mateka. Askari waliokuwa nao waliamuru kusubiri, kisha wakatoka na kuufunga mlango nyuma yao. Baada ya muda waliletewa chakula na vinywaji. Wakala na kunywa.

SASA SONGA NAYO....................

Baada ya muda, kama walivyotegemea, walianza kutembelewa na maafisa wa upelelezi, ambao waliuliza maswali kemkem. Maswali yote waliyajibu kwa ukamilifu kama walivyojiandaa; kwamba walikuwa wameishiwa na hila za kuwaepuka INTERPOL wakaona hawana njia nyingine zaidi ya kukimbilia huku ambako wangehitaji hifadhi.

Baada ya maswali yalifuata mawaidha na badala ya mawaidha ikawa kashfa. "Wewe kama Joram Kiango ambaye nchi yako na Afrika nzima ilikutegemea huoni aibu kufanya ulivyofanya na kuja huku?" aliulizwa

"...Utajisikiaje utakapolazimika kufuata matakwa yote ya ubaguzi na kulazimika kushuhudia Waafrika wanavyonyanyaswa?"

"...Unaweza kukiri hadharani kuwa viongozi wote wa Afrika ni wadanganyifu na hawajui watendalo?"

"...Ukipewa bastola ili umuue mpigania uhuru yeyote atakayematwa, utafanyaje?"

"...Huyu msichana na uzuri wake wote ni malaya? Mbona anakubali kuandamana na mwizi?"

Yalisemwa mengi zaidi ya hayo. Yako ambayo Joram alijibu kwa namna ambavyo alijua walimtegemea kujibu. Mengine hakuyajibu, akijua kuwa walimtegemea kutojibu. Mengine ilimlazimu kuinama kwa haya akiwa na hakika kwamba walitarajia aone aibu. Baadhi ya maswali aliyakwepa kijanja akijua ni mitego iliyokusudiwa kumnasa.

Kutoka hapo walipelekwa katika chumba kilichokuwa na mitambo mingi ambayo eti ingeonyesha kama walikuwa wakisema ukweli au la. Waliwekwa katika mitambo hiyo na kuanza kuulizwa tena maswali. Yote hayo Joram alikwishamfafanulia Nuru kabla hawajaondoka Paris kuja Kinshasa, Zaire, ambako waliiteka nyara ndege ile ya kukodi. Alimweleza kuwa ambacho mtambo kama huo unaweza kuonyesha ni dalili za moyo kudunda na damu kuchemka mara unapoulizwa swali ambalo litakushtua au unapobuni uongo. Hivyo, endapo utazungumza kwa kujiamini haitaonekana dalili yoyote.

Ndivyo ilivyotukia. Saa chache baadaye walichukukuliwa na gari kutoka katika chumba hicho na kupelekwa katikati ya mji ambako waliingizwa katika nyumba moja kubwa na kuelekezwa katika chumba kilichokuwa na vitanda viwili. Humo walikuta mizigo yao yote. Ingawa mizigo yao ilikuwa kama ilivyokuwa, lakini Joram hakusita kugundua kuwa tayari ilikuwa imekaguliwa kwa ukamilifu. Hilo alilithibitisha baada ya kufungua na kukuta kila kitu kimo isipokuwa furushi la pesa zilizokuwa zimesalia. Hilo pia alilitegemea. Hivyo, hakubabaika. Akamwendea Nuru na kumvuta mkono akimwelekeza kitandani ambako alimketisha ili ampumzike kidogo.

"Pole,” alimwambia.

"Kwa?"

"Usumbufu."

"Mbona bado sijasumbuka. Naamini huu ni mwanzo tu, kuna mengi yanayokuja na nitakuwa tayari kuyakabili yote..."

"Shii," Joram alimnyamazisha. “Usijisikie huru kiasi hicho," alinong'ona. "Bado tuko chini ya ulinzi mkali. Yawezekana wanatutazama na kutusikiliza. Kiswahili si lugha ngumu kiasi hicho. Endelea kujihadhari."

Moyoni Joram alikuwa na sherehe kubwa. Alikuwa akishangilia mafanikio ya msafara huo ambao ulienda kama alivyokusudia kuelekea kuzaa matunda. Kufika Afrika Kusini na kupata mapokezi yenye hadhi kwa kiwango hiki ilikuwa jambo pekee la pili ambalo alilihitaji sana. Jambo la awali ambalo alihakikisha limefanikiwa kabla hajabandua mguu wakekuiacha dunia huru na kujitosa jehanamu kiasi hiki ilikuwa kulisafirisha sanduku lake ambalo lilikuwa na kila kitu alichohitaji katika jukumu lililokuwa mbele yake. Kati ya vitu vilivyokuwemo ni pamoja na pesa za matumizi muhimu, silaha aina aina, madawa ya kila aina, ramani mbalimbali, ngozi na sura za bandia ambazo zingemfanya aonekane mtu mweupe, na zaidi ya yote ni vile vijigololi maalumu ambavyo alivipata kutoka kwa hayati Chonde.

Ilikuwa imemgharimu uongo mkubwa na pesa kuweza kulifikisha sanduku lile katika nchi hii. Alikuwa ametumia hila za kumwendea mfanyabiashara wa Kimarekani ambaye alikuwa akisafirisha mizigo yake moja kwa moja kutoka Ufaransa. Baada ya kujijenga kwake kwa urafiki bandia alimhadaa kuwa amepata oda ya kuuza madawa ya kulevya nchini Afrika Kusini. Mmarekani huyo alikataa kabisa kujihusisha kwa hali yoyote katika biashara ya aina hiyo. Joram alikazimika kumpigia magoti kwa maneno huku akimpa pesa nyingi na kumwahidi sehemu kubwa ya faida. Ndipo sanduku hilo liliposafiri pamoja na mizigo mingine muhimu ya Joram. Na aliarifiwa kuwa sanduku hilo limefika salama. Ilimpendeza sana Joram kuona kati ya watu wengi waliokuja kiwanjani kushuhudia wateka nyara hao wakitelemka kutoka ndani ya ndege, mmoja wao alikuwa Mmarekani huyo aliyeitwa Moore. Ilimpendeza zaidi kuwa Moore hakuweza kufahamu kuwa mteka nyara huyo ndiye yule aliyekuwa rafiki yake siku tatu zilizopita nchini Ufaransa. Joram akiwa amekariri ramani ya nyumba ya Moore kama anavyovifahamu viganja vyake vya mkono, alikuwa akiisubiri kwa kiu kibwa fursa ya kuweka mikononi mwake mizigo yake.

Kabla ya kuoga kama alivyohitaji kufanya, Joram alijitia shughuli na kufanya kama anayepanga vitu chumbani kwake vizuri. Alichokuwa akifanya hasa ni kitu au vitu fulani na haukupita muda kabla ya kukiona alichokuwa akitafuta. Kipande kidogo sana cha kioo kilichokuwa kimejitokeza sakafuni katika pembe moja ya chumba kama kilichosahauriwa na waashi kwa bahati mbaya. Joram alijua kuwa nyuma yake kipande hicho kulikuwa na nyaya ambazo zilisafiri hadi kwenye mtambo ambao ulikuwa na jukumu la kupeperusha kila wanachoongea au hata kuwaona. Baada ya kuona hayo Joram alilidhika, akijua kuwa alikuwa hana haraka ya kuwa msiri. Alihitaji faragha kwa usiku mmoja tu, na katika usiku huo alijua ambacho angefanya kuufanya mtambo huo ushindwe kuwajibika kwa dakika kadhaa.

Wakaoga.

Wakalala.

Jasho jembamba lilikuwa likiwatoka maofisa wanne wa Boss ambao walikuwa katika chumba fulani wakiwashuhudia Joram na Nuru walipokuwa wakifanya mapenzi katika chumba chao. Maofisa hao walikuwa wamekaa katika chumba hicho kwa muda mrefu, dhamira yao kuu ikiwa kupata hakika kama kweli Joram alikuwa hana hila nyingine iliyomleta Afrika Kusini zaidi ya ukimbizi. Taarifa za maofisa wote waliotumwa kuwahoji na ambao walikagua mizigo yao haikuonyesha hila wala ila yoyote. Hata hivyo upinzani uliokuwepo uliishia kuamuliwa kuwa wapewe chumba hiki na kuachiwa uhuru kiasi fulani ili waendelee kuchunguzwa. Chumba hiki kilikuwa maalumu na siri kubwa isipokuwa kwa maofisa wachache wa ngazi za juu. Ndipo jukumu la kuwatazama Joram na Nuru likawaangukia kaburu Von Iron na wenzake.

Ndipo walipolazimika kutokwa na jasho. Kwani walikuwa wakitazama kwa namna moja ilikuwa kama picha ya kupendeza sana, kwa maaana nyingine picha ya kuchukiza, inayotesa na kuadhibu.

Ilikuwa picha ya kupendeza wakati walipokuwa wakiwatazama Joram na mpenzi wake Nuru walipokuwa wakitazamana kwa mapenzi pindi wakati wakijiandaa kulala. Ikaanza kuchukiza walipoanza kuvua mavazi yao na kuketi kama walivyozaliwa huku wakibusiana. Na ilianza kutesa walipojibwaga kitandani na kufanya mapenzi kiroho mbaya bila kujali au kujua kama wanatazamwa, kana kwamba walikuwa wakiwaonyesha watazamani kwa makusudi.

Von Iron aliuzima mtambo huo na kulifuta jasho lililokuwa katika paji lake la uso. Hakujiamini kuwatazama wenzake machoni, akihofu wasije wakasoma kitu alichokuwa akikisoma akilini. "Tukutane kesho..." Von aliamuru akianza kutoka nje. Bila kuinua macho aliweza kuhisi kuwa wenzake walikuwa wakimhurumia zaidi ya walivyokuwa wakijihurumia wao. Alijua vilevile kuwa wenzake hao walijua kama alivyojua yeye kuwa baada ya kuagana nao angerudi katika chumba hicho.

Alirudi.

Akiwa peke yake aliwatazama kwa makini na uhuru zaidi, akisherehekea kila hatua iliyofuata katika mapenzi yaliyokuwa yakiendelea mtindo mmoja juu ya kitanda. Tangu alipokuwa amewaona Nuru na Joram katika televisheni hajua kuwa wangeweza kuwa wazuri kiasi hiki. Kadhalika hakutegemea kuwa Mwafrika aliyevua nguo angeweza kuwa kiumbe mzuri kama hawa, aliwategemea kuwa viumbe wa kutisha sana kama mizimu. Kumbe sivyo.

Aliendelea kuwatazama. Alijipinda na kujinyoosha kwa maumivu na tamaa kubwa huku mkono wake mmoja akiubembeleza uume wake, mkono wake wa pili ukiwa umelea kichwa kwa wivu wa masikitiko. Starehe au mateso yake yalikoma Joram alipozima taa.

Von alijifariji kwa kuizima mitambo hiyo na kubonyeza ile ambayo ilimfanya akague ulinzi na usalama wa ule mtambo wa nyuklia unaoendesha Satilaiti maalumu iliyoko angani ikisubiri kufanya kazi ambayo haitafutika katika kurasa za historia ya dunia. Aliuona ulinzi ulivyokuwa makini. Askari wanne wenye machine guns walikuwa wakipita kwa zamu kulikagua jengo hilo. Ndani mafunzi wenye silaha walikuwa machio wakikagua mwenendo wa mtambo huo kwa umakini na uangalifu mkubwa. Von aliweza kuona katika screen kubwa iliyokuwa mbele ya wanasayansi hao jinsi setileiti hiyo ilivyokuwa ikielea huku na huko katika bahari ya Hindi kando ya pwani ya Afrika Mashariki. Alitabasamu kidogo alipojikumbusha utaalamu wa hali ya juu uliotumika katika kuunda chombo hicho hata kisiweze kuonekana kwa macho ya kawaida.

Kisha alibonyeza mahali fulani kuondoa mtambo huo machoni kwake. Badala yake alibonyeza mahali ambapo palimwezesha kuona gereza la ardhini ambamo kulikuwa na mateka au wafungwa ambao walitakiwa kuteswa hadi kufa. Humo kulikuwa na kila aina ya mateso. Haikuwepo njia yoyote ya kuweza kutoka isipokuwa kwa funguo maalumu ambazo alidhihifadhi yeye mwenyewe. Von aliwatazama wafungwa au mateka hao waliokuwa wakikaribia kufa. Baadhi yao walikuwa weupe, Mmarekani mmoja ambaye alikuwa mpumbavu kiasi cha kuamua kuwasaidia wapigania haki wa Afrika Kusini, pia walikuwepo Warusi wawili ambao pia tabia zao hazikuwa tofauti na mzungu huyo pamoja na watu weusi watatu. Ni hawa watu weusi ambao walimfanya Von aangue kicheko kwa sauti. Alijiuliza walikuwa wamepatwa na nini weusi hawa hata wakathubutu kujileta wenyewe huku kama wapumbavu. Mtu atajipeleka jehanamu na kutegemea atatoka salama?

Zimesikika habari nyingi za watu ambao waliwahi kufa na baada ya siku kadhaa kufufuka. Watu hao hudai kuwa walipokuwa wafu wamefika peponi na kuwaona malaika. Haijawa kutokea hata mtu mmoja ambaye aliwahi kwenda jehanamu na akarudi duniani. Hawa weusi aliwaona kama watu walipenda sana kufa vifo vya kikatili. Jambo la kusikitisha kwao ni kwamba BOSS iliarifiwa tangu walipoondoka Naijeria na Tanzania na kuja Botswana. Iliarifiwa pia walipoanza mbibu za kuvuka mpaka. Hivyo hila zao za mmoja kujifanya wendawazimu asiyejua analofanya na mwingine kujitia mkimbizi anayeishi kambi ya wapigania uhuru hazikuwa na mafanikio yoyote. Von hakupenda kuwaona ana kwa ana. Aliamua wafungiwe katika chumba cha mauti wasubiri kifo. Hawa walikuwa wawili tu kati ya wanane ambao walikuwa wamekamatwa siku mbili zilizopita. Wawili walikuwa wameuawa kwa mateso wakati wakihojiwa. Mmoja alikuwa amejiua mwenyewe kwa sumu baada ya kumvamia askari aliyekuwa akimhoji na kumjeruhi vibaya kwa kisu kabla hajameza vidonge ambavyo vilimuua mwenyewe.

Wapelelezi hawa walikuwa ni matokeo ya juhudi za kuthibitisha uwezekano wa kuwepo kwa mtambo maalumu unaoziadhibu nchi za Kiafrika. Von alifahamu kuwa bado wangekuja wengi zaidi, weupe kwa weusi, lakini kamwe wasingefika popote pa haja. Na kamwe wasingefika popote kwani zilikuwa zimesalia siku mbili tu kabla ya Afrika huru kuipigia magoti Afrika Kusini na kusubiri vilio na maombolezo yasiyo na mfano. Von alicheka tena, safari hii kwa kujipongeza akijua kuwa sifa ndogo kuwa na wadhifa kama aliokuwa nao sasa. Roho za watu wengi kuwa mikononi mwako zikisubiri tamko lako kabla ya kuteketezwa!

Kisha Von aliufunga mtambo huo na kurudi nyumbani kwake. Akiwa kapera ambaye hakujua lini angeoa alijikuta akikosa usingizi alijikuta akimfikiria Nuru na kumwonea Joram wivu. Bila kufahamu anachokifanya Von alijikuta akiapa kwa jina la Mungu kuwa asingekufa kabla hajamuonja. "Mara moja tu..." alijiambia. "Nione wana nini wanawake weusi..."

Kesho yake aliamuru Joram na Nuru waletwe katika ofisi yake. Akiwa amezungukwa na wasaidizi wake Von alijitahidi kuwatazama Joram na Nuru kwa namna tofauti kabisa na ile iliyokuwa ikipita katika akili yake.

"Sina haja ya kuwahoji chochote", Von aliwaambia kwa sauti nzito. "Kwa kiasi mlichohojiwa naamini mmeonyesha kuwa mmechoshwa na upuuzi wa hawa viongozi wanaojiita wanamapinduzi katika nchi zenu. Sivyo?"

"Kwa maana hiyo mngependa kuishi huku daima. Msimamo wenu ni wa kishujaa. Nawapenda watu shujaa. Ni hilo ambalo limenisukuma kuwaacha hai pamoja na kuwapa heshima ya kuwaita hapa ili niwape habari njema".

Joram akiwa amesimama mbele yake, akiwa kamshika Nuru mkono, hakuwa na haja ya kuambiwa huyu ni nani katika nchi hii. Alimfahamu mara moja kuwa alikuwa mkuu wa shirika la kijasusi la utawala huu. Kwa maana nyingine alikuwa adui yake namba moja. Mtu ambaye asingeondoka bila kumpa adhabu ya risasi ya kichwa kwa hatia ya kusababisha maafa kwa Waafrika wengi wasio na hatia. Hata hivyo Joram hakuonyesha dalili yoyote katika macho yake alipouliza kwa upole, "Habari njema ipi? Tumeruhusiwa kupewa uhuru zaidi ya huu tulionao? Tunajiona kama ndio tuko kifungoni".

"Mko huru kuliko mnavyostahili", Von alimjibu Joram. "Habari njema niliyotaka kuwapeni ni juu ya uhalibifu ambao utazitokea nchi za Kiafrika kesho saa nne mchana endapo hawatawatuma viongozi wao hapa leo kuweka saini mikataba ya kuwa watiifu kwa utawala huu na kutothubutu kuwasaidia wendawazimu wanaodai uhuru wa Namibia na haki hapa Afrika Kusini. Kama hawatafanya hivyo hadi saa tatu na nusu za mchana. Nyie mtapewa heshima ya kushuhudia moja kwa moja Ikulu zinavyoungua, majengo yanavyoteketea na watu kupoteza maisha. Mtabahatika kushuhudia jambo la kupendeza. Jambo la kihistoria".

Macho yake yaliwatazama Joram na Nuru kwa umakini. Nao wakifahamu kuwa kuna kitu kilitakiwa kuonekana katika macho yao, Joram aliruhusu tabasamu kidogo huku Nuru akifuta machozi.

"Ni habari njema", Joram alisema polepole baadaye akauliza. "Habari njema..., tunaweza kuruhusiwa kurudi chumbani kwetu?".

Binadamu hajapata kuwa na adui mwingine, mkubwa na mkatili katika maisha yake zaidi ya kifo. Ni kifo pekee ambacho kimeishinda akili ya binadamu. Hakukosea yule mwanamuziki aliyeimba "kifo hakina huruma, kifo ni kiboko yao". Hutokea binadamu akawa na shughuli zote, siku nenda rudi bila kukipa kifo wazo lolote hadi kinapotokea bila kutegemewa. Ni hiyo sababu pekee inalomfanya mwanadamu asitokwe na jasho la hofu siku zote za maisha yake kwa kuogopa kifo. Kwa vile hutokea bila ya kutegemewa.

Hivyo hakuna kifo kibaya kama kifo cha kusubiri siku na saa. Hasa kifo cha kinyama na cha kikatili kama hiki ambacho kilikuwa kikitegemewa na watu kadha wa kadha katika nchi kadha wa kadha za Kiafrika. Leo ilikuwa imewadia siku ile. Siku ambayo Afrika ya Kusini ilikuwa imetoa kuwa ingekuwa ya mwisho kabla ya kuachia pigo la mwisho ambalo lingeiteketeza miji yote ya nchi zilizoko mstari wa mbele.

Pamoja na ukweli kwamba tukio hili lilikuwa limeamriwa kuwa siri kubwa sana miongoni mwa wahusika, kama yale mengine ambayo huishia katika masikio ya wachache na hutoweka bila ya raia wa kawaida kuyapata, lakini hili kwa njia moja ama nyingine lilikuwa limevuja na kusambaa mitaani. Jambo ambalo lilisababisha mashaka na hofu kubwa mitaani. Wananchi waumini wa dini walitoroka makazini na kukimbilia kwenye makanisa na misikiti ili kutubu dhambi zao zote na kumbembeleza Muumba awanasuwe awanasuwe katika janga hili. Wale ambao hawakumwamini Mungu walitulia katika vikundi vikundi wakizungumza kwa utulivu. Wachache sana waliamua kuyamalizia maisha yao huku wakinywa pombe katika baa ambazo hazikufunguliwa milango.

Viongozi wa Chama na Serikali walikuwa katika vikao vya dharura wakijaribu kujadiliana hili na lile. Lolote la haja halikupatikana, japokuwa yalitokea mapendekezo mengi. Jambo ambalo kila mmoja alitamani kutamka ingawa ulimi ulishindwa kutamka hadharani kwa aibu, ni ambalo lingewahakikishia wananchi uhai na usalama wao. Lakini maadamu ungekuwa uhai usio na uhuru, na usalama usio na uhakika na hakuna aliyethubutu kupendekeza hivyo. Iliyonaki ilikuwa kupeana moyo tu kuwa haiweze kutokea, na endapo itatokea cha kufanya ni kujaribu kuepuka majengo ambayo yanaweza kuelekea kuyavuta macho ya muuaji. Ilielezwa pia kuwa kote nchini wananchi walikuwa wakichimba mahandaki kwa ajili ya kujificha.

Ikulu, Rais na baraza lake la mawaziri walikuwa katika kikao cha muda mrefu. Kikao ambacho kilichukua siku nzima, hata usiku ukaanza kukaribia. Inangawa kilikuwa kikao cha siri sana, lakini ilikuwa dhahiri kuwa chochote ambacho kilikuwa kikijadiliwa ndani hakikupata ufumbuzi ya tatizo. Mmoja alikuwa amependekeza kwa mara nyingine kuwa nafasi hiyo itumike kuivamia Afrika Kusini kijeshi, "Ili tukomeshe kabisa suala hili la kutishiwa na kuonewa mara kwa mara. Tutumie majeshi yetu yote ya nchi za mstari wa mbele kuingia nchini humo na kuanzisha mapambano ili kuunda utawala halali. Najua, adui ana jeshi imara na silaha kali sana. Lakini wingi witu wetu utasaidia tutashinda..."Mapendekezo hayo yalijadiliwa lakini hayakuonekana kama yangekuwa jibu la kuziokoa nchi za Afrika na kumaliza tatizo ambalo lilikuwa mbele likisubiri saa chache ili litokee. mwingine akatoa wazo. "Si rahisi kutumia masaa manane yaliyobaki kukusanya majeshi na kuyaongoza katika nchi nyingine na kuanzisha vita. Zaidi yote, hatari au mkasa ambao uliokuwa ukisubiriwa ulikuwa ukitokea angani, hivyo uvamizi huo usingesaidia au kuzuia maafa hayo...". Baraza la mawaziri liliendelea kujadiliana kwa utulivu katika ukumbi huo wa Ikulu. Jengo hilo likiwa miongoni katika majengo kadhaa yaliyokuwa katika orodha ya kulipuliwa ilikuwa kana kwamba Rais na mawaziri wake walikuwa wameamua kikisubiri kifo hicho kwa pamoja; kufa kiofisa...

Binadamu aliyekuwa na hali mbaya kuliko wote nyumbani nchini Tanzania aliitwa Inspekta Mkwaju Kombora. Yeye alikuwa akitaabika kimwili na kiakili. Juhudi zake zote, pamoja na wenzake wa kutoka nchi mbalimbali, zilikuwa kama upuuzi. Upelelezi ulikuwa haukuzaa matunda yoyote yale. Na hasa upelelezi huo ulikuwa kama umewafanya wazidi kujipalia mkaa wa moto; kwani ilikuwa dhahiri kuwa kila jambo linaloafikiwa hapa wakati huo huo utawala wa makaburu unakuwa na taarifa nalo. Hayo yalithibitika alipoarifiwa kuwa wapelelezi wote waliotumwa kuingia Afrika Kusini walikuwa mikononi mwa makaburu. Ilikuwa kama waliopelekwa kufa makusudi kabisa. Jambo ambalo lilimfanya ashuku mara moja kwamba miongoni mwao alikuwemo chui aliyejivika ngozi ya kondoo.

Hivyo Insipekta Kombora aliugeuza upelelezi wake kutoka mstari wa mbele na kuanza kuchunguza mstari wa nyuma. Na haukupita muda kabla dalili hazijajitokeza kuwa huyu mgeni aliyedhaniwa kuwa msamaria mwema, ambaye alileta fununu nyingi kutoka Afrika Kusini angehitaji kuchunguzwa zaidi. Uchunguzi ukaanza katika vikosi vyote vya wapigania uhuru duniani, katika vyuo na hospitali ambazo alidai amepitia na hata Afrika Kusini. Taarifa zilizidi kuongeza haja ya kutazamwa kwa makini. Na haukupita muda kabla kabla ya watu waliokabidhiwa jukumu la kumwangalia hawajatoa taarifa kuwa alikuwa mtu wa BOSS. Habari hiyo ilimuumiza sana Kombora. Alitoa amri kuwa mtu huyo aliyejiita Clay achunguzwe kwa makini sana, kwani kwa vyovyote leo ilikuwa siku ya mwisho iliyotolewa na utawala huo haramu na lazima angekuwa na jambo la kuarifu kwa mabwana zake.

Baada ya hayo Insipekta Kombora aliendelea na shughuli katika ofisi yake. Alipokea na kujibu simu na walkie talkie nyingi ambazo hakuona kama zilikuwa zikimsaidia chochote. Aliwasiliana na maofisa wenzake katika nchi za Zambia, Zimbabwe, Angola, Msumbiji, Naijeria na kwingineko kujaribu kuona wamefikia wapi. Hakuna alichopata zaidi zaidi ya yale aliyotegemea. Kwamba wananchi walikuwa wakitaabika na kulalamika mitaani katika hali ya hofu kubwa. Kwamba hata makazini hawakuwa wamekwenda.

Ofisi ilikuwa haikaliki. Kila Kombora alipojaribu kutulia juu ya kiti, kiti hakikuelekea kuafikiana naye. Kila alipoinuka ili atoke, hakujua angeelekea wapi. Unawezaje kutulia na huku unahesabu saa kusubiri kifo au maafa ya kusikitisha ambayo ni aibu kwako, kwa taifa lako na bara lako zima? Aliendelea kutaabika kimwili na kimawazo, akipokea na kusikiliza habari kutoka sehemu mbalimbali. Mara zilimfikia habari za Joram na Nuru kuwa walikuwa wameingia Afrika Kusini na kuomba hifadhi ya kisiasa. Kwa kombora zilikuwa habari za kushangaza sana. Habari za kusikitisha. Habari zinazotia aibu. Joram Afrika kusini! Hata hivyo, alikwishachoka kushangazwa na habari za kijana huyu anayeitwa Joram. Mambo yote aliyokuwa akiyafanya, ambayo yaliwafikia watu wa habari, Kombora aliyasikia au kuyaona katika vyombo vya habari. Angeweza kumsifu Joram kwa mbwembwe zake ambazo ziliwafanya polisi wote wa miji mbalimbali na nchi zilizoendelea washindwe kumtia mikononi. Lakini kila alipokumbuka kuwa mbio hizo za Joram zilikuwa za kukimbiza akiba pekee za pesa ya kigeni alizoibia nchi yake alijisikia vibaya. Hayo yakifuatwa na tishio lililokuwa likizidi kusogea, vilimfanya ajilazimishe kuliondoa jina hilo akilini mwake.

“… Inspekta Kombora anaongea. Namba ngapi hiyo?” alijibu sauti katika walkie talkie iliyokuwa mkononi mwake. Alipotajiwa namba alijikuta akisikiliza kwa makini zaidi. Ilitoka kwa kiongozi wa makachero ambao walikuwa wakifuatilia nyendo za Clay.

“… Inaelekea kama tutamkamata red handed, mzee. Sasa hivi anaunganisha mitambo yake ya mawasiliano…”

“Nisubiri. Nakuja mara moja.”

Dakika mbili tatu baadaye, Kombora alikuwa miongoni mwa polisi wanne waliokuwa katika chumba fulani katika hoteli ya Kilimanjaro. Chumba hiki kilikuwa cha nne kutoka chumba cha Clay. Hata hivyo, kutokana na mitambo waliyoitega kitaalamu, japo hawakuwa wakimwona, waliweza kumsikia anavyoongea katika chombo fulani cha kijasusi.

“Sikiliza mzee… sikia…” askari mmoja alimwambia Kombora huku akitweta.

“…Ndiyo. Ndiyo… nimefanikiwa kupanda katika majumba ya kutosha. Moja Ikulu.. hapa Kilimanjaro moja… jengo la IPS moja… Kitegauchumi… Muhimbili… Benki Kuu ya muda… Tipper… kiwanda cha Urafiki na sehemu mbalimbali muhimu. Tunachosubiri ni saa moja tu. Ikifika, kwa jinsi nilivyotega inaelekea jiji zima litalipuka. Mimi nitaondoka hapa wakati wowote…”

“Unasikia mzee?... Unasikia?”

Kombora hakusubiri kumsikiliza afisa huyo. Aliwaamuru kumfuata kukiendea chumba cha Clay. Kinyume cha mategemeo yao waliukuta mlango ukiwa wazi. Naye alikuwa kaketi kwa utulivu juu ya kochi, gazeti mkononi. Yeyote ambaye angeingia bila ya kufahamu kinachotokea angemdhania kuwa alikuwa akisoma gazeti.

ITAENDELEA....................

Post a Comment

0 Comments