TUTARUDI NA ROHO ZETU? (05)


 ILIPOISHIA................

Kumbe alikuwa fisi katika ngozi ya kondoo. Huyu, Uingereza haiwezi kumstahamili. Lazima apatikane, ahukumiwe na kupokonywa kila senti aliyobaki nayo.”

Nuru alimaliza kuisoma habari hii huku akitetemeka kidogo. Lakini ilimshangaza alipoinua uso na kukutana na ule wa Joram ambao ulikuwa ukichekelea. Hilo lilimshangaza. Akiwa mtu ambaye ameishi na Joram kwa kipindi cha kutosha, alikuwa na hakika kuwa amemfahamu Joram vya kutosha. Asingelaghaika kama watu wengine kung'amua wakati gani anacheka kwa hasira na wakati upi anajifanya kuchukia hali amefurahi. Tabasamu hili, ambalo lilikuwa likiendelea kuchanua katika uso wa Joram, halikuwa tabasamu batili, bali tabasamu halisi, tabasamu ambalo huutembelea uso huu kwa nadra sana. Hivyo, ilimshangaza sana Nuru. Alimtegemea Joram kujisingizia kucheka huku rohoni akibabaika na kukata tamaa. Si kushangilia kama aliyepata tuzo au ushindi mkubwa baada ya shindano gumu.

"Sijakuelewa Joram, sidhani kama hii ni habari njema," alimwambia.

"Wala sidhani kama una haki ya kutegemea habari njema tangu ulipokubali kuandamana na mwizi mkubwa kama huyu," Joram alimjibu taratibu. Alipoona uso wa Nuru bado una maswali na dalili za kutoridhika, aliongeza, "Kinachonichekesha ni huyu Mwingereza anavyojifanya ana uchungu na nchi yetu kuliko sisi wenyewe. Utafiti aliofanya hautokani na moyo wake wa kuwajibika bali ni nguvu alizonazo kiuchumi, uwezo ambao ameuiba toka katika makoloni miaka nenda rudi." Alikohoa kidogo kabla ya kuongeza, “Hawawezi kunitisha kabisa. Nitaishi hapa nikistarehe katika jiji hili kubwa ambalo linapendeza kwa madini yaliyoibwa toka makwetu, yaliyochimbwa kwa jasho la babu zetu. Nitaondoka hapa tu tutakapokuwa tayari kuondoka. Sivyo, dada Nuru?"

"Nilichosema ni jinsi unavyoifurahia habari hii badala ya kuionea aibu. Sikutegemea. Au nakosea. Pengine hili ni fumbo jingine?" Joram hakumjibu.


SASA SONGA NAYO...................

Jioni hiyo maisha yaliendelea kama kawaida. Joram alijipitisha hapa na pale akifanya hili na lile. Sasa ilikuwa dhahiri kwa Nuru kuwa alikuwa katika shughuli kubwa na ngumu kinyume cha alivyoiruhusu sura na sauti yake kuonyesha. Nuru hakujisumbua kumuuliza lolote akichelea kupoteza muda wake kwani ingekuwa sawa na kumpigia mbuzi gitaa ukimtegemea kucheza rumba. Hata hivyo, Nuru alipopata wasaa alimkabili Joram na kumwambia taratibu,"Unadhani mwandishi yule anatania anaposema watafanya juu chini kututafuta? Huoni kama tunaweza kupatikana? Hila hizi za kujibadili si zimekuwa teknolojia ya kawaida siku hizi? Sidhani kama zinaweza kutusaidia."

"Najua, mpenzi. Ninachojivunia ni wingi wa watu na ukubwa wa jiji hili. Itachukua muda hadi wafike hapa na kutukamata. Wakati huo hatutakuwa hapa tena, bali tutakuwa angani tukimalizia kuitembelea nchi ya mwisho ya dunia. Usijali Nuru. Starehe bila hofu yoyote..."

Joram hakuumalizia usemi wake kabla ya kuusikia mlango ukigongwa. Wakatazamana huku wakisikiliza. Mlango uligongwa tena kwa nguvu kuliko mwanzo. Joram hakuwa mgeni na ugongaji wa polisi. Kwa mara ya kwanza akajikuta kuwa alikuwa amekosea sana kuwadharau polisi wa Uingereza kiasi hicho. Akamtupia Nuru jicho ambalo lilibeba ujumbe ambao masikioni mwa Nuru ulieleza waziwazi "Cheza nao." Papo hapo akatoka na kuingia bafuni huku akiufunga mlango nyuma yake.

Mlango ulipogongwa tena Nuru aliinuka na kuufungua. Kama alivyotegemea mlango ulipofunguka aliingia askari mmoja mwenye cheo cha Sajenti akifuatana na mmoja kati ya maofisa wa hoteli hiyo.

"Samahani sana dada," afisa huyo alieleza. "Tumelazimika kukusumbua kidogo. Nadhani utatuwia radhi. Huyu hapa ni Sajini Brown kutoka Scotland Yard, yuko katika ziara ya kuwatembelea wageni wote wa hoteli hii ili kutazama hati zao za usafiri na maswali madogo madogo ambayo nadhani utamjibu. Ni mzunguko wa kawaida tu kwa ajili ya tukio dogo ambalo wangependa kulikamilisha ili wasirudi tena katika hoteli hii."

"Bila samahani,"Nuru alijibu akimgeukia polisi huyo ambaye alikuwa akitoa kitambulisho chake.

"Kwa kawaida hapa kwetu hatusumbui wageni," askari huyo alieleza. Tunatimiza ombi la INTERPOL tu," alisita akimtazama Nuru kwa makini zaidi. Sijui dada unaitwa nani?"

"Mrs Prosy Godwin".

"Kutoka?"

"Naijeria".

"Yuko wapi bwana Godwin?"

"Ametoka, nadhani atarudi baada ya dakika chache."

"Naweza kuona hati zenu za usafiri pamoja na nyaraka nyingine kama zipo?"

"Bila shaka," Nuru alimjibu akiendea mfuko ambao aliufungua na kutoa hati. Akazikabidhi kwa askari huyo ambaye alianza kuzipekuapekua.

Dakika hiyohiyo mlango wa bafu ulifunguka. Askari alipogeuka kutazama alikutana na pigo ambalo lilitua katika shingo yake kikamilifu. Pigo lililokusudiwa kummaliza, lakini halikutimiza wajibu. Lilimfanya apepesuke na kuegemea ukuta. Mkono wake ukapaa kukinga pigo la pili huku mkono wake wa pili ukisafiri kuitafuta bastola. Joram hakuruhusu mkono huo utoke na bastola. Aliachia judo ambayo ilitua ubavuni mwa askari huyo na kumlegeza. Pigo lililofuata lilimlazimisha kuanguka sakafuni. Baada ya kazi hiyo ndipo Joram alipomgeukia afisa wa hoteli ambaye alikuwa kaduwaa, mdomo wazi, kama asiyeamini macho yake.

"Mwinue ndugu yako na umpeleke bafuni," Joram alimwamuru.

"Vipi bwana Godwin? Nadhani hukumwelewa huyu bwana. Alikuwa hana nia mbaya zaidi ya... ya..."

Joram hakuwa na muda wa kuchezea. Alijua afisa huyu alihitaji nini kumtoa mshangao. Pigo moja tu, ambalo halikutegemewa lilimfanya afisa huyo aanguke chini kama gunia. Hima, Joram alianza kuwavutia bafuni mmoja baada ya mwingine. Kisha aliufunga mlango wa bafu kwa funguo na kumfuata Nuru ambaye pia alikuwa ameshangaa.

"Kwa nini umefanya hivyo Joram? Haikuwepo kabisa haja ya kuwashambulia. Askari huyo asingegundua lolote. Sasa watajua kuwa uko hapa na wataanza kututafuta kwa udi na uvumba."

Si kitu. Kwa nini tujikombekombe kwao? London si mji mzuri pekee yake katika dunia hii. Bado tuna haja ya kuiona miji mingine."

***

"…Ni mtu wa hatari duniani. Ameidhihirishia dunia kuwa hana tofauti na yule mwuaji mwingine anayetafutwa duniani kote, Carlos. Sasa kinachotakiwa kufanyika si kumtafuta yeye bali roho yake. Vinginevyo, dunia itakuwa imestarehe ikisubiri kuimarika kwa kiumbe mwingine wa hatari zaidi ya faru mwenye wazimu.”

Hayo yalikuwa mapendekezo ya mwisho katika gazeti lile lililohisi kuwepo kwa Joram Jijini London, na hatimaye kuandika juu ya tukio la kutisha lililowapata askari wa Scotland Yard na Afisa wa hoteli. Watu hao ambao walifunguliwa kutoka katika bafu saa kadha wa kadha baada ya Joram kuondoka zake, walieleza jinsi walivyowakabili watu ambao mtu yeyote asingefahamu kuwa wangeweza kuwa Joram Kiango na Nuru. Askari huyo alieleza hayo akiwa katika chumba cha X-ray, kuangalia uwezekano wa kuungika kwa mbavu zake tatu zilizovunjwa na Joram.

Baada ya kuongea nao kwa marefu na mapana ndipo waandishi wa gazeti hilo wakatoa habari hizo zikiwa zimepambwa kwa picha nyingi za kuchora, picha ambazo ziliwachora Joram na Nuru katika sura na mavazi tofauti; wakijaribu kuonyesha jinsi gani wanavyoweza kujibadili. Chini ya michoro hiyo kulikuwa na maelezo yaliyoandikwa kwa herufi nzito yakisema; "Unashauriwa kujihadhari nao. Ukimwona ua kwanza, uliza maswali baadaye."

Gazeti hilo lilisomwa kote duniani. Maelezo yake yalidakwa na TV na redio zote duniani. Watu wengi, ambao walimchukia Joram walizidi kushangilia, hali wale waliompenda walizidi kushangaa.

"Sijui amepatwa na nini mtoto huyu,"Inspekta Kombora alifoka huku akilitupa gazeti hilo mezani. "Yuko London na anafanya anavyojua. Anazidi kulipaka matope jina lake ambalo tayari amelichafua.”

Ilikuwa dhahiri kwa yeyote amtazamaye Kombora machoni kwamba alikuwa hajapata usingizi wa kutosha kwa muda mrefu. Mambo mengi yalimkabili kichwani kiasi cha kumpokonya hata hamu ya kula. Angewezaje kustarehe wakati siku zilikuwa zikisogea huku halijapatikana lolote la haja katika kukomesha tishio kutoka nchi adui ambalo lilitaka serikali iache msimamo wa kimapinduzi, la sivyo ajali zingeendelea kutokea. Tanzania kuacha kuzisaidia nchi zinazopigania haki na uhuru wake ilikuwa ndoto ya kupendeza. Kamwe isingetokea. Lakini kuendelea kusaidia nchi hizo huku ukisubiri maafa ya hatari sana, kwa nchi yake na rafiki zako hali huna uwezo wa kufanya lolote ilikuwa ndoto ya kusikitisha sana, ndoto ambayo ingeweza kutokea.

Walikuwa wamefanya yote ambayo wangeweza kufanya katika juhudi za kuhakikisha usalama. Yote; mema kwa maovu. Magereza ya Keko na Ukonga yalikuwa yamejaa wageni wengi ambao ama waliingia nchini kinyume cha utaratibu, au hati zao zilitia mashaka. Wote hawa walihojiwa kwa maneno na vitendo. Waliokuwa watakatifu waliachiwa, wenye madhambi ya magendo na uzururaji wakifunguliwa mashitaka. Ni mtu mmoja tu ambaye alielekea kuwa na mengi au machache ambayo yangehusiana na usalama wa nchi.

Huyu alikamatwa katika hoteli ya New Africa baada ya kulala hapo kwa siku moja. Wapelelezi walimshuku baada ya kumsikia akiulizauliza maswali juu ya watu walikufa katika hoteli hiyo; ni wa aina gani na walikufa vipi. Alipokamatwa na kutakiwa kutoa vitambulisho, hati zake zilionyesha kuwa ni mwanachama wa ANC ambaye ametoroka kutoka Namibia. CID waliwasiliana na ofisi hizo. Jina la Kweza halikuwemo katika orodha ya wanachama wa ANC. Ndipo lilipofunguliwa bomba la maswali dhidi yake. Na ni hapo ilipodhihirika kuwa hakuwa mtu wa kawaida jinsi alivyoweza kuyajibu maswali yote kwa ukamilifu kama ambaye alijiandaa kuyajibu.

Begi lake ambalo lilikaguliwa harakaharaka bila ya kuonekana chochote, lilipekuliwa tena. Baada ya jitihada kubwa iligundulika mifuko ya siri ambayo ilificha silaha, vyombo vya mawasiliano na vitu mbalimbali vya kijasusi. Alipoulizwa alikovipata alikanusha kuwa havifahamu, wala hakupata kuviona vitu hivyo. Ni majibu hayo ambayo yalimuudhi Kombora hata akaamua apelekwe katika chumba cha mateso ili, kama hasemi, autapike ukweli. Taarifa zilizomjibu Ispekta Kombora zilisema kuwa alikuwa hajasema lolote.

Ndipo alipolitupa gazeti alilokuwa akisoma habari za Joram, na kumtoa akilini kwa muda. Akaondoka na kuingia katika lifti ambayo ilimteremsha chini ya ardhi kiliko chumba cha mateso. Kombora hufika katika chumba hiki kwa nadra sana. Harufu ya mchanganyiko wa damu, kinyesi, jasho na machozi ni jambo moja ambalo humfanya aape kuwa asingerudi tena kila anapofika humu. Jambo jingine ni sura za watesaji. Sura hizi humtisha zaidi ya mateso yenyewe, zikimfanya aamini kuwa watu hao kama kweli wana roho, basi wana roho za chuma. Nayo macho ya wanaoteswa si jambo ambalo macho ya mtu mstaarabu yatapendezwa kuangalia.

Leo hii alimkuta Kweza, au kilichosalia katika umbo la aliyekuwa Kweza; akiwa amelala sakafuni, sura yake ikiwa haitambuliki kwa kuvimba na kuchubuka. Vidole vyake vyote tayari vilikuwa vimevunjika, jicho moja limetumbuka na meno manne yamepotea. Watesaji walikuwa wamemwinamia wakimdunga sindano ambayo ilikuwa na waya, iliyotokea katika soketi ya umeme.

"Mwachieni kidogo," Kombora aliamuru akikiendea kiti na kuketi. "Mleteni hapa."

Kweza alisimamishwa mbele ya Kombora, akitetemeka kwa uchungu na maumivu makali. Nusura Kombora amhurumie, huruma hiyo ilimtoka mara moja mara alipomfikia mtu huyo; mtu mweusi; kibaraka, msaliti wa juhudi za weusi wenzake katika kujikomboa kutoka kwenye udhalimu ambao umewaandama miaka nenda rudi. Mtu kama huyu ahitaji kuhurumiwa hata chembe.

"Wewe!” Akafoka. "Kwa nini hutaki kusema ukweli? Kama ukisema ukweli tutakuacha uende zako."

Pamoja na maumivu aliyokuwanayo mtu huyo, alicheka, "Nimekwisha sema kila kitu. Tatizo lenu ni kwamba hamtaki kuelewa ninachosema. Na juu ya kuniacha niende zangu nimewaambieni mara nyingi kuwa sihitaji kwenda popote. Naomba mkichoka kunitesa, mniue."

"Umesema ukweli? Ukweli gani?"

"Nimesema kuwa mimi sifahamu chochote juu ya maswali mnayoniuliza. Nilichofuata ni kumtafuta rafiki yangu Chonde ambaye inasemekana amefariki. Nilitaka kufahamu amefariki vipi ili niitulize roho yangu.

"Chonde rafiki yako vipi?"

"Alikuwa rafiki wa kalamu. Sikuwahi kuonana naye ana kwa ana."

Kombora alimtazama kwa makini. Macho yake makali yalimfanya Kweza aangue tena kicheko dhaifu huku akisema, "Mnaupoteza bure muda wangu na wenu. Mimi sifahamu chochote. Nanyi hamna lolote ambalo mnaweza kufanya zaidi ya kusubiri maafa kama nilivyoambiwa. Mwenye akili ningemshauri aikimbie nchi hii mapema badala ya kusubiri kifo cha kutisha cha moto mkali utakaokuja na ufukara wa kutisha baada ya moto huo." Akaangua kicheko kingine dhaifu. Safari hii alicheka kwa muda hata akateleza kutoka mikononi mwa askari waliomshika na kuanguka chini. Hapo chini alitulia kwa muda kisha akapapatika na kukata roho.

Kombora na wenzake walisogea na kuimana wakimtazama. Hakuna aliyefahamu kama alikuwa na sumu kinywani au aliitapika roho yake. "Miujiza, iliyoje!”

WALIKUWA wameitembelea miji mingi maarufu ya dunia. Walionja anasa na starehe za kila mji. Baada ya kutoroka kutoka London kwa hima walikwenda Ufaransa ambako walipitia miji mbalimbali na kuingia Paris. Toka Paris walikwenda New York ambako hawakukaa sana kabla ya kuruka tena hadi Washington, HongKong, Moscow na kwingineko.

Ingawa ziara yao ilikuwa ya starehe, lakini ilikuwa ziara ngumu kiasi cha kumtatanisha Nuru na kumsisimua Joram. Safari zao nyingi zilikuwa za kujifichaficha usiku na mchana kuwaepuka polisi na wapelelezi ambao ama walimhitaji Joram kwa makosa ama kuzishuku hati zao za usafiri, ambazo mara kwa mara zilikuwa za bandia. Hila za hali ya juu, pamoja na ruswa nzito, ni njia pekee iliyowafanya wafanikiwe kuiepuka mitego yote ya CID, KGB, INTERPOL na wapelelezi wa nchi mbalimbali.

Katika tukio moja kwenye mji mmoja, ilimlazimu Joram kujifanya mwanamke malaya ili kuwaepuka polisi ambao waliizingira hoteli aliyokuwemo. Polisi hao walipoingia katika chumba ambamo walitegemea kumnasa Joram walijikuta wakirudi nje kwa aibu baada ya kukuta wasichana wawili, waliofanana kwa uzuri, wakiwa nusu uchi juu ya kitanda chao kwa namna ya kufanya mapenzi ya wao kwa wao. Wakati askari hao wakisubiri nje ili kuwahoji vizuri, Joram na Nuru walitumia dirisha kuondoka zao na kila kilichokuwa chao.

Katika tukio jingine Joram alilazimika kuiteka nyara ndege ndogo ya abiria na kuilazimisha kutua katika uwanja ambao haukukusudiwa jijini New York. Kutoka uwanjani hapo walipata kinga kwa risasi za askari walioizingira ndege hiyo kwa kuwachukua rubani na msaidizi wake huku wakizielekeza bastola katika vichwa vyao. Polisi walikuwa wakiwafuata kwa mbali, televisheni ikiwaona na kuwaonyesha kwa kila mtu. Lakini ilifika mahali ambapo si polisi wala rubani waliojua kilichotokea. Polisi waliikuta ndege hiyo ikiwa imesimama kando ya nyumba, marubani wakiwa usingizini kwa kunusa dawa fulani bila kutaraji. Watu walioshuhudia tukio hilo, wakiwa hawajui kinachotokea, walidai kuwa waliwaona "vijana wazuri" msichana na mvulana wakishuka kutoka ndege hiyo na mizigo yao na kuingia katika jumba la jirani ambamo hawakuonekana wakitoka tena.

Harakati na machachari yao katika miji mbalimbali ziliondokea kuwa habari ambazo ziliwavutia sana waandishi wa habari. Mara kwa mara televisheni, redio na magazeti zilitoa habari zinazowahusu; Leo kaonekana hapa; hapa kafanya hivi; pale alifanya vile, na kadhalika.

Habari hizo zilipambwa kwa picha zao zinazovutia, kurudiwarudiwa kwa historia ya maisha ya Joram kiango pamoja na kutiwa chumvi nyingi ili kugusa masikio ya watu wote na kumsisimua kila mmoja. Hivyo, jina lilipanuka na athari kuneemeka. Ilikuwa kama dunia imesita kushughulikia masuala yaliyo muhimu na kuandamana na Joram katika ziara yake hii ndefu, jambo ambalo lilimfanya kila mpelelezi kuwa na hamu kubwa ya kubahatika kumtia mikononi Joram ili amfikishe kunakohusika.

Jambo ambalo lilimshangaza Neema katika mkasa huo mzima ni jinsi ambavyo alielekea kufurahishwa na jinsi habari hizo za aibu juu yake zilivyopata nafasi kubwa katika vyombo vya habari. Iliendelea kumfurahisha Joram badala ya kumchukiza. Nuru ambaye alimfahamu Joram asivyopenda sifa alijikuta akijawa na msgangao kwa mabadiliko hayo ya Joram.

Hata hivyo mshangao wake ulianza kupungua pale Joram alipoanza au alipolazimika kumshirikisha katika baadhi ya mambo aliyokuwa akiyafanya. Jambo la kwanza lilikuwa mazoezi ya viungo. walifanya kila starehe, lakini baada ya starehe, wakiwa chumbani kwao, walifanya mazoezi makali ya viungo. Mazoezi ambayo awali yalimtoa Nuru jasho, machozi na damu. Lakini baada ya muda machozi na damu vilikoma na jasho kupungua. Akawa hodari, akiwa bega kwa bega na Joram katika kila jambo. Zoezi la pili lilikuwa la matumizi ya silaha mbalimbali ambazo Joram alikuwa akizinunua kwa siri sana.

Alimwelekeza Nuru namna ya kuzificha mwilini, namna ya kuzitumia na kumfundisha jinsi ya kulenga shabaha kwa ukamilifu. Nuru alikuwa mwepesi wa kuelimika.

Hayo yaliufanya moyo wa Nuru uwe na tumaini kubwa. Sasa aliamini kuwa Joram alikuwa na jambo fulani zito la muhimu ambalo alikuwa akishughulikia. Pengine katika safari hiZo za mji hadi mji alikuwa akimhitaji mtu kwa madhambi fulani. Mtu gani huyo? Na ni madhambi gani aliyoyafanya?

Maswali ambayo yaliimarika hasa kutokana na simu nyingi ambazo Joram alikuwa akipiga kwa rafiki zake sehemu mbalimbali ulimwenguni, ambazo mara kwa mara zilikuwa katika mafumbo ya aina aina. Japo alimsikiliza kwa makini Nuru hakuambua chochote cha haja, zaidi ya kuishia kuhisi tu. Wakati wote huo Joram hakukoma kujifungia.

Halafu ikaja jioni ya leo, ambapo Joram alionekana mtulivu kuliko ilivyokuwa siku zote. Sigara ziliteketea mdomoni mwake moja baada ya nyingine, macho yake yakimtazama Nuru ambaye alikuwa ameketi juu ya meza ya kuvalia akishughulikia nywele zake. Joram alimtazama kwa makini kwa dakika kadhaa, kisha alimsogelea na kumshika bega.

"Nilichoshika hapa ni kipande murua cha kazi ya sanaa ambayo ni mfano halisi wa kazi ya Muumba. Nadhani hana budi kujivunia mafanikio yake", alisema akitabasamu.

Nuru aliinua uso kumtazama.

"Kwa bahati mbaya kazi hii ya sanaa iki katika hatari ya kuharibika endapo itandelea kuandamana na binadamu wenye akili mbaya kama Joram Kiango".

Hilo lilimfanya Nuru atabasamu. Alijua Joram anaelekea wapi. Siku hizi mbili alikuwa akimchunguza kwa makini na kuona mabadiliko katika fikira zake. Alikuwa akiona na kushuhudia kutoweka kwa ile starehe ya kujisingizia katika nafsi ya Joram na badala yake starehe kamili kuchukua nafasi yake. Mfano wa mtu ambaye yuko katika jahazi hafifu katikati ya bahari iliyochafuka anapobahatika kufika pwani salama. Hivyo alijua kuwa Joram ana neno. Akamhimiza kulisema kwa kumwambia, "Unachotaka kufanya Joram ni kunitisha... Lazima uelewe kuwa sitishiki ng'oo. Tumekuwa nawe katika heri na shari. Tutakuwa pamoja jehanamu na peponi. Usijisumbue kuniambia lolote lenye dhamira ya kututenga".

Joram akacheka. "Una akili nyepesi sana Nuru", akamwambia. "Nilichokuwa nikielekea kukuomba ni kukushauri urudi nyumbani, uniachie kazi iliyoko mbele yangu. Ni kazi chafu, ya hatari, yenye nuksi, ambayo sidhani kama itanifanya nirudi nyumbani na roho yangu".

"Nimekwisha sema usijisumbue kunitenga. Nina hamu na kazi nzito, chafu yenye damu. Sijasahaun nilivyoshirikishwa kuwaangamiza wakuu wa nchi wasio na hatia. Nahitaji kujitakasa. Ni damu pekee itakayonitakasa. damu ya adui wa Afrika.

Joram aliduwaa huku akimtazama msichana huyo. Hakuwa na shaka kuwa msichana huyo ni shujaa. Lakini hakujua kuwa ni shujaa kiasi hicho. Ndiyo, alimtegemea sana katika msafara wake. Lakini hakukusudia kumwingiza katika mkasa ambao ilikuwa dhahiri kuwa pamoja na ugumu wa maandalizi yake ya muda mrefu hadi sasa matekeo yake yalikuwa gizani. Yeye alikuwa tayari kwenda, tayari kufanya kazi inayompeleka; uwezekano wa kurudi haukumsumbua. Kufa kusingemtisha sana mradi atakuwa ameifanya kazi yake. Kifo chake ni jambo moja, kusababisha kifo cha mtoto wa watu, mzuri kama Nuru, ni jambo jingine.

"Sikia Nuru. Labda huelewi... Nakusudia kwenda toka hapa sio nchi ya kawaida. Ni nchi ambayo kuna watu wenye kiu kubwa ya damu ya mtu mweusi na njaa kubwa ya roho zetu. Na ninahitaji kujipeleka moja kwa moja mikononi mwao. Kwa ufupi nategemea kwenda Afrika Kusini...".

"Tutakwenda pamoja".

...Na ninachokwenda kufanya ni hujuma. Wakinigundua watanitafuna mbichi".

"Watatutafuna pamoja".

Joram akaduwaa. "Labda nikufunulie kila kitu kilivyo Nuru", Joram akamwambia. ""Nisubiri", alisema akiliendea begi lake lililokuwa limefurika kwa vitabu aina aina pamoja na encyclopedia ambazo Joram alikuwa akizitumia kwa muda mrefu kujaribu kuyasoma yake maandishi ya kijasusi ambayo aliyapata katika mfuko wa hayati Chonde. Humo alitoa karatasi ndefu, iliyoandikwa kwa mashine, ikiwa tafsiri ya maandishi hayo. Alimkabidhi Nuru na kumwabia asome haraka haraka.

 ITAENDELEA..................

Post a Comment

0 Comments