TUTARUDI NA ROHO ZETU? (03)

 


ILIPOISHIA............

"Hata hivyo, sauti yako haifanani kabisa na madai yako Joram. Kuna watu ambao silika yao ni kukesha katika mabaa na madansi, wewe si mmoja wao. Kuna wanaostarehe kusubiri maafa ya kusikitisha, wewe si mmoja wao, Joram. Kuna wanaofurahia ladha ya pombe na utamu wa muziki zaidi ya kazi na ushujaa, wewe si mmoja wao vilevile."

"Zamani, Inspekta. Sasa hivi mimi ni mmoja wao na nitaendelea kuwa mmoja wao. Na kama huna maongezi mengine zaidi ya haya mzee nitashindwa kuendelea kukusikiliza," Joram alimaliza akitoa sigara yake na kuiwasha.

Kombora hakujua afanye nini ili amshawishi Joram. Alimtazama Nuru kama aliyehitaji msaada wake. Akayaona macho yake mazuri yaliyojaa huzuni katika hali ya kukata tamaa. Hilo, kiasi lilimfariji Kombora. Alifahamu kuwa anaye msaidizi ambaye angesaidia katika juhudi zake za kumrejesha Joram Kiango katika dunia ya Joram Kiango. Akiwa si mgeni katika dunia hii Kombora alielewa kuwa mwanamke mzuri ni silaha. Hivyo, akamtupia Nuru jicho la kumtaka aelewe kuwa anautegemea msaada wake. Kisha akainuka na kuaga bila ya kumaliza kinywaji chake.


SASA SONGA NAYO...........................

"Hukufanya vizuri, Joram," Nuru alimwambia.

"Mfuate mkafanye vizuri".

"Sivyo, sikia..."

Nuru akavunjika moyo. Uchungu mkubwa ukamwingia rohoni. Akajilazimisha kuendelea kunywa pombe, lakini haikumuingia. Baada ya jitihada nyingi alimtaka Joram radhi, akaondoka kutangulia chumbani kwao.

"SAMAHANI, naweza kuketi hapa?" mtu mmoja alisema akimsogelea Joram mara tu Nuru alipoondoka.

Alikuwa mtu wa umri wa kati. Sura yake ilionyesha dalili zote za kutosheka, macho yake yakionyesha kila dalili ya kuelemika. Kiasi alionekana kama ambaye pombe ilianza kumshinda nguvu, japo alitembea kwa uhakika.

Joram alimtazama kwa makini kabla ya kumjibu, "Una haki ya kukaa popote. Nchi huru hii."

"Asante," mtu huyo alijibu huku akijibweteka kitini. Baada ya dakika mbili tatu za kunywa na kuvuta kwa utulivu alimgeukia Joram na kumwambia, "Samahani. Sinabudi kulitoa dukuduku langu. Siku zote nimekuwa na hamu ya kuipata fursa hii ya kuketi nawe meza moja. Kama sikosei ni Joram Kiango." Joram alimtazama mtu huyo kwa makini. Alipochelewa kumjibu mgeni wake aliendelea, "Tumekuwa tukikutana mara kwa mara katika majumba ya starehe. Kilichonifanya nikufahamu ni msichana huyo mzuri unayefuatana nae. Kwa kweli, sina budi kukupa pongezi zako. Wazuri nimewaona wengi, wa aina yake sikupata kumwona. Ulimpataje yule dada, Joram?"

Jambo moja lilimvutia Joram katika kumsikiliza mtu huyu. Jambo la pili lilijitokeza. Sauti. Ilikuwa sauti ya kawaida, ikizungumza kiswahili cha kawaida katika masikio ya watu wa kawaida. Lakini katika masikio ya Joram Kiango, Joram ambaye sasa alikuwa amekaa chonjo, sauti hiyo ilificha uhalisia fulani.

"Unadhani una haki gani ya kunifahamu, na kumfahamu msichana wangu hali mimi sikufahamu hata kidogo?" Alimwuliza. Kama ambaye alilitegemea jibu hilo mgeni huyo alijibu mara moja, japo kwa kusitasita, "Mimi! kwa jina naitwa Ismail Chonde. Ni mfanyabiashara wa siku nyingi. Nimezaliwa na kukulia hapahapa ingawa siku hizi naishi Nairobi."

"Na unawezaje kunifahamu kwa urahisi kiasi hicho?"

"Nasoma vitabu, nasoma magazeti. Hakuna asiyekufahamu Joram." Sauti iliendelea kuwa na walakini katika hisia za Joram. "Inaelekea bado una maswali uliyotaka kuniuliza bwana Chonde. Nataka kumuwahi huyo msichana unayemwita mzuri".

"Kweli. Inaonyesha aliondoka hapa akiwa amechukia."

Joram alitabasamu. "Naona umeona mengi zaidi ya hilo."

"Ndiyo, nimeona na kusikia mengi. Kwa kweli, endapo hutaniona mlevi, nilichokusudia kuongelea ni yule mzee aliyekuacha muda uliopita. Namfahamu yule. Ana madaraka makubwa serikalini. Kama sikosei alikuwa akikushawishi utoe mchango wako katika kupeleleza matukio haya. Na niliona akiondoka bila furaha. Yaelekea umemkatalia. Hivi kweli umekataa katakata?"

Joram alimtazama kwa makini zaidi. "Sielewi maswali yako yanaelekea wapi," baadaye alisema.

"Inashangaza," Chonde aliongeza. "Joram ninayemfahamu mimi hawezi kuipoteza nafasi nzuri kama hii ya kuonyesha ushujaa wake. Afrika iko katika mashaka makubwa. Watu wanakufa hovyo. Majumba yanalipuka hovyo. Bara zima liko mashakani. Joram ninayemfahamu mimi angeitoa hata roho yake kujaribu kupambana na hali hii."

Joram aliipima sauti hiyo, akiilinganisha na uso wa msemaji. Ingawa aliongea kama mtu mwenye uchungu kwa nchi na bara lake, bado hisia fulani zilimfanya Joram aone kitu kama kebehi katika macho yake, kama kwamba alikuwa na hakika kuwa Joram na U Joram wake wote asingeweza kufanya lolote. Wazo hilo lilimuongezea Joram hamu ya kuendelea kumsikiliza.

"Bado sijaelewa unalotaka kusema," alichochea.

"Sidhani kama wewe ni mzito wa kuelewa kiasi hicho."

Wakatazamana, kila mmoja akimsoma mwenzake. Kisha Chonde aliangua kicheko kirefu kilichomwacha Joram akitabasamu. Baada ya kicheko hicho akaongeza, "Samahani endapo umeniona mhuni au mlevi. Sikuwa na nia mbaya zaidi ya kuzungumza nawe na kufahamiana. Kwa kheri." Aliinuka na kuondoka akielekea maliwatoni. Mwendo wake ulikuwa wa kilevi zaidi ya sauti yake. Joram aliendelea kunywa taratibu. Alipomwona rafiki yake huyo mpya akitoka nje ya hoteli na kusikia mlio wa gari likiondoka, akaenda mapokezi ambapo alimsalimu tena msichana aliyekuwa hapo na kumuuliza kwa upole, "Samahani dada. Hivi huyu bwana aliyetoka sasa hivi anakaa hoteli hii?"

"Yule, hakai hapa. Huwa anatokeatokea tu. Kila mara huja na msichana. Leo ndio kwanza nimemwona peke yake. Sijui wamekosana nini na msichana huyo, maana huyu bwana anaonekana pesa si moja kati ya matatizo yake," msichana huyo alieleza.

"Pengine hawajakosana," Joram alimchokoza.

"Wamekosana. Bila hivyo asingenikonyeza mara mbili."

Joram alicheka. Maongezi hayo yalikatizwa kidogo kwa simu ambayo msichana huyo alikuwa akiijibu. Alipotaka kuanza tena maongezi iliingia simu nyingine. Ambayo msichana huyo alionekana kuifurahia zaidi. Alizungumza kwa furaha huku akitabasamu. Baada ya kutoa chombo cha kuongelea alimgeukia Joram na kusema, "Unaona? Nimekwambia leo hana mtu. Ananiambia nikimaliza kazi nimkute hoteliya New Africa, chumba namba 104."

"Ndipo anapokaa?" Joram alihoji.

"Bila shaka."

Baada ya mazungumzo hayo Joram aliirudia meza yake na kuendelea kunywa. Mawazo yake yalimfikiria Chonde. Hakuelewa dhamira ya maongezi yake yote yale ilikuwa nini hasa. Alishuku kuwa pengine alikusudia kupata undani wa Joram na uamuzi wake. Kwanini? Zaidi Joram alishuku kuwa mtu huyo hawakukutana kuzungumza kiajaliajali, bali alikuwa akimfuata yeye au Kombora kwa ajili hiyo. Juu ya yote hayo zile hisia za Joram katika sauti ya mtu huyo zilizidi kujiimarisha akilini mwake. Aliona kama ulikuwemo walakini fulani katika sauti ya kiswahili chake ambao uliutia dosari Utanzania wake. Hayo na kile alichoona katika macho ya mtu huyo vilimtia Joram hamu ya kumfahamu vizuri.

Hivyo, dakika tano baadaye alijikuta mitaani akielekea New Africa. Alipofika hapo alimwendea mfanyakazi wa mapokezi na kujitia akizungumza naye hili na lile huku macho yake yakiwa kazini kutazama endapo ufunguo wa chumba namba 104 ulikuwepo. Aliuona. Akauliza juu ya mtu wa chumba fulani ambacho aliona ufunguo wake haupo.

"Yuko ndani. Ameingia sasa hivi."

"Ngoja nikamwone."

Badala ya kwenda chumba hicho, Joram alipanda gorofani hadi chumba namba 104 ambacho kilikuwa kimefungwa. Kuacha kwake tabia ya kutembea na bastola hakukumfanya aache kutembea na vifaa vyake vidogovidogo, kama funguo malaya ambazo hazishindwi kuifungua kufuli yoyote ya kawaida. Hivyo, kitasa hicho cha mlango wa Chonde kilimpotezea nusu dakika tu.

Chumbani humo, Joram aliurudisha mlango na kuufunga kwa ndani. Kisha aliangaza huku na huko kwa makini. Kilikuwa chumba cha kawaida kama vilivyo vyumba vingine vya hoteli. Hivyo, Joram hakuwa na kazi ngumu zaidi ya kupekuwa magodoro na viti. Hakuona chochote. Ndipo alipoliendea Kabati na kulifungua. Ndani ya kabati hilo mlikuwa na sanduku kubwa ambalo pia Joram alilifungua. Mlikuwa na pesa za kutosha pamoja na mavazi. Vitu hivyo havikumvutia. Macho yake yalivutiwa na makaratasi mbalimbali ambayo aliyapekua kwa makini. Mengi yalikuwa makaratasi ya kawaida ambayo yalimwezesha kumfahamu mtu wake kuwa aliitwa Afith Chonde. Baada ya kupekuwa zaidi aliipata hati yake ya usafiri. Aliifunua harakaharaka huku akisoma mihuri mingi iliyopigwa katika hati hiyo kuonyesha nchi Chonde alizozitembelea. Alikuwa anatembea sana. Mihuri ya Nairobi, Lagos, Lusaka, Harare, London, New York, Hong Kong, Tripol n.k ilionekana waziwazi. Hilo lilimfanya Joram azidi kuvutiwa na mtu huyo. Hakuonekana kama mfanyabiashara mkubwa kiasi hicho. Zaidi ya vipindi alivyokuwa akitumia mji hadi mji vilikuwa vifupi mno kiasi kwamba Joram alishuku kuwa hakuwa akifanya biashara za kawaida. Hivyo, akaongeza umakini katika upekuzi wake.

Kama alivyotegemea, Joram aliigundua mifuko ya siri katika begi hilo, mifuko ambayo maafisa wa forodha wasingeweza kuipata bila ya ujuzi maalumu. Katika mifuko hiyo, Joram alipata bastola moja aina ya revolver, maandishi mbalimbali ambayo alijaribu kuyasoma hakagundua kuwa hawezi kwani yaliandikwa kimafumbomafumbo katika hali kamili ya kijasusi. Pamoja na kijaluba kidogo cha chuma ambacho kilikuwa kimefungwa kwa ufunguo. Kijaluba hicho kilimvutia Joram zaidi. Alihisi kuwa kilikuwa kimeficha mengi zaidi ya yale aliyokwishayaona. Hivyo, akaanza kuzijaribu funguo zake malaya. Zilimchukua dakika kadhaa kugundua kuwa kamwe asingeweza kukifungua kijisanduku hicho. Kilitengenezwa maalumu kupambana na hila zozote za kufunguliwa pasi ya utaalamu wa mwenyewe. Kiu ya Joram juu ya kumjua vyema mtu huyu ikazidi kuneemeka. "Vipi awe na kisanduku kama hicho? Kilificha nini? Na maandishi haya ya siri yanasema nini? Siyo bure. Liko jambo," aliropoka.

"Ndiyo. Kuna jambo," sauti ilizungumza nyuma ya Joram. Akageuka hima na kukutana na uso wa Chonde ambao ulikuwa ukimtazama kwa kebehi. Alikuwa kaketi juu ya kochi. Alivyoingia chumbani humo kwa ukimya kama jini na kuketi kwa utulivu kwa kipindi chote hicho ni jambo ambalo lilizidi kumwongezea Joram ushahidi kuwa alikuwa hachezi na binadamu wa kawaida. Joram akageuka na kumtazama Chonde huku akiruhusu moja ya zile tabasamu zake za kishujaa, tabasamu ambalo lilifuatwa na sauti yake tulivu akisema, "Tuseme nimefumaniwa".

"Umefumaniwa. Na una bahati mbaya kuwa umefumaniwa na kifo. Binadamu hanichezei mimi na akaendelea kuishi," Chonde alisema akianza kuinuka taratibu. "Ulijifanya umeacha maisha yako ya kuingilia mambo yasiyokuhusu. Kumbe ulikuwa ukijifurahisha kwa kujidanganya mwenyewe. Umekosea sana." Akamtazama kwa dharau na kebehi. "Huwa nafurahia zaidi kuwaua watu wangu kwa mikono," alisema akizidi kusogea.

Mzaha haukuwemo katika macho na sauti ya Chonde. Alionekana mtu anayejua anachokifanya, jambo ambalo lilimfanya Joram asogeze mkono kuiendea ile bastola ambayo ilikuwa imelala kando yake. Kama alikuwa ameuhisi wepesi wa Chonde basi alikuwa hajauona. Mara tu mkono huo ulipoifikia bastola tayari mguu wa Chonde ulitua juu ya mguu huo. Wakati huo huo Joram alipokea ngumi mbili ambazo zilizomfanya apepesuke na kuisahau bastola. Chonde hakuwa na roho mbaya kiasi hicho. Alimpa muda wa kujiandaa. Joram akavuta pumzi kwa nguvu na kuanza kumwendea Chonde. Alimshitua kwa mkono wa kulia, Chonde aliudaka na wakati huohuo kumkata Joram judo ya mgongo ambayo ilimfanya aanguke kifudifudi. Alipoinuka Chonde alikuwa akimsubiri huku akicheka, "Wanasema Tanzania kuna mtu mmoja tu wa kujihadhari nae, ambaye anaitwa Joram Kiango. Niko naye chumbani, sioni Ujoram wake."

Maneno hayo yalimwuma Joram zaidi ya kipigo alichopokea. Akainuka ghafla na kumwendea Chonde akitumia mitindo yake yote ya kupigana. Vipigo kadhaa vilimpata Chonde. Lakini kwa jinsi vipigo hivyo vilivyopigwa kwa hasira havikuwa na madhara makubwa kwa Chonde. Dakika chache baadaye Joram alijikuta chali sakafuni, kasalimu amri. Chonde akaendelea kutabasamu.

Sasa Joram alimtazama Chonde kwa mshangao zaidi ya hasira. Ni mtu wa aina gani huyu anayeweza kumwadhibu kama mwanae? Bila shaka si mtu wa kawaida. Amejifunza mengi kama anavyoonekana kujua mengi. Pamoja na kwamba kipindi kirefu kilikuwa kimepita bila ya Joram kufanya mazoezi ya viungo wala akili, pamoja na kule kuzoea starehe za mahotelini na ulevi mwingi, bado hakuona kama binadamu yeyote angekuwa na haki au uwezo wa kumfanya apendavyo kama Chonde alivyokuwa amemfanya.

Ile hamu iliyokuwa imelala usingizini ikaibuka upya katika moyo wake, hamu ya mapambano, vitisho, maafa, damu, na mikasa, hamu ya kuwatia adabu watu wanaopenda kuwafanya vibaya binadamu wenzao. Chonde alionekana kama mmoja wao. Joram akamtazama tena na kutabasamu kwa uchungu huku akisema, "Haya, umeshinda. Kinachofuata?"

"Kifo chako," Chonde alimjibu kijeuri. "Siwapendi vijana watundu kama wewe. Kufa, huna budi.”"Kosa langu."

 "Unapenda kufa?"

Joram alifikiri kwa makini angefanya nini kuiahirisha hukumu hiyo ya kifo. Muda. Alihitaji muda ili ikiwezekana itokee njia moja au nyingine ya kuyaokoa maisha yake. Akaanza maongezi kwa sauti ambayo aliifanya dhaifu kuliko ilivyokuwa, akimwuliza Chonde hili na lile. Chonde alikuwa mgumu wa kutoa habari kama jabali. Kati ya maneno ya kashfa na matusi kwa Joram, nchi na bara zima hakutamka neno lolote ambalo lilimfanya Joram amjue yeye ni nani na anafanya nini katika ulimwengu wa ujasusi. Alichoambulia ni zile hisia tu kwamba Chonde hakuwa raia wa kawaida.

"Umeahirisha sana kifo chako," Chonde alisema baadaye kama aliyekuwa akizisoma fikra za Joram. “Sasa iliyobaki ni kazi ndogo ya kukutoa uhai. Nitakuua kwa mkono wangu wa kushoto. Maiti yako itaokotwa kesho ikiwa imevunjikavunjika kama mtu aliyeanguka toka ghorofani. Kwa jinsi ulivyobadilika kitabia watu hawatashangaa kusikia kuwa umejirusha dirishani.”

Baada ya maneno hayo, aliinuka na kumwendea tena Joram kwa utulivu kama awali, lakini macho yake yalitangaza kitu kimoja tu, kifo.

Joram alijiandaa, akijua kuwa vita vilivyokuwa mbele yake vilikuwa vikubwa kuliko vyote alivyowahi kupambana navyo, vita vya kuitetea roho yake. Akaikusanya akili yake yote na kumsubiri Chonde kishujaa.

Mara mlango ukagongwa.

Chonde aligutuka kwa mshangao na kuutazama mlango huo. Joram hakuipoteza nafasi hiyo. Aliruka na kuufanya mguu wake utue katika shingo ya Chonde. Lilikuwa pigo ambalo Chonde hakulitegemea. Likamtia mweleka. Lakini pigo la pili alilitegemea, akalikwepa na kuachia judo ambayo Joram aliikinga. Papo hapo mlango ukagongwa tena na kufunguka ukiruhusu sura ya msichana mzuri kuingia.

Alikuwa yule msichana wa mapokezi wa hoteli ya Embassy. Alitokwa na macho ya mshangao kuona miili yenye jasho, michubuko na damu, ya wanaume hao, ikiwa tayari kuvamiana. Wote walimtazama msichana huyo, Chonde akimlaani, Joram akimshukuru. Akiwa kama hajui lipi la kufanya msichana huyo aliduwaa mlangoni, Mdomo wazi.

"Karibu ndani. Tulikuwa tukifanya mazoezi ya viungo na huyo rafiki yangu," Chonde alimhimiza akivaa tabasamu ambalo lilificha kabisa mauaji yaliyokuwa katika uso huo dakika iliyopita. "Karibu ndani. Nawe ndugu yangu nenda zako sasa. Tutakutana siku nyingine".

Joram aliyarekebisha mavazi yake na kutoka chumbani humo taratibu. Hakuwa amesahau kumwachia msichana huyo tabasamu jingine la shukrani.

********

"Nadhani hakuna njia nyingine zaidi ya kumlazimisha," Kombora alikuwa akifoka katika kikao cha dharura kilichofanyika usiku huo. "Hawezi kuachwa aendelee kustarehe katika mabaa huku taifa na bara zima likiwa mashakani. Mchango wake unahitajika."

Kikao hicho kilihudhuriwa na viongozi wote wa ngazi za juu katika idara zote za usalama nchini. Kiliitishwa ghafla baada ya kuokotwa barua moja ya vitisho katika ofisi ya Waziri Mkuu, barua ambayo iliandikwa kwa ufupi sana ikidai kuwa ajali za kimiujiza zingeendelea kuipata nchi ya Tanzania na zote zilizo mstari wa mbele, endapo serikali isingechukua hatua za haraka kukomesha msimamo wake wa kupinga utawala wa kibaguzi wa Afrika Kusini. Barua hiyo iliongeza kwamba safari hii moto ungeiteketeza hospitali ya Muhimbili, hoteli ya Kilimanjaro, Jengo la Kitega Uchumi na baadae Ikulu.

Aliyeiokota barua hiyo na kuisoma aliwaonyesha wakubwa wake ambao waliikabidhi kwa Waziri Mkuu. Baada ya kuisoma yeye pia, alikwenda Ikulu ambako alimpa Rais.

"Upuuzi ulioje huu. Hatutaacha kuwatetea ndugu zetu wanaoteswa bila makosa kwa ajili ya vitisho hivi. Havikuanza leo. Wala haviwezi kwisha leo. Tutapigana hadi mtu wetu wa mwisho katika kuilinda hadhi ya mtu mweusi katika bara letu hili." Pengine Rais alijibu hivyo akifoka kwa hasira. "Barua hiyo wakabidhi watu wa usalama. Nadhani hawatakubali kuendelea kuchezewa kiasi hiki. Waambie kwamba hatutaki upuuzi wowote ulioandikwa katika waraka huu haramu utokee." Huenda Rais aliongeza hayo.

Hakuna aliyeshiriki katika maongezi yao ya faragha, isipokuwa hisia hizo zinakuja kwa jinsi Waziri Mkuu alivyomwita Inspekta Kombora katika ofisi yake na kumkabidhi barua hiyo. Baada ya Kombora kuisoma kwa makini Waziri Mkuu alimwambia, "Ni barua ya khatari sana. Na imeandikwa na watu khatari, watu wenye kichaa. Kufuatana na hali ilivyo hatuwezi kukubali kuwa watumwa au mateka wa Makaburu kwa kuhofia ukatili wa vitisho vyao. Lazima tupambane nao ana kwa ana kama tunavyopambana nao katika uwanja wa mapambano. Tuliwashinda Msumbiji, Angola na Zimbabwe. Kwa nini tusiwashinde Namibia na Afrika Kusini? Tutawashinda. Wao wanajua hivyo, ndiyo sababu inayowafanya wakimbie toka katika uwanja wa mapambano na kuja huku kupigana kiuoga."

"Kama tulivyoshuku kitambo, mikasa hii haikuwa ya kawaida. Kulikuwa na mkono wa mtu, mkono wa mtu huyu ambaye ameandika barua hii na kuthubutu kuipenyeza katika ofisi yangu. Ingawa haijafahamika mbinu gani wanatumia kuweza kuanzisha mioto hii, nadhani hutashindwa kufanya juu chini ili uugundue na kuukomesha kabisa upuuzi huu."

Akijua uzito wa jukumu hilo ndipo Kombora aliporudi ofisini na kuitisha kikao hiki kilichokuwa kikiendelea. Walijadiliana kwa mapana na marefu kulikuwa na nini hasa hata majumba yalipuke moto ilihali uchunguzi kamili ulionyesha kuwa haikuwepo kasoro yoyote ya umeme. Hawakupata jibu. Walijaribu kuzijumuisha taarifa zote za upelelezi juu ya nani anaweza kuwa alihusika katika kusababisha mioto hiyo lakini bado hazikuwepo dalili zozote zilizoleta matumaini. Wakapanga mipango mipya. Wakawaandaa wapelelezi na vyombo kadha wa kadha katika majumba yaliyotajwa. Wakawekwa watu katika mahoteli, viwanja vya ndege na vituo vyote vya usafiri kuchunguza nani anaingia, nani ametoka na ameleta nini. Zaidi ya yote hayo, ndipo lilipotolewa tena pendekezo la kumshirikisha kila mtu mwenye uwezo wa kuchangia katika upelelezi. Hapo ndipo jina la ‘Joram’ lilipowatoka midomoni. Ikawashangaza wajumbe kusikia kuwa hata baada ya kuombwa na Kombora alikataa katakata kushiriki katika kazi hiyo. Joram waliyemfahamu alikuwa hangoji kuombwa au kutumwa bali alijituma. Vipi Joram huyu?

Ndipo mzee Kombora alipoibuka na uamuzi wa kumshurutisha. "Lazima tumlazimishe. Kama ameacha upelelezi kwa ajili ya mwanamke, basi atarudia upelelezi kwa ajili ya mwanamke. Yote hayo niachieni mimi," Inspekta Kombora aliwaambia.

Baada ya kikao hicho, alimchukua msaidizi wake mmoja na kumpeleka chemba. "Sikia," akamweleza, "Nakutaka uwe msiri wangu, wewe peke yako. Unaweza kutunza siri?"

"Bila shaka. Isipokuwa ya wizi na mauaji tu."

"Hii si ya mauaji wala wizi. Nataka unisaidie kumteka mtu nyara."

"Kuteka mtu nyara? Hiyo mbona haiko mbali sana na wizi? Na kama sikosei ni hatari zaidi ya wizi."

"Ndiyo. Lakini mtu tunayemtaka atafurahi sana. Bado ni msichana mzuri sana," Kombora alivuta pumzi kwa nguvu kisha akaongeza, "Nataka tumteke yule msichana wa Joram. Hiyo ndiyo njia pekee ya kumlazimisha."

Baada ya kujadiliana kwa muda walielewana. Wakaandika barua ambayo ilikusudiwa iwe imetoka kwa mteka nyara akidai kuwa amemteka msichana huyo na angemwua endapo Joram angethubutu kujihusisha na upelelezi unaoendelea nchini dhidi ya maafa ya kutatanisha. Licha ya barua hiyo, pia waliandaa damu ambayo ilipatikana kwa msaada wa daktari mmoja wa hospitali yao Ocean Road ili waidondoshe chumbani humo kuonyesha kuwa kulikuwa na mapambano ambayo yalisababisha damu kumwagika.

"Tunacheza mchezo mchafu sana, mchezo wa aibu. Lakini hatuna budi," Kombora alisema baada ya matayarisho yote ya kwenda katika chumba cha Joram.

Uchunguzi uliwapa fununu kuwa Joram alikuwa akiishi katika hoteli hiyo ya Embassy. Habari za mwisho usiku huo zilieleza kuwa Joram alipoachana na Kombora usiku huo alikuwa peke yake akinywa bia wakati msichana wake alipoondoka kwenda chumbani, na kwamba baada ya muda mrefu Joram alionekana akitoka nje na hadi sasa alikuwa hajarudi. Kombora alitegemea kuwa muda huo ulitosha kumfikia msichana huyo, kumshawishi na akikataa, kumlazimisha kisha kuondoka naye kwa siri kabla Joram hajarudi.

Walifanya hivyo.

Waliifika hoteli na kukiendea chumba chake kwa siri kubwa. Mlango waliukuta ukiwa wazi. Wakaufungua na kuingia huku wakiufunga nyuma yao. Macho yao yalivutwa na dalili za vurugu katika chumba hicho. Vitu vilikuwa vimetupwa ovyoovyo, matandiko yakiwa yamepinduliwa na masanduku kufunguliwa. Juu ya meza kulikuwa na karatasi yenye damudamu. Upande wa pili wa karatasi hiyo kulikuwa na maandishi ambayo yalikuwa barua ya wazi kwa Joram Kiango, barua ambayo haikutofautiana sana na ile ambayo Kombora aliiandaa: Ndugu Joram,

Tunayo furaha kukufahamisha kuwa tumemchukua msichana wako na tutakuwa nae hadi hapo tutakapomaliza shughuli zetu. Hii ni kwa ajili ya kukuonya usithubuti kujihusisha na mambo yoyote yanayoitokea nchi hii. Endapo utakuwa mtoto mtiifu kama ulivyo siku hizi, hatadhurika, nawe utakuwa salama. Vinginevyo, utakipokea kichwa chake kwa njia ya posta na kisha kitafuata kifo chako.

Amri

Kombora aliisoma tena barua hiyo, kisha akamgeukia msaidizi wake na kumnong'oneza, "Tumechelewa sana. Wenzetu wametuwahi." akampa barua hiyo ili aisome.

"Sasa tutafanya nini?" askari huyo aliuliza baada ya kuisoma.

"Rudisha kila kitu kama kilivyokuwa. Fanya hima tuondoke hapa haraka," alimhimiza akianza kusogea mlangoni.

"Nilidhani tungemsubiri Joram!"

"Hakuna haja. Akirudi atajua la kufanya." Wakatoka na kuifuata njia ya kawaida. Wakiwa katika mavazi ya kiraia, watu wachache sana waliwatupia macho zaidi ya mara moja. "Jambo moja la kupendeza ni kwamba," Kombora alikuwa akisema. "Wamemchokoza Joram. Hawamfahamu vizuri. Wataujutia uamuzi wao"

ITAENDELEA....................

Post a Comment

0 Comments