TUTARUDI NA ROHO ZETU? (06)

 

Joram aliduwaa huku akimtazama msichana huyo. Hakuwa na shaka kuwa msichana huyo ni shujaa. Lakini hakujua kuwa ni shujaa kiasi hicho. Ndiyo, alimtegemea sana katika msafara wake. Lakini hakukusudia kumwingiza katika mkasa ambao ilikuwa dhahiri kuwa pamoja na ugumu wa maandalizi yake ya muda mrefu hadi sasa matekeo yake yalikuwa gizani. Yeye alikuwa tayari kwenda, tayari kufanya kazi inayompeleka; uwezekano wa kurudi haukumsumbua. Kufa kusingemtisha sana mradi atakuwa ameifanya kazi yake. Kifo chake ni jambo moja, kusababisha kifo cha mtoto wa watu, mzuri kama Nuru, ni jambo jingine.

"Sikia Nuru. Labda huelewi... Nakusudia kwenda toka hapa sio nchi ya kawaida. Ni nchi ambayo kuna watu wenye kiu kubwa ya damu ya mtu mweusi na njaa kubwa ya roho zetu. Na ninahitaji kujipeleka moja kwa moja mikononi mwao. Kwa ufupi nategemea kwenda Afrika Kusini...".

"Tutakwenda pamoja".

...Na ninachokwenda kufanya ni hujuma. Wakinigundua watanitafuna mbichi".

"Watatutafuna pamoja".

Joram akaduwaa. "Labda nikufunulie kila kitu kilivyo Nuru", Joram akamwambia. ""Nisubiri", alisema akiliendea begi lake lililokuwa limefurika kwa vitabu aina aina pamoja na encyclopedia ambazo Joram alikuwa akizitumia kwa muda mrefu kujaribu kuyasoma yake maandishi ya kijasusi ambayo aliyapata katika mfuko wa hayati Chonde. Humo alitoa karatasi ndefu, iliyoandikwa kwa mashine, ikiwa tafsiri ya maandishi hayo. Alimkabidhi Nuru na kumwabia asome haraka haraka.

 SASA SONGA NAYO............................

MPANGO KABAMBE WA KUIFANYA AFRIKA ITUPIGIE MAGOTI

 

Taarifa hii ni siri kubwa miongoni mwa watu wachache sana, wa ngazi za juu katika serikali yetu. Ni taarifa ya mafanikio ya jaribio lililofanyika muda mrefu, kwa gharama kubwa, baina ya wana sayansi wetu na waliotoka katika nchi marafiki duniani; juu ya uwezekano wa kufanya nguvu za nukria zitusaidie katika kuwaweka Waafrika, na ikiwezekana dunia nzima katika kwato zetu.

Itakumbukwa kuwa kifungu kikubwa cha pesa kilitengwa ili kufanyia majaribio haya. Kwa siri kubwa sana mtambo madhubuti ulijengwa na setilaiti kutupwa angani. Mbili kati ya setilaiti hizo zilidondoka katika nbahari ya Hindi kabla ya kuonyesha matokeao. Lakini setilaiti ya tatu imetimiza majibu. Majaribio yamefanywa na kuleta matokeo ya kuridhisha kabisa. Mtu wetu alitumwa Lagos na kutega gololi maalumu ambazo baada ya kufyatuliwa zimeifanya setilaiti hiyo iliyoundwa kwa madini yanayoifanya isionekane kwa macho iweze kuingia katika anga la nchi hiyo na kuachia bomba la moto mkali ambao uliteketeza uwanja na watu kadhaa. Jaribio la pili lilifanywa huko Harare ambako maghala yaliteketea. Jaribio la tatu na la mwisho linakusudiwa kufanywa Tanzania, katika jengo la Benki Kuu inayojengwa. Hatuna shaka kuwa jaribio hilo litafanikiwa.

Baada ya jaribio hilo ndipo tutaanzisha mpango wa kuzifanya nchi zote zinazojiita za mstari wa mbele, kutupigia magoti. Mtu wetu anayekwenda Tanzania ni mtu wa kutegemewa, aliyeishi huko miaka mingi. Atapewa pesa nyingi zitakazomwezesha kwenda mahala popote duniani, na kumnunua mtu yeyote. Huyu atakuwa na jukumu la kusubiri amri yetu ili aachie vipigo vingine ambavyo vitaifanya Afrika itokwe na machozi huku dunia ikilalamika...

Nuru aliinua kichwa ghafla kumtazama Joram. Tayari uso wake ulikuwa umelowa jasho la hofu na mshangao. "Joram" Nuru alifoka, "Mungu wangu. Huoni kama hii ni habari ya kutisha kuliko zote? Tunawezaje kustarehe hivi huku nchi yetu ikiwa mashakani?".

"Imenichukua siku nyingi kuigundua. Waliyaficha maandishi hayo kwa hila ambazo zingemtoa jasho mtu yeyote mwenye akili timamu. Hata hivyo ugunduzi huu hautatusaidia chochote. Kama ulivyosoma setilaiti hiyo iko angani na haionekani kwa macho. Inaendeshwa na mtambo ambao uko katika himaya yao, bila shaka ukilindwa kwa hali na mali. Hakuna njia nyingine zaidi ya kuubomoa mtambo huo".

"Je. Tukitoa siri hii kwa dunia?", Nuru alimuuliza Joram.

"Haisaidii. Umoja wa Mataifa utalalamika na kuilaani Afrika Kusini. Pengine watawekewa vikwazo vya kiuchumi. Unadhani hayo yatawafanya watuhurumie?". Mara ngapi wamelaaniwa? Mara ngapi wamewekewa vikwazo? Hapana Nuru. Lazima nifike Afrika Kusini. Dawa ya moto ni moto".

Nuru alitulia kwa muda akiitafakari taarifa hii kwa makini. Mara aliinuka na kumwendea Joram. Akamkumbatia na kumnong'oneza masikioni. "Samahani sana mpenzi. Nilikuelewa vibaya sana ulipoiba pesa benki. Vilevile nilishangaa unavyozitumia pesa hizo vibaya kwenda huku na kule ukuwa hujali matusi ya waandishi wa habari. Sasa nimekuelewa. Nimeelewa kwanini ulifanya vile. Ulikuwa ukijiandaa kwenda Afrika Kusini. Ulichofanya ilikuwa kuilaghai dunia ili uonekane mhalifu na mkimbizi asiyeweza kuishi popote isipokuwa Afrika Kusini. "Sivyo mpenzi?". Joram alipochelewa kujibu Nuru aliongeza, "Mpenzi. Wewe ni shujaa kuliko mashujaa wengine niliopata kuwasikia. Tutakwenda pamoja Afrika Kusini...".

"Tatizo siyo kwenda Nuru. Tatizo ni kurudi. Unaoneje, tutarudi na zoho zetu?".

Wakati Joram na Nuru walipokuwa wakizungumza hayo, Kombora alikuwa Ikulu mbele ya Rais akitokwa na jasho jembamba. Alifika ofisini, akiwa hoi kwa ukosefu wa usingizi wa siku kadhaa. Mara alipopata simu ambayo ilimtaka kwenda Ikulu mara moja, alilitia gari lake moto na kufunga safari hiyo ya dharura hadi Ikulu ambako alielekezwa katika chumba cha faragha. Humo aliwakuta Rais, Waziri Mkuu, Waziri wa Ulinzi na Katibu Mkuu katika Wizara ya Ulinzi. Aliwasalimu kishujaa, ingawa tayari moyo ulikuwa ukimdunda kwa kujua kuwa hakuwa tayari kuyajibu maswali yao.

"Nini hiki? Rais alimwuliza akimsogezea kijibarua ambacho kiliandikwa kwa mkono.

Kombora alikipokea na kukitazama. Hakuwa na haja ya kukisoma kwani ilikuwa moja kati ya zile barua ambazo zilikuwa zikiwafikia wakubwa wa nchi za mstari wa mbele mara kuwatisha ili waache msimamo wao dhidi ya Afrika Kusini.

"Isome," Rais alihimiza.

Kombora akakisoma. Mara alielewa sababu ya kusisitiziwa aisome. Ilisema: "ONYO LA MWISHO." Ikarudia kutaja sehemu muhimu ambazo aliyeandika barua hiyo alikusudia kuzichoma, sehemu ambazo ni pamoja na Ikulu. Baada ya kuikodolea macho, Kombora aliyarudisha katika uso wa Rais. "Nimeisoma mzee."

"Barua hiyo imekutwa katika ofisi yangu," Rais alieleza. "Ni dhahiri kuwa aliyeileta anao uwezo na nafasi ya kufanya lolote katika nchi na ofisi hii. Kwanini mmempa haki hiyo?"

Kombora hakujibu. Hakujua ajibu nini. Yeye na vijana wake wote walikuwa taabani katika mapambano haya. Majasusi wengi ya Afrika Kusini yalishikwa, lakini halikutokea lolote ambalo lingeweza kusaidia kukomesha vitisho vya ainaaina. Mengi yalikuwa majasusi wa kawaida, ambayo ama hawakuwa na lolote la haja au yalitumwa kwa ajili ya masuala yasiyo na uzito mkubwa. Wapelelezi wake ambao walikuwa nje pia walivitesa vichwa vyao bila ya kupata matunda ya kuridhisha. Nusura Kombora apate hasira kwa lawama hizo ambazo hakuona kama zinamstahili. Alitamani ainuke, atangaze kujiuzulu. Lakini hayo hakuyafanya kwa kukumbuka kuwa hasira si dawa. Na licha ya hayo aliona wazi kuwa lawama zilimstahili. Kufanya kazi ni kupata matokeo ya kazi hiyo. Kazi isiyo na matokeo haiwezi kuitwa kazi.

"Sina haja ya kukulaumu," Rais aliendelea. "Nauona ugumu wa jukumu mlilonalo. Nilichokuitia ili kukukumbusha kwa mara nyingine ni kuwa hata kwa bei ya roho zetu hatuwezi kukubali kufuata masharti ya utawala huu dhalimu. Lazima tupambane nao. Na huu ni wakati pekee wa kuonyesha moyo wetu. Uoga hauwezi kutufanya tukubali kuwa mateka wa utawala haramu kama huu. Lazima tushinde," akasita kidogo akimtazama Kombora kwa makini. "Inspekta," aliongeza kwa sauti ya amri kidogo. "Huu ni wakati wako. Kuna wakati wa njaa; wakulima hutakiwa kuiokoa nchi; wakati wa uhaba wa fedha za kigeni wafanyakazi viwandani huombwa kujitoa mhanga; wakati wa vita jeshi hulazimika kulinda nchi. Huu ni wakati wako, Inspekta. Nchi inakuhitaji na kukutegemea. Gavana wa Benki amepewa amri ya kukupa kifungu chochote cha pesa unazohitaji, Mkuu wa jeshi ameambiwa akuruhusu kutumia kikosi chochote na Bunge limependekeza uruhusiwe kufanya lolote. Kazi kwako," Rais alimaliza akainuka na kutoka.

Kombora alipumbazuka kidogo juu ya kiti hicho. Jasho jembamba lilikuwa likimtoka. Mara akajilaani kwa kusita kuleta barua ya kujiuzulu kwake. Hakujua angefanya nini zaidi. Aliwatazama viongozi ambao walikuwa wametulia, wakimtazama. Kiongozi mmoja alitamka neno ambalo halikumfikia Kombora. Mwingine alitikisa kichwa. Kombora akainuka na kuwaaga. Alipoifikia gari yake ndipo alipokumbuka kuwa ile barua ya vitisho bado alikuwa nayo mkononi. Akaitia mfukoni na kuamuru gari limrudishe ofisini.

***

Kidole kimoja kamwe hakivunji chawa; Kombora aliwaza akiwa kaketi ofisini mwake akifikiria afanye lipi zaidi kufanikisha vita hivi ambavyo havikuwa na uelekeo maalumu. Akamwagiza opereta wake kumpatia viongozi wa ofisi zote za usalama katika nchi za mstari wa mbele, pamoja na Naijeria. Alipowapata alipanga nao kufanya mkutano wa dharura ambao ulikusudiwa kujadili hali inayozikabili nchi zao. Ilikuwa kama wote walikuwa wakiusubiri kwa hamu wito huu. Wakaafikiana kukutana Jijini Dar es Salaam siku mbili baadae.

Kombora, akiwa mwenyeji, alikuwa Mwenyekiti wa Mkutano huu uliofanywa kwa siri kubwa. Mkutano huu ulijumuisha watu wenye sura mbalimbali, umri tofauti, viwango tofauti vya elimu; wote wakiwa na dhamira moja. Kila mmoja alieleza tishio lililokuwa likiikabiri nchi yake na kila mmoja alieleza hatua ambazo tayari zilikuwa zimechukuliwa. Lakini wote waliafikiana kuwa matunda ya juhudi zao hayakuwa ya kuridhisha. Wote walifahamu kuwa matunda ya maafa yaliyokuwa mbele yao siku za usoni, endapo yasingekomeshwa, yangesababisha maafa na vilio ambavyo historia haikupata kuvishuhudia.

"Jambo linalotisha zaidi ni maoni au hisia za wanasayansi wetu," mjumbe mmoja alieleza. "Wanaamini kuwa moto huu unatokea angani katika chombo ambacho hakionekani kwa macho. Hivyo, jukumu letu ni kukilipua chombo hicho. Tutawezaje wakati hatukioni?"

"Labda tuilazimishe Afrika ya Kusini ikiteremshe."

"Hilo ndilo tatizo. Tutawezaje kuilazimisha? Tumejaribu kutazama uwezekano wa kuishambulia kijeshi kwa pamoja na kuona si rahisi. Wao wamejiimarisha sana kiulinzi angani, majini na nchi kavu. Nasi Waafrika umoja wetu unalegalega kiasi kwamba hatuwezi kuafikiana mara moja. Vilevile, wakati tutakapokuwa tukijiandaa kwenda huko madhara waliyotishia yatakuwa yakiendelea kutukia."

"Lakini haiwezekani tukubali kuwa hatuwezi kufanya kitu," Kombora alieleza kwa sauti. "Lazima tufanye jambo. Jema au baya, lazima tulifanye mapema."

Aliungwa mkono.

Mara simu ikaroma katika meza ya Kombora. Akaitazama saa yake na kuona kuwa zilikuwa zimesalia dakika nane kutimia saa kumi za alfajiri. Akainua simu hiyo na kusikiliza. Ilipigwa na msaidizi wake ambaye alimwomba atoke nje mara moja. Kombora akawataka radhi wageni wake na kutoka.

Dakika chache baadaye alirudi ndani akiwa kaandamana na mgeni mmoja ambaye alikuwa katika hali ya kusikitisha. Mgeni huyo alikuwa mtu mweupe, aliyevaa mavazi yaliyochakaa. Mwili wake ulikuwa umejaa majeraha na mikwaruzo mingi kiasi cha kumfanya aonekane mahututi. Hata hivyo, macho yake yalikuwa na uhai.

"Huyu ni mgeni ambaye amekamatwa huko mpakani mwa Malawi na Tanzania leo," Kombora alieleza. "Amesema ametoroka kutoka Afrika ya Kusini kuja baada ya kuponea chupuchupu. Maelezo yake nadhani yatatufaa katika kikao hiki," alimaliza akimwashiria mtu huyo kujieleza. "Kwanza ningependa ieleweke kuwa mimi sio mzungu, "mtu huyo alisema. "Mimi ni mtu mweusi, mzaliwa wa Soweto," alisema akifungua vifungo vya shati lake. Kila mmoja alitokwa na macho ya mshangao kwa kuona kuanzia tumboni alikuwa na ngozi nyeusi. "Ngozi hii nyeupe iliyokaa usoni na mikononi ni matokeo ya plastic surgery ambayo nilifanya miaka kumi iliyopita ili niweze kuingia miongoni mwa makaburu na kuiba siri zao ili zitusaidie katika vita vyetu vya kujikomboa," alisita kidogo. Kisha akaendelea. "Nimefanya kazi mbalimbali katika jeshi hilo, daima nikiwa macho kupeleleza hiki na kile. Majuzi ndipo nilipogundua jambo la kutisha zaidi. Niligundua kuwa umejengwa mtambo ambao unaendesha Setilaiti ambayo haionekani kwa macho inayotumiwa kuteketeza majumba na sehemu muhimu za kiuchumi katika nchi za kiafrika. Nikaanza upelelezi wa makini kutafuta uwezekano wa kuangamiza tishia hilo. Kwa bahati mbaya, walinishuku katika upelelezi wangu. Sikuwa na la kufanya zaidi ya kuikimbiza roho yangu. Hata hivyo, nimeona mengi, nadhani naweza kutoa mchango madhubuti ambao utatuwezesha kushinda."

Wakuu hao wa upelelezi walimtazama mtu huyo kwa makini kisha wakatazamana. Mmoja alicheka, mwingine akatabasamu.

"Hatimaye...." mmojawao alinong'ona.

*****SURA YA NANE*****

KATIKA jumba fulani, mtaa fulani, jijini Johannesburg, makaburu wanne waliketi katika ofisi moja wakisikiliza taarifa za kijasusi kutoka Tanzania. Jasusi moja lilikuwa likiwaarifu kwa kutumia chombo maalumu juu ya msafara wake na mafanikio ya shughuli zake.

"Nimefika salama na kuwakabili nikiwa katika hali ya kusikitisha iliyonifanya niaminike kama mmoja wao. Wameumeza kabisa uongo wangu. Sasa hivi wananiamini sana. Wameniuliza mwaswali mengi na nimewajibu kiume nikiwapa taarifa za uongo. Nadhani wamekusudia kuwatuma wapelelezi wao huko, ingawa hawakupenda kunishirikisha moja kwa moja. Hata hivyo, msijali, nitakuwa macho nikiarifu kila kitendo chao hatua kwa hatua."

Makaburu wakatazamana tena na kutabasamu kwa namna ya kupongezana. Mmoja wao hakuona kama tabasamu linamtosha. Yeye aliangua kicheko. Kisha aliona kicheko hakitoshi. Akainuka na kuliendea kabati lililokuwa nyuma yake ambamo alitoa chupa kubwa ya pombe kali, aina ya JohnWalker na glasi nne. Akazileta mezani na kuziweka mbele ya kila mmoja. Akaifungua na kumimina. "Lazima tusherehekee ushindi." Baadae akaongeza, "Sitoi ruhusa ya kunywa ofisini isipokuwa inapobidi kufurahi. Mwanadamu hana budi... Cheers..."

Kaburu huyu kwa jina aliitwa Von Iron, kwa sura hakutofautiana sana na mtoto mchanga ingawa kiumbo alikaribiana na kiboko aliyeshiba vizuri. Yeye ndiye aliyekuwa kiongozi wa kamati hii maalumu ya BOSS ambayo iliundwa kuzishughulikia kikamilifu nchi za kiafrika 'zinazojitia kichwa ngumu.' Amekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa shirika hili la kijasusi tangu lilipoundwa miaka mingi iliyopita. Mara kwa mara kazi yake imekuwa nzuri kwa wakubwa zake. Haikupata kutokea mpango aliouandaa ukashindwa kutoa mafanikio, jambo ambalo lilimpa heshima na hadhi machoni mwa weupe na kumfanya jazanda ya mauti katika fikra za weusi. Ni yeye aliyebuni uwezekano wa kuitumia nguvu ya nyuklia kuwaangamiza Waafrika. Hakuwa Mwanasayansi, lakini alipewa jukumu la kushirikiana nao, akiwa na uhuru wa kutumia kiasi chochote cha pesa hadi majaribio yalipofanyika na kutoa matunda ya kupendeza. Kadhalika, ni yeye aliyebuni mpango wa kuwapa ngozi nyeusi baadhi ya wapelelezi wao, kwa kupoteza pesa nyingi katika hospitali zinazofanya Plastic Surgery. Watu hao waliingizwa kwa hila katika vikundi vya wapigania uhuru na kujifanya wenzao huku wakitoa siri zote na hata kuua inapobidi. Mmoja wa watu hao ni huyu ambaye alikuwa akiwafurahisha sana kwa taarifa zake kutoka Tanzania.

Yeye alifanyiwa mabadiliko ya ngozi yake miaka mitano iliyopita, akawa mweusi na kutibua mambo mengi katika chama cha SWAPO na ANC. Majuzi alirudishwa Ulaya ambako alirudishiwa ngozi ya mtu mweupe usoni na mikononi, kisha akatumwa Tanzania ambako waliona ni chimbuko la misukosuko yote dhidi ya utawala wao, na hasa ili wajue nini kinafanyika katika kutapatapa kwa Serikali na wananchi wa Tanzania juu ya mtambo wao wa aina yake ulioko angani baada ya kutoeleweka kilichomtukia mtu wao, Chonde, hata akafa katika hoteli moja. Zaidi, huyu alikuwa amepewa akiba ya kutosha ya zile gololi zinazouongoza mtambo huo kulipua miradi teule ili wakati utakapowadia waachie pigo hili walilokusudia kulifanya, "Pigo la mwisho."

Umaarufu wa Von Iron dhidi ya ngozi nyeusi ulichipuka katika roho yake tangu utotoni baada ya kukua katika familia ya kitajiri ambayo iliwatenda waafrika kama wanyama. Hayati baba yake alikuwa na mgodi wa dhahabu. Watumishi wengi walifanya kazi humo huku wakilipwa ujira hafifu mno kiasi cha kuwafanya washindwe kuyamudu maisha. Jambo hilo hakuna aliyeonekana kulijali, hata katika fikra za Von ikajengeka kwamba mtu mweusi ni chombo cha mtu mweupe, ambacho hakina haki wala thamani.

Halafu ikatukia maafa katika mgodi. Baba yake alikuwa katika moja ya ziara zake adimu wakati ilipotokea hitilafu hii ambayo hadi leo chanzo chake hakifahamiki. Hitilafu hiyo ilisababisha maafa makubwa kwa wafanyakazi wengi, weusi kwa weupe. Hayati Iron mwenyewe aliponea chupuchupu. Kama asingejitokeza mtumishi wa Kiafrika, mzee mkongwe, ambaye alitumia nguvu zake zote kumtoa katika chumba kilichokuwa kimefunikwa kwa mawe, siku hiyo angeyapoteza maisha yake. Hata hivyo, jukumu hilo lilimgharimu mzee huyo maisha yake kutokana na majeraha mabaya aliyopata. Kifo hicho kilimsikitisha sana mzee Iron hata akajitolea kuishi na mtoto pekee wa mzee huyo ambaye alikuwa msichana mzuri, ingawa uzuri huo ulipotoshwa na unyonge aliokuwa nao rohoni. Uamuzi wa kuishi na Mwafrika katika nyumba moja, ukiwa jambo geni sana wakati huo, uliisababishia familia yake mgogoro mkubwa, hasa mkewe. Lakini Iron hakulikubali hilo asilani. Badala yake akazidisha mapenzi kwa msichana huyo huku akiahidi kumpeleka masomoni, nje ya nchi.

Halafu ikatokea. Mzee Iron akafumaniwa na msichana huyo. Ilikuwa habari iliyojaa aibu kubwa masikioni mwa kila mtu mweupe. Lakini Iron hakuona aibu. Alikitetea kitendo chake na kukataa matakwa ya mkewe kwamba msichana huyo yatima afukuzwe. Hata mkewe alipotishia kujiua Iron hakukubali kumtupia msichana huyo lawama ambazo hazikumstahili. Ikatokea tena. Wakafumaniwa kwa mara ya tatu. Hapo mama Iron hakustahamili zaidi. Alirudi chumbani ambako alichukua bastola na kumwua msichana yule mweusi.

Mzee Iron alizirai kwa hasira. Fahamu zilipomrudia aliipokonya bastola hiyo kutoka mikononi mwa mkewe na kumpiga risasi mbili kifuani. Kisha alijilenga kichwa na kufyatua risasi zote zilizosalia. Vifo vyao vilikuwa simulizi kubwa mitaani kwa muda mrefu. Vilimwacha Von katika msiba wa uyatima, msiba ambao ulizaa hasira dhidi ya mtu mweusi; akijua kuwa ni mtu mweusi aliyemnyima haki ya kuwa na wazazi. Jambo hilo lilimfanya siku zote awe mstari wa mbele katika kutukuza na kutekeleza taratibu zote za ubaguzi. Daima alikuwa mkatili kuliko wakatili, mnyama kuliko wanyama dhidi ya mtu mweusi. Matokeo yake yakawa kupata vyeo vilivyomwezesha kuwa na mamlaka juu ya uhai na kifo kwa kila mtu mweusi katika shirika hili la kijasusi. Wengi waliuawa kwa ajili yake, mengi yaliendelea kufanyika ili kumkomoa mtu mweusi kutokana na mapendekezo yake. Lakini hakukoma kuendelea kubuni. Mtambo uliokuwa angani ukisubiri kuiharibu Afrika huru ulikuwa moja tu kati ya ubunifu wake.

Pamoja na kutenda mengi ya kikatili, pamoja na kuhakikisha watu weusi wengi wasio na hatia wakipoteza maisha yao, bado Von hakuona kama viumbe hawa walielekea kumpigia mtu mweupe magoti. Badala yake waliendelea kusimama kiume wakitetea haki yao. Alipokufa huyu, alizaliwa huyu, wimbo uleule ukiwa mdomoni. Hata Mandela, ambaye alikuwa kifungoni, alipoteswa bado aliendelea kuwa na msimamo uleule. Hilo, kiasi lilimtisha sana kaburu Von. Hakuwaelewa kabisa watu hawa. Wana nini katika damu yao?

Swali hilo lilikuwa likimletea maswali mengine ambayo yalijenga hisia fulani, maswali yaligongana kichwani mwake. Alikuwa akijiuliza: baba yake aliona nini katika nywele kavu, ngozi nyeusi na sura ya kusikitisha ya yule msichana wa Kiafrika hata akadiriki kumwua mkewe na kujiua mwenyewe! Aliwahi kusikia hadithi ya mtu mwingine ambaye alimwacha mkewe na kukimbia na msichana mweusi hadi Marekani ambako walifunga ndoa. Wana nini watu hawa? Iko siri gani ndani ya ngozi zao zinazotisha? Labda ingebidi alifumbue fumbo hili kwa kumpata mmoja ili aonje? Lakini...mweusi... Hapana. Mara kwa mara aliyafukuzia mbali maswali hayo ambayo yalimjia bila taarifa, hasa alipoukumbuka uyatima wake.

"Cheers," Von aliropoka tena.

Wenzake wakageuka na kumtazama kwa mshangao. Kisha wakatabasamu kimyakimya, wakiendelea kunywa taratibu. Baada ya vinywaji hivyo, Von aliamua waendelee na kikao chao.

Walivuta mafaili ya suala la Chonde na kuangalia wamefikia wapi juu ya kisa cha kifo chake na mali zake zilielekea wapi. Bado haikueleweka nani alimuua na maiti ya pili chumbani mle ilikuwa ya nani. Zaidi haikufahamika vitu alivyokuwa navyo, ambavyo ni vya hatari na siri kubwa, vilikwenda wapi. Kitu kimoja walikuwa na hakika nacho. Vitu hivyo havikufika mikononi mwa polisi, jambo ambalo liliwafanya waafikiane kuwa watu waliomwua Chonde na kumwibia pesa nyingi na vitu alivyokuwanavyo ni majambazi wa kawaida, ambayo yangevitupa vifaa vile muhimu kama takataka na nyaraka za siri kama uchafu. Kitu ambacho wangejua kukitumia ni pesa za Tanzania na za kigeni ambazo zingewachukua miezi mingi kabla ya kuzimaliza.

Pesa hazikuwa tatizo kwa akina Von. Walilitupa suala hilo kando bila kinyongo, hasa wakijua kuwa tayari mtu wao mwingine, Clay, alikuwa nchini Tanzania akiwa na kila kitu kilichohitajika na tayari kwa yote waliyohitaji kufanya. Alikuwa na nafasi nzuri zaidi ya Chonde kwani uongo aliokwenda nao ungemfanya aonekane kama almasi machoni mwa maafisa wa usalama wa nchi zote za mstari wa mbele za Kiafrika.

"Nadhani iliyobaki ni kuongeza ulinzi katika mtambo wetu," Von aliendelea. “Ingawa Clay yuko kwao na atatuarifu kila wanachokusudia kufanya, lakini kuna mengine watakayoshindwa kumwambia. Ni wazi kuwa watatumwa wapelelezi waje, lakini sitaki warudi. Nadhani tunaelewana." Akaungwa mkono.

Mara simu ya dharura ikaanza kulia. Ikiwa simu ambayo hulia kwa nadra sana, Von aliinua mkono na kuidaka mara moja. "Von hapa," akanguruma katika chombo cha kusemea.

"Bosi, hapa ni kikosi cha ulinzi wa anga. Ndege zetu za ulinzi zimeizunguka ndege moja ambayo ina watu wanne tu, rubani na msaidizi wake na abiria wawili ambao ni mwanamke na mwanamume. Rubani wa ndege hiyo anaomba kutua, akidai kuwa ametekwa nyara na abiria hao ambao wamejitambulisha kama Joram Kiango na mpenzi wake Nuru. Tunauliza kama tuwaruhusu kutua au tuwalipue".

"Nani, Joram?" Von aliuliza.

"Ndiyo. Joram Kiango. Yule..."

Mara Von akalikumbuka jina hilo vizuri. Halikuwa jina la kupendeza hata chembe masikioni mwake, ingawa siku mbili tatu zilizopita limesikika kwa namna ya kupendeza kiasi. Joram kuja Afrika Kusini! Baada ya kuharibu mipango yao mingi ya kuikomoa Tanzania! Bila shaka ni kujaribu kujificha baada ya kuiibia nchi yake akiba yote ya pesa za kigeni. Vizuri. Tutampa hifadhi ya kudumu. Anaweza kujificha milele katika makaburi yetu. Hatuna roho mbaya.

"Umesema Joram siyo? Sikia. Huna haja ya kutumia silaha kubwa. Anaweza kufa polepole. Mwambie atue."

Kwa Afrika Kusini ilikuwa kama nafasi ya dhahabu. Vyombo vyote vya habari vilishangilia kwa nguvu kuwasili kwa Joram na Nuru katika nchi yao. Waliipamba habari hiyo kwa kutia chumvi nyingi juu ya wizi wake. Walieleza jinsi alivyopokonya pesa hizo, alivyozitumia kwa starehe sehemu mbalimbali duniani, alivyofaulu kuwalaghai polisi wote wa dunia, na mwisho alivyoona hana hila zaidi ya kukimbilia Afrika Kusini, ili ajifiche maisha.

"Huu ni mfano hai kwa watu weusi kote ulimwenguni," mtangazaji mmoja wa televisheni alieleza. "Hakuna asiyemfahamu huyu Joram. Alijifanya mpigania haki, usawa na usalama wa watu wake. Amesababisha vifo vya watu wengi ambao walikuwa na nia njema ya kuikomboa nchi yake. Ndivyo walivyo watu weusi wote. Wanawalaghai wenzi wao na kuwafanya waote mikia misituni eti wakidai haki na uhuru. Matokeo yake ni kuwafanya, hao wenzi wao, vijakazi, wakati wao wakituna matumbo mara tu baada ya kupata madaraka. Natumaini watu weusi wote mnaodanganywa mtaitumia nafasi hii kuuona ukweli wa mambo. Ngozi nyeusi ni dalili ya laana. Nywele fupi ni dalili ya akili ndogo. Bila hekima na uongozi wa mtu mweupe Afrika ingekuwa bado gizani, na endapo ataondoka mtu mweupe giza litarudi..."

Hayo yalisemwa baada ya watu kuwatazama Joram na Nuru wakitoka katika ndege iliyowaleta, huku wakiwa wametanguliwa na rubani ambaye walikuwa wamemshikia bastola. Nje ya ndege Joram aliitupa chini bastola yake na kuweka mikono yake juu. Ndipo Polisi wa makaburu ambao walikuwa wameuzingira uwanja wakiwasubiri, wakajitokeza na kuwakimbilia. Wakawavamia na kuwakagua harakaharaka. Walipoona kuwa hawana silaha nyingine wakawaongoza kuliendea gari lililokuwa likisubiri. Muda wote huo kamera za televisheni na zile za wapiga picha wa magazeti ziliwaelekea Joram na Nuru kwa ukamilifu. Kama kuna chochote kilichowashangaza watazamaji ni jinsi sura za vijana hawa zilivyoonekana tulivu, nzuri, zisizo na dalili zozote za ugangwe kama walivyotegemea.

Msafara wa gari uliishia katika jumba moja kubwa lenye ghorofa kadhaa. Humo, badala ya lifti waliyoingia kuwapandisha juu iliwateremsha chini ambako walijikuta katika chumba kilichoelekea kuwa maalumu kwa kuhoji mateka. Askari waliokuwa nao waliamuru kusubiri, kisha wakatoka na kuufunga mlango nyuma yao. Baada ya muda waliletewa chakula na vinywaji. Wakala na kunywa.

ITAENDELEA............

Post a Comment

0 Comments